https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, April 27, 2013

RC Gama: Ushirikiano unainua maendeleo mkoani Kilimanjaro


Awataka wanasiasa wazuie juhudi za watendaji serikalini
Apania makubwa zaidi kuhakikisha mambo yanasonga


Na Mwandishi Wetu, Moshi
ILI suala ma maendeleo liweze kupatikana, hakika kunahitaji utayari wa kujitolea, uvumilivu na uwajibikaji kutoka kwa jamii yote pamoja na ushirikiano na viongozi wao.
                    Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro, Leonidas Gama
Juhudi hizo zikifanywa kwa makini bila bila kuwapo kwa muingiliano wa majukumu au msuguano wa kifikra ni rahisi kupatikana maendeleo.
Mlima Kilimanjaro ni miongoni mwa vivutio vya Utalii mkoani humo na Tanzania kwa ujumla.
Katika kulisema hilo, Mkoa wa Kilimanjaro ni miongoni mwa mikoa inayopiga hatua kubwa kimaendeleo kutokana na ushirikiano miongoni mwa viongozi na wananchi wake.

Utekelezaji wa mipango ya ukuaji wa kiuchumi, inatekelezwa kwa kuzingatia fursa mbali mbali zinazopatikana, ikiwemo uwekezaji wa muda mfupi, muda mrefu na muda wa kati, unaoendelea kufanywa na wananchi pamoja na serikali ya mkoa.

Katika mazungumzo yaliyofanyika hivi karibuni mkoani Kilimanjaro, Mkuu Mkuu wa Mkoa huo, Leonidas Gama, anasema kuwa mipango mbali mbali ya uwekezaji na utekelezaji wake unafanikisha maendeleo.

Anasema miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na uanzishwaji wa Kituo cha Kimataifa cha Utalii, katika wilaya ya Siha kitakachokuwa kitovu kikubwa cha mapato mkoani humo.

“Mkoa pia umeanza utekelezaji wa mkakati wa kuwa na soko la kimataifa la mazao ya nafaka na mboga mboga linalotarajiwa kujengwa katika eneo la Himo, wilayani Moshi mkoani hapa.

“Katika hatua za awali za utekelezaji wa mkakati huyo tayari sekretarieti ya mkoa wa Kilimanjaro, imesaini mkataba wa mkopo wa shilingi bilioni 10 na benki ya uwekezaji ya TIB, kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu katika soko hilo,” alisema Gama.

Anasema kuwa mradi huo utaambatana na mradi mwingine wa ujenzi wa mji wa viwanda na biashara kuzunguka soko hili la kimataifa la Lokolova, ambapo pia litatoa ajira nyingi kwa wakazi wa mkoa wa Kilimanjaro.

Wakati mipango hiyo ikiendelea pia mkuu huyo wa mkoa ameendelea kutekeleza mkakati wa hifadhi ya mazingira wenye lengo la kurejesha uoto wa asili, hasa kwa kuzingatia kuwa mkoa wa Kilimanjaro ulikuwa miongoni mwa mikoa iliyokuwa inapata mvua kwa wingi.

Anasema kuwa tathmini ya utekelezaji wa mikakati hiyo inaonyesha kuwa malengo yaliyowekwa na mkuu huyo wa mkoa yanaweza kufikiwa kwa kutumia kipimo cha mafanikio ya maendeleo ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya mwaka 2005/2012 mkoani Kilimanjaro.

Katika ripoti hiyo ya mafanikio ya utekelezaji wa ilani kwa kilindi hicho inaonyesha kuwa mkoa wa Kilimanjaro umepata mafanikio makubwa katika kipindi cha miaka saba ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa mwaka 2005 mpaka 2012.

“Mkoa umekuwa ukitekeleza na kusimamia ilani hiyo ya CCM, pamoja na mpango mkakati wa mkoa wa miaka mitano kwa kuweka vipaumbele katika nyanja muhimu za kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni.

“Katika kipindi cha miaka saba ya utendaji kazi kuanzia mwaka 2005 hadi mwaka 2012, mkoa umekuwa na mafanikio makubwa katika kukuza uchumi wake na kupunguza umaskini wa kipato kwa wananchi wake,” alisema RC Gama.

Anasema kuwa sehemu ambazo zimekuwa na mafanikio na kuufanya Mkoa kuweza kuwa na mafanikio kwa kipindi hicho ni baada ya kuimarika kwa huduma za elimu, afya, maji, barabara.

Akieleza mafanikio yaliyopatikana katika ukuaji wa uchumi, Gama anasema pato la Mkoa limekuwa likiongezeka, kutoka shilingi milioni 714 mwaka 2005 hadi kufikia shilingi bilioni 1.448 mwaka 2008.

Wastani wa pato la mtu mmoja mmoja nalo limeongezeka kutoka shilingi 755,037 kwa mwaka 2008 mpaka shilingi 881,884 kufikia mwaka 2010, ikiwa ni juu ya wastani wa pato la mkazi kitaifa la shilingi 770,464.

