https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Friday, February 21, 2014

Biashara ya ngono Ziwa Victoria, yadaiwa kuwa wanawake wanalazimishwa penzi ili wapate samani nchini Kenya

Katika ufuo wa bahari ya Ziwa Viktoria kuna biashara inayovuma-dau za uvuvi zilizotengenezwa kwa mbao zimejaa si haba, asubuhi zimejazwa Samaki wa Tilapia.Nyakati za asubuhi na mchana, wavuvi hukusanyika na kupiga foleni kununua Samaki; wengi wao wakiwemo wanawake ambao wanatumainia kupata faida; japo kidogo, katika soko lililo karibu.
Ila, katika sehemu hii ya Kenya, biashara hii haifanywi kwa ubadilishanaji wa pesa kwa Samaki. Malipo ni ubadilishanaji wa ngono kwa Samaki: wanawake wanauza miili yao kwa matumaini kuwa wataeleