https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, April 17, 2013

Ni Bunge la utani, vitimbwi na porojo



MGODI UNAOTEMBEA
Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
SASA nimepata picha kamili kwanini Ofisi ya Bunge walikuwa na mpango wa kusitisha matangazo ya moja kwa moja ya vipindi vya Bunge vinapofanyika mjini Dodoma.
Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM), Murtaza Mangungu
Ni dhahiri Ofisi ya Bunge ilijua mengi na kuhitaji kuficha aibu inayoweza kujitokeza, kama hii ya kuendelea kusikiliza maneno ya dharau, kejeli na mengineyo ya kuogofya.
Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe
Pamoja na kuwa na lengo hilo la kusitisha, lakini wanaharakati na wadau wengine walikuwa wakali kama mbogo. Kila mmoja aligoma na kushangaa pia uamuzi huo.
 John Mnyika, Mbunge wa Ubungo kwa tiketi ya Chadema

Wengine waliupachika jina la kandamizi la uhuru wa habari kwa wananchi juu ya Bunge lao. Ati maneno haya yalitolewa na waliotaka utaratibu wa kurushwa moja uendelee kuwapo.

Ni sawa, ila kwa jinsi hali ya mambo inavyoendelea, wakati mwingine nasema bora hata vipindi hivyo vizimwe tu. Havina faida tena na Watanzania.


 Ismail Aden Rage, Mbunge wa Tabora Mjini kwa tiketi ya CCM
 Profesa Maji Marefu, Mbunge wa Korogwe Vijijini kwa tiketi ya CCM
 Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Kaskazini kwa tiketi ya Chadema
Waziri Mkuu wa zamani na Mbunge wa Monduli kwa tiketi ya CCM, Edward Lowassa

Zaidi watu wanajifunza maneno machafu kutoka kwa watu ambao eti jamii inawategemea wao. Hili ni sawa na kusubiri embe chini ya mwarobaini. Wakati nasema haya, nakumbuka mzigo mzito wa maisha magumu yanayoendelea kumkumba Mtanzania.

Maisha yamekuwa magumu na hakuna tena ahueni. Sio mjini wala vijijini. Kote hali ni tete. Kwa mfano, licha ya kipato cha wananchi wengi kubaki kama kilivyo, lakini bidhaa zimekuwa zikipanda juu kama ulivyokuwa Mlima Kilimanjaro.

Leo nauli za mabasi yaendayo mikoani imepanda mara dufu bila kusahau za daladala ambazo nyingi hazina ubora. Nyingine viti vinachana nguo za abiria, lakini mwisho wa siku nauli 4oo kutoka Kimara hadi Ubungo lazima ilipwe na kama mtu hataki atembee kwa miguu na sijaona wabunge wakisimama kwa kauli moja kupinga ongezeko la nauli maana lipo kwa ajili ya kuwakomoa zaidi Watanzania.

Nilitarajia wabunge wote wangepinga kwa vitendo na kuwatetea Watanzania, maana wanajua jinsi maisha yalivyokuwa magumu zaidi ya wao walivyolia mwaka jana bungeni na kuomba waongezewe posho ambapo baadaye Zitto Kabwe, aliziponda kwa nguvu kwa madai zinanufaisha wabunge na sio wananchi.

Pamoja na mzigo huo wa nauli, bado zipo bidhaa ambazo ni ngumu kuzipata kiurahisi kama huna kitu. Unga uliokuwa unauzwa Sh 200 hadi 300 mwaka 2007 sasa unauzwa kwa Sh 1500, wakati vitu kama vile sukari, mchele vikionekana kama vile ni anasa.

Kwa kuliangalia hili, mimi nilidhani wabunge wetu wangetumia jambo hili kuwaza namna gani ya kuwakomboa watu wao na sio kukaa kwenye viti vya kuzunguuka na kusuta umbea.

Je hicho ndio kilichowapeleka bungeni? Je, fedha za umma ndio matumizi yake hayo? Katika jambo hilo hakika ifikie wakati wabunge wetu waone haya na kushikwa na uzalendo na Taifa lao.

Wasipoteze muda kujadili vitu visivyokuwa na msingi wakati wapiga kura wao, wawakilishi wao wanakufa njaa. Kwa Tanzania ya leo yenye changamoto lukuki hatuhitaji kupoteza muda hata robo.

Kauli kama hizi za ‘Siongei na mbwa bali na naongea na mwenye mbwa zinaashiria kitu gani’. Wengine wanafika mbali zaidi kwa kutamka maneno ambayo ukiyatafakari kwa kina utagundua kama sio matusi, basi hayapo kwenye kundi la wastaarabu.

Hii sio haki na haipendezi hata kidogo. Kwanini nasema hivyo? Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Tanzania (CAG), Ludovick Utouh, amesema kuwa ndani ya serikali kuna ufisadi wa kutupwa unaohitaji kudhibitiwa kama lengo ni kupiga hatua kimaendeleo kwa kusimamia vyema rasilimali zake badala ya kutegemea wahisani.