RC Gama anasema kuwa makusanyo katika Halmashauri za wilaya na Manispaa katika vyanzo vyake vya ndani nayo yameongezeka kutoka shilingi bilioni 2.24 mwaka 2005/2006 na kufikia shilingi bilioni 6.082 kwa mwaka 2011/2012.

Mpango wa sasa katika kukuza mapato yake ni kuona kuwa halmashauri hizo zinafikia lengo la kukusanya wastani wa shilingi bilioni 12.081 kwa mwaka wa fedha 2012/2013.

Anasema kuwa kwa upande wa kilimo ambacho kinachangia zaidi ya asilimia 60 ya pato la mkoa, kumekuwa na mikakati ya kukabiliana na ufinyu wa ardhi ya kilimo, kwa kuongeza mahitaji ya pekee ya pembejeo za na kuboresha utaratibu mzima wa usambazaji wa vocha za pembejeo.

Mkoa wa Kilimanjaro una eneo la hekta 643,000 zinazofaa kwa kilimo na kati ya hizo hekta 579,700 ndizo zinazotumika kwa kilimo cha umwagiliaji, na kubainisha kuwa yapo matumaini makubwa ya kuendeleza hekta 238,500 kwa ajili ya kilimo.

Mpango wa kuongeza vocha za pembejeo unakusudia kuwa Mkoa wa Kilimanjaro umepatiwa jumla ya vocha 181,577, ikiwa ni ruzuku kwa ajili ya kaya 60,519, ukiwa ni mpango wa kukuza uchumi kupitia sekta ya kilimo.

Gama anasema kuwa Mkoa wa Kilimanjaro una viwanda vikubwa na vya kati vipatavyo 28, ambavyo vimeajiri jumla ya wafanyakazi 4,862, sambamba na kuwa na biashara rasmi 8,800 na zile zisizokuwa rasmi 7,080 na kutoa ajira 42,240.

Kuhusu Utalii, Gama anasema kuwa wakati mipango hiyo ikiwa kwenye mchakato, Kilimanjaro kwa miaka saba iliyopita, umefanikiwa kuwa na vivutio vya utalii ikiwemo hifadhi ya taifa ya Mlima Kilimanjaro na msitu unaozunguka mlima huo, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Bwawa la Nyumba ya Mungu na Misitu ya Asili.

Kulingana na takwimu idadi ya watalii imeongezeka kutoka 28,417 mwaka 2003/2004 hadi watalii 52,570 mwaka 2010/2011, huku mapato yaliyotokana na utalii huo yakiongezeka kutoka shilingi bilioni 10.15 mwaka 2003/2004 hadi bilioni 45.604 mwaka 2010/2011.

“Changamoto kubwa hivi sasa ni kukosekana kwa hoteli zenye hadhi ya nyota tano, hivyo kulazimika kuunda kamati ya kuibua fursa za utalii kwa madhumuni ya kuongeza vivutio vya utalii, ajira na mapato kwa halmashari.

“Sekta ya utalii imechangia kutoa ajira kwa vijana wakiwemo wapagazi, waongozaji watalii, makampuni ya utalii na ajira kwenye mahoteli mbali mbali hapa mkoani,” Alisema.

Kwa kutambua hilo mkuu wa mkoa Gama, anasema hivi sasa mkoa wa Kilimanjaro umeamua kuelekeza nguvu kupiga vita matumizi ya pombe kwa wananchi hasa vijana wengi saa za kazi.

Anasema unywaji pombe saa za kazi ni changamoto kubwa kwa mkoa wa Kilimanjaro, kwani wote wanaojihusisha na unywaji huo pia wamekuwa wakipata madhara kiafya.

Unywaji wa pombe pia umekuwa ikiambatana na vitendo vya ukahaba unaofanywa na baadhi ya wasichana ambao wanaacha kujishughulisha na kutafuta njia ya mkato ya kujipatia kipato.

Aidha, Gama anasema kuwa ukiacha mafanikio pamoja na mipango ya mkoa chini ya uongozi wake, kumekuwa na changamoto ya kisiasa inayojitokeza na kuwalenga viongozi na watendaji wa serikali katika mkoa wao wa Kilimanjaro.

Changamoto hii kutoka kwa baadhi ya viongozi wa vyama vya kisiasa vya upinzani ya kuwakashifu na kuwakejeli viongozi na watendaji wa serikali inatokana na hatua yao ya kudhibiti matumizi mabaya ya fedha za serikali zinazotengwa kwa ajili ya maendeleo kupitia Halmashauri za wilaya mkoani hapa.

Mathalani kwa kipindi cha miezi sita sasa baadhi ya viongozi wa kisiasa kutoka vyama vya upinzani wakiwemo wale wa kitaifa, wametoa maneno ya kashfa na kejeli wa viongozi wa serikali mkoani Kilimanjaro, jambo ambalo kwa upande wao haliwezi kuwakatisha tamaa.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...