https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, April 23, 2013

SIWEZI KUVUMILIA


Timu zetu ziwe na uchu wa mafanikio
Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
INASIKITISHA kuona bado tunaendelea kuwa wale licha ya kufanikiwa na kuwa na wachezaji wazuri wenye vipaji vya aina yake katika suala zima la michezo, ukiwapo mpira wa miguu.

Tanzania hii yenye kila aina ya vipaji, lakini tunapokuwa kwenye mipango ya kimaendeleo, tunakwama na kuonyesha kuwa kumbe dhamira zetu ni kutesa katika soka la ndani na sio nje ya nchi.
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage
Kwa bahati mbaya, hali hii zaidi huchochewa na viongozi wetu wanaofanikiwa kuwa kwenye klabu za soka; wale ambao mawazo yao huwa ni mepesi kwenye uongozi wao.
Rais wa TFF, Leodgar Tenga
Hili si jambo zuri katika kuhakikisha kuwa Tanzania yetu inapiga hatua katika medani ya kandanda. Katika kulisemea hilo, sitaacha kuishukuru na kuipongeza timu ya Azam ambayo inaonyesha uchu wa kusonga mbele Kimataifa, lakini kazi ipo kwa wanaoona kuwa wenye haki hiyo ni klabu za Simba na Yanga tu.

Mlinda mlango wa Simba, Juma Kaseja
Hii siwezi kuvumilia. Nikiwa kama mdau wa michezo, ni vyema sasa watu tukabaini kuwa jambo kubwa linalozifanya timu zetu, hasa za Simba na Yanga zishindwe kufanya vyema ni kutokana na kupatikana viongozi wasiokuwa na malengo.
Mwenyekiti wa Yanga, Yusuph Manji

Viongozi ambao lengo lao kubwa ni kuhakikisha kuwa wanajiwekea mazingira ya kunyenyekewa na kuonekana wao bora, jambo ambalo hakika likiendelea kuachwa kama lilivyokuwa bado hatutaweza kuvunja mwiko wa kusonga mbele Kimataifa.

Huo ndio ukweli. Kwa mfano, Simba inaweza kusajili wachezaji 30, lakini kati ya wote waliosajiliwa, wapo kwa ajili ya watu Fulani ndani ya timu hiyo, kwakuwa ndio waliolipa fedha.

Inapotokea kutoelewana, bosi aliyemsajili mchezaji husika, huweza kutoa amri ya kucheza chini ya kiwango, jambo ambalo huchangia kuvurunda kwa timu zetu mara kwa mara.

Hali hii haipo Simba tu. Bali Yanga mara kadhaa imekumbwa na suala hili, kabla ya kumchagua mwenyekiti wao mpya, Yusuph Manji, ambaye naye amekuwa akiingiza watu kwenye mfumo wa uongozi, akiwapo mtoto wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ridhiwan Kikwete, aliyepewa cheo cha Mwenyekiti wa Maendeleo ya Jengo la Mafia.

Ndio maana nasema, kama hatutakuwa na viongozi wenye mipango ya kweli hatuwezi kufanya vyema kamwe. Viongozi wanaowaza maisha yao na si klabu zao hapo hakuna kitu.

Kwa mwaka huu timu ya Simba inaonyesha haina hata uwezo wa kuchukua nafasi ya tatu kama si ya pili kutokana na ugumu wa mechi zilizosalia na mikakati ya wapinzani wao.

Itakuwa ngumu Azam wajibweteke hadi wapitwe na Simba, au Yanga wajilegeze na kulikosa taji hilo la Tanzania Bara. Itakuwa ni ndoto ya mchana na haiwezi kutokea.

Ukiangalia kwa karibu, Simba inayoongozwa na mwenyekiti wake, Ismail Aden Rage, mwaka wote huu imekuwa kwenye migogoro isiyokwisha, tena inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na Rage.

Hii ni kwasababu amekuwa akitoa kauli za kejeli, dharau na kudanganya, hali ya kuwa anafahamu kuwa klabu ya Simba ni mali ya wanachama na sio ya mtu mmoja.

Naweza kusema kuwa Rage hajaweza kusimamia vyema nafasi yake ya uongozi kwa mwaka huu wote. Mara nyingi amekuwa kwenye mambo yake binafsi ukiwapo ubunge.

Hii ni jambo linalotakiwa liangaliwe kwa manufaa ya klabu za Tanzania, hasa kwa kuhakikisha kuwa zinakuwa na viongozi wenye mipango mizuri kwa maendeleo yao.

Ni bora tuambiane ukweli, japo mara kadhaa huibua malumbano au kutokuelewana na wadau hao. Tunataka mafanikio na sio ubabe wa Tanzania pekee.

Kwangu mimi siumii kuona Simba haijachukua Ubingwa wa Bara msimu huu, bali nitaumia zaidi kuona hata hao Yanga watakaofanikiwa kupata taji hilo, hawatakuwa na cha maana katika michuano ya Kimataifa, Ligi ya Mabingwa Afrika.

Hawa ni wazee wa mechi moja nje. Si Simba wala Yanga. Kwenye michuano ya Kimataifa, hulitia aibu Taifa, maana mipango yao inakuwa bure kabisa, ndio maana siwezi kuvumilia.

Nadhani huu ni wakati sasa wa watu wote wakiwapo viongozi wa klabu za soka Tanzania kuona hakuna muda wa kupiga porojo zaidi ya kutenda kazi zenye manufaa.

Kama wachezaji wazuri wapo, ndio maana wanafanikiwa kuonyesha uwezo wao Afrika, akiwamo Mbwana Samatta aliyetokea Simba na sasa anaipaisha mno timu ya TP Mazembe.

Wapo wachezaji wengine ambao ni Watanzania wanaocheza soka nje ya nchi, hivyo kuonyesha kuwa viongozi wa soka Tanzania wanashindwa kuwatumia kwa kuweka mipango thabiti yenye kuleta tija, zaidi ya kuwaamuru wacheze chini ya kiwango, kufungisha inapotokea migongano ya kimaslahi.

Kazi kweli kweli.
0712 053949
0753 806087


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...