https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, April 21, 2013

Balozi Kagasheki: Wanasiasa wananufaika na mgogoro wa Hifadhi za Taifa, Loliondo



Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MARA kadhaa migogoro baina ya wananchi na Serikali huweza kuchochewa na wanasiasa, Taasisi zisizo za Serikali na za Serikali yenyewe lakini ikiwa na malengo ya kila kundi kujinufaisha lenyewe kiuchumi, kisiasa.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki
Makundi kama ya NG’O hujitokeza kwa wingi pale yanapoona sehemu yenye mgogoro ina maslahi kwao na sehemu ya kuweka huruma mara kadhaa imekuwa ni ndogo kuliko maslahi binafsi au ya taasisi husika.
Hali hii mara nyingi hujitokeza hasa panapokuwa na migogoro ya ardhi baina ya wananchi na wawekezaji utakuta NG’O zinarundikana na kuanza kuhamasisha wananchi kufanya vurugu zisizokuwa na mantiki ya kuendeleza kijiji au sehemu husika kwa maslahi ya taifa na kijiji chenyewe.

Kwa takribani miaka 20 sasa eneo la Loliondo limekuwa na migogoro ya muda mrefu inayotokana na muingiliano wa matumizi ya ardhi katika eneo lililotengwa na kutangazwa na serikali kuwa la Pori Tengefu la Loliondo.
Hata hivyo hakuna asiyefahamu  kuwa  mrundikano wa NG’O zaidi ya 30 ni kutokana na kutaka maslahi  binafsi au ya taasisi kwa kua Hifadhi ya Taifa ya Serengeti; Tarafa ya Loliondo inajumuisha Pori Tengefu (Loliondo Game Controlled Area –LGCA) eneo ambalo  lenye vitega uchumi vingi.
Baadhi ya vitega uchumi katika eneo hilo ni la wawekezaji wa Otterlo Business Corporation Ltd (OBC) ambao walifanikiwa kupata kibali cha uwindaji katika hifadhi hiyo.

Thomson Safaris ambao  wanaendesha shughuli zao za utalii wa asili katika maeneo ya Sukenya, Soitsambu. African Safari | Mount Kilimanjaro Climb

Dorobo Tours and Safaris ambao wanaendesha utalii wa kiikolojia.
Sokwe Asilia hawa wanaendesha kambi za kudumu za muda Nomad Safaris: Kampuni hii inamiliki kambi lakini hizi ni baadhi tu ya kampuni.