Kwa sasa wahisani mbalimbali wanategemewa kuchangia bajeti ya Tanzania kwa asilimia 30.

Mbali na ufisadi huo uliozungumzwa na CAG, bali pia ripoti inasema kuwa deni la Taifa limekuwa kwa kasi ya ajabu na kufikia Shilingi Trilioni 22, huku mwendo wake ukishindwa kueleweka.

Aidha pia kuna tatizo kubwa la Mfuko wa Pensheni wa Mashirika ya Umma (PSPF) zaidi ya Shilingi Bilioni 20 bila kuwapo mtiririko mzuri wa kulipwa fedha hizo ambazo ni michanago ya watumishi wa umma.

Haya ni kati ya mambo ambayo wabunge wetu walistahili kuyavalia njuga na sio kukalia kazi ya kupeana maneno ya kejeli na dharau. Watu waamini nini juu ya utendaji kazi wao?

Watanzania watakuwa na imani ya dhati na baadhi ya wabunge ambao hakika uwepo wao hauna faida. Sio siri, wapo baadhi ya wabunge ambao hata wasingekuwapo, wananchi wanaona wangeweza kujiendesha.

Kama hivi ndivyo, ina maana heshima tena hawana. Hata wapiti mbele za watu, ila wenye akili zao wanaona hakuna cha maana anachoweza kuambiwa au kufanyiwa zaidi ya kusikia maneno mitihiri ya waimbaji wa taarabu kutoka katika baadhi ya vinywa vya wabunge wetu.

Je hili ndilo kusudio? Sikatai kuwa kuepuka mabishano kati ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Chama Cha Mapinduzi (CCM) ni kazi kubwa, ila ukiwekwa uzalendo hilo linawezekana.

Linapojadiliwa suala la Watanzania, kila mtu ajuwe kuwa si kila Mtanzania ni mfuasi wa CCM au mfuasi wa CHADEMA, bila kusahau wale wa CUF, TLP na vyama vingine vya siasa.

Katika kulijua hilo, wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, iwe ni Zitto Kabwe, John Mnyika, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’, Murtaza Mangungu, Idd Azzan, Deo Filikunjombe, Mussa Azzan Zungu na wengineo lazima wahakikishe kuwa wanaitendea haki nchi yao.

Angalia, kwangu mimi mbunge makini ni yule anayepigania wananchi na sio kutoa maneno machafu kwa ajili ya kutetea mkate wake au chama chake cha siasa.

Huo ndio ukweli wa mambo. Tukifanya hivyo tutaweza kuinua ari ya utendaji kazi kwa Watanzania wote, maana viongozi wao watakuwa wameshajitambua pia.

Kinyume cha hapo hakuna jipya. Tutakuwa na Bunge la porojo wakayi utendaji kazi ukiwa sifuri. Tutasikia maombi ya miongozo, kanuni za Bunge, lakini yote si kwa ajili ya Taifa letu.

Kelele hizo kutoka katika vinywa vya waheshimiwa hao zitaishia kwenye matusi kuitana ‘boya’, mwingine anamwambia mwenzake kazi yake eti ni kujamba jamba tu, kweli?

Ndio kazi nzuri ya waheshimiwa hawa? Katika kulifuatilia zaidi Bunge hili nakumbuka kauli ya Mbunge wa Kinondoni, Idd Azzan kuwa watu wenye nia ya kugombea ubunge eti lazima kwanza wapiti JKT.

Kwa madai huko watafindishwa uzalendo. Sawa, kauli nzuri kutoka kwa Mbunge huyu, ila pia anapaswa kujua kuwa tatizo la Taifa letu ni mfumo mbovu pamoja na watu kutokuwa na mapenzi mema na nchi yao.

Uzalendo mzuri zaidi mtu anajifunza tangu chekechea, shule ya msingi au sekondari. Kama ukiona hadi amefika chuo hana uzalendo kamwe hawezi kuupata JKT.

Si kwamba utaratibu huo ukiwekwa hawatakwenda. Watakwenda, lakini si kutafuta uzalendo bali CV za kuwawezesha kugombea Ubunge kama njia yao ya kuwapatia wanachokihitaji.

Hatuwezi kwenda hivyo. Ndio maana naendelea kuwaza kila sekunde juu ya mwenendo wa wabunge wetu. Mara nyingi napatwa na hofu, je, tutarajie kuvunjwa kwa viti Bungeni siku wabunge hao watakavyoanza kushikana mashati na kutwangana makonde?

Kumbe je? Mbona maneno ya shombo yanatoka katika vinywa vya wawakilishi hao wa wananchi bungeni? Je, siku hiyo Lameck Mwigulu Nchemba atavovaana na Freeman Mbowe bungeni mtaani nako hali itakuwaje?

Nahofu Tanzania kuwa nchi ya vurugu siku za usoni kama wabunge wasipokumbuka thamani ya kura za wananchi wao kwa ajili ya kuwatumikia na kuwapatia maisha bora kwa Mtanzania na sio joto, suruba, njaa, mateso wanayoendelea kukutana nayo kila uchwao.
0712 053949
0753 806087

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...