https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, April 15, 2013

Extra Bongo wafanya balaa Garden Breeze Magomeni



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
BENDI ya Extra Bongo, maarufu kama Next Level Wazee wa Kizigo, Jumapili ya jana walifanya balaa katika viwanja vya Garden Breeze Magomeni kwa kuwapatia mashabiki wao shoo ya ukweli na ya aina yake na kuwaacha watu hoi.
Wanenguaji wa Extra Bongo wakiwa jukwaani

Shoo hiyo iliongozwa na Mkurugenzi wao Ally Choki, akishirikiana na wanamuziki mahiri wa bendi hiyo, akiwamo Banza Stone, Khadija Kimobiteli, Rogati Hega Katapila na wengineo.
Mkurugenzi wa Extra Bongo, Ally Choki
Kama kawaida, shoo hiyo ilianza jioni kwa wadau na mashabiki kujivuta katika viwanja hivyo vilivyoanza kujizolea umaarufu kwa kuhusisha bendi mbalimbali zinazofanya vyema katika tasnia ya muziki nchini.

Ingawa nyimbo na aina ya uimbaji wa Extra Bongo ilikuwa nzuri na kufurahisha watu wote, lakini safu ya wacheza shoo wa kike na wa kiume wakiwa chini ya kiongozi wao Super Nyamwela jana walitulia zaidi na kufanya viwanja hivyo vitawaliwe na kelele za furaha.

Takribani dakika kumi na ushee kwa kila safu upande wa wanawake na wanaume walitumia kuwa kuwa jukwaani kuonyesha uwezo wao na kuwafanya watu washindwe kukaa vitini mwao, huku wengine wakiacha viti vyao na kukimbilia mbele ili waone vizuri.

Akizungumzia shoo hiyo, Mkurugenzi wa Extra Bongo, Ally Choki alisema kwa sasa hakuna maneno zaidi ya vitendo kwa ajili ya kuonyesha ubora wao katika tasnia ya muziki wa dansi nchini.

“Sisi ni kazi maneno waseme wao, hivyo kwa sasa tutaendelea kufanya mambo makubwa ili kuwavutia mashab iki wetu na hakika lazima waseme kitu juu yetu,” alisema Choki.

Extra Bongo ni bendi inayofanya vyema katika tasnia ya muziki wa dansi nchini huku ikiheshimiwa kutokana na mikakati yake ya kujiimarisha kileleni.


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...