Kutokana na hali hiyo inanisukuma kusema kuwa wawekezaji hawa wako katika ushindani mkubwa  ikiwa ni pamoja na kwenye  maslahi kutokana na suala zima la kiutalii, mapambano katika uchumi  na kila mmoja kupigania kupata eneo kubwa la Loliondo.
Kutokana na masuala hayo yote kuna kila sababu ya hawa washindani kuwatumia wanasiasa katika kuhakikisha kuwa wanalinda maslahi yao binafsi na hata kuwatumia viongozi wa vijiji na wananchi  ili kila mmoja aweze kuvutia kwake kwani waswahili wanasema kila mwamba ngoma huvutia kwake na hivyo ndivyo ilivyo kwa mgogoro huu wa Loliondo eneo ambalo lina vivutio  vizuri vya kiutalii.
Loliondo imekuwa ni sehemu ya mgogoro mkubwa ambao umekuwa ukiundiwa tume kwa takriban mara mbili mfululizo inakua na majibu lakini hatua madhubuti ya kuunusuru mgogoro huo kutochukuliwa na hii husababisha kadhia na vurugu kuchukua nafasi yake.
Katika taarifa ya tume ya uchunguzi ya mwaka 2009 iligundua kuwa NGOS zisizo za Serikali kuwa ndio sababu kubwa ya kueneza chuki na hata kusababisha mapigano baina ya wananchi na kampuni ya uwindaji wa kitalii ya Ortello Business Cooperation (OBC) ya Falme za Kiarabu (UAE).
Lakini kutokana na hali ya mgogoro kuendelea  Waziri wa Maliasili na Utalii Balozi Khamisi Kagasheki aliona ni vyema kuweza kuufanyia utatuzi wa haraka ili wananchi waweze kuishi kwa amani na furaha huku wakifurahia matunda ya wawekezaji wao.
Waziri alifanya ziara katika eneo hilo kwa takribani  mara tatu kuzungumza na wananchi na mwekezaji wa OBC ili kujua chanzo na kulipatia ufumbuzi suala hilo.
Hata hivyo katika hali isiyo ya kawaida wanasiasa ,NGO wamekuwa katika mstari wa mbele kuhakikisha wanaweza kuingilia majadiliano hayo ya amani kwa maslahi yao na si kwa maslahi ya Wananchi.
MAJIBU YA ZIARA YA WAZIRI LOLIONDO
Hata hivyo katika ziara zake hizo naye amegundua kuwa wanasiasa wamekuwa katika mstari wa mbele kuhamasisha vurugu kutokana na kulinda mtaji wa kura 2015 jambo ambalo alisema si sahihi na kwamba halitakiwi kufumbiwa macho hata kidogo.
Anasema migogoro iliyopo Loliondo  imejenga hisia zisizo sahihi kwa watanzania na hata wengine katika jumuiya za Kimataifa na ilikua vema kupata ufumbuzi wa kudumu wa migogoro ya ardhi katika eneno hilo.
Hata hivyo anasema kuwa ili kunusuru ikolojia ya Hifadhi za Serengeti ,Ngorongoro  na pori Tengefu Loliondo, Serikali itatenga sehemu ya ardhi ya pori tengefu la Loliondo yenye ukubwa wa Kilomita za mraba 1,500 kutoka kwenye eneo la kilomita za mraba 4,000 za pori hilo itakayoendelea kuwa na hadhi ya pori tengefu kwa ajili ya kulinda  mazalia ya wanyamapori,mapito na vyanzo vya maji kwa ajili  ya ustawi wa hifadhi hizi kwa manufaa ya wananchi wenyewe na taifa kwa ujumla.
“Serikali itasimamia eneo litakalobaki kuwa pori tengefu kwa mujibu wa sheria za uhifadhi wa wanayamapori na ardhi itakayobaki baada ya kuondoa eneo la pori Tengefu Loliondo itasimamiwa na vijiji kwa mujibu wa sheria ya ardhi ya kijiji namba 5 ya mwaka 1999,”anasema Kagasheki.
Anasema baada ya hapo wananchi watawezeshwa kuanzisha eneo la jumuiya la hifadhi ya wanaymapori (WMA) katika ardhi itakayobaki kuwa ardhi ya kijiji kwa mujibu wa sheria ya ardhi .
Nasema pia mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji katika eneo la Loliondo utaandaliwa na utaambatana na huduma za mifugo ndani ya vijiji,kwa mfano wa majosho ,malambo ya maji ya mifugo ,minada na mengineyo.
Alisisitza kuwa msisitizo wa serikali ni kuwataka wafugaji kufuga kisasa zaidi kufuga mifugo inayoendana na ukubwa wa eneo la malisho lililopo katika kijiji husika ambapo sheria ya kudhibiti idadi ya mifugo itakayoruhusiwa kwa mujibu wa uwezo wa eneo la malisho kumudu itazingatiwa ili mifugo isizidi kwenye eneo husika pia.
Hata hivyo kulikuwa na tamko ambalo lilitolewa na wananchi ,viongozi wa kisisa na wanaharakati kwa serikali halikuwa sahihi lakini pia imeona kuna haja ya kuangalia upya eneo alilopewa mwekezaji OBC na hata ikibidi kupunguizwa ili wananchi wapate maeneo hayo.
Waziri Kagasheki pia aliwataka wananchi kutii sheria bila shuruti kuondoka katika maeneo tengufu huku akisema kwa sasa hakuna kubembelezana ni wakati wa kufuata sheria.
Lakini alifika mbali zaidi na kuzishangaa NGO mbalimbali ambazo anasema zafikia 30 kujiweka katika eneo hilo kwa ajili ya kuchochea vurugu kwa maslahi yao na si ya wananchi.
Kutokana na hali hiyo alizitaka NGO kuachaa kuchochea wananchi vurugu na badala yake kuhamasisha amani na uwasaidia wananchi njia mbadala za kupata maendeleo.
Lakini pia anashangazwa na kitendo cha eneo kubwa la Loliondo kukaliwa na kuendeshwa shughuli zake na kabila la watu wa kimaasai ambao ni wafugaji na ndio ambao wamekuwa pia kichocheo kikubwa cha vurugu hizo.   
“Hii haikubaliki hata ,hivi kwa mfano ingetokea wafugaji wakitanzania wangejaa kule Kenya wale wangekubali sidhani kama watakubali na hii inatokana na Kenya kuwa na uhaba mkubwa wa ardhi, lakini si vizuri kuwabagua ila wasianzishe vurugu kwa maslahi yao huku wakijua wanaloliondo wanategemea watalii katika kukuza uchumi pia,”anasema Kagasheki.
Vyombo mbalimbali vya habari vilikariri uongozi wa Kampuni ya Ortello Business Corporation (OBC),kwa kusema kuwa  maslahi binafsi yakiwemo ya wanasiasa na baadhi ya watendaji serikalini, ndiyo chanzo cha mgogoro unaoendelea katika eneo tengefu la ardhi la Loliondo ambako kampuni hiyo imepewa kibali cha kuwinda.

Mkurugenzi wa OBC Tanzania, Isaac Mollel, amesema, maslahi hayo binafsi yanachangia kuwepo kwa mgogoro huo, lakini kama sheria zikifuatwa, hakutakuwa na mgogoro katika eneo hilo ambalo Ortello imekuwa ikiendesha shughuli zake kwa kibali cha serikali tangu mwaka 1993.

Mollel anaungana na kauli ya Waziri Kagasheki na kusema kuwa mgogoro huo hutokea pindi Serikali inapotaka kugawa vitalu na kila watanzania wakijiandaa kwa Uchaguzi Mkuu, akitolea mfano wa mwaka 1993 na sasa watu wanapolekea uchaguzi wa mwaka 2015 .

Anasema,kwa kuwa Kenya ardhi ni tatizo, wapo baadhi ya watu kutoka nchi hiyo ambao wengi ni wa jamii ya wafugaji wa Kimasai, wameingia Loliondo na kuchukua ardhi, na kusababisha mtafaruku kwa jamii ya wenyeji.


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...