https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, April 06, 2013

Yanga sasa waichokonoa klabu ya Simba



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
UONGOZI wa klabu ya Yanga, umesema katika adhma yao ya kujenga uwanja mpya wa kisasa hawataangalia nyuma, hata kama watani zao wa jadi, Simba SC watachekwa au kupalilia migogoro ndani ya klabu hiyo, inayoongozwa na Ismail Aden Rage.
Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako
Yanga inatarajia kuingia mkataba wa kujengewa uwanja wao na Kampuni ya Beijing Construction Engineering Group mwishoni mwa mwezi wa tano na kupokelewa kwa shangwe na wanachama na mashabiki wa timu hiyo inayoongozwa na Yusuph Manji.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto, alisema kuwa hawataangalia nyuma kwa ajili ya kutimiza malengo ya klabu yao kuwa na uwanja wa kisasa na wenye hadhi ya kufanana na timu yao.

Alisema ingawa kukamilika kwa uwanja au dalili njema za kujengwa kwake kutaibua migogoro zaidi kwa watani zao Simba, ila hilo litakuwa jambo jingine na litapaswa kushughulikiwa na wenye klabu yao.

“Hatutaki utani katika suala hili, ndio maana tayari tumeshakaa na wenzetu wa Beijing kwa ajili ya kushusha uwanja wenye hadhi na kuitangaza Yanga katika maendeleo ya soka duniani.

“Wale watakaolumbana kwasababu ya maendeleo yetu watajua wenyewe, ila kila mtu anapaswa ajuwe kuwa wanachama, mashabiki na wadau wote wa Yanga tumeungana katika jambo hili la maendeleo,” alisema.
Katika kikao cha kuonyesha ramani ya uwanja huo wa kisasa utakaojengwa katika eneo la Jangwani City, Uwanja wa Kaunda, kiliwakilishwa na Mjumbe wa Bodi ya Udhamini ya Yanga, Francis Kifukwe, Lawrence Mwalusako na viongozi waandamizi ndani ya klabu hiyo.

MWISHO


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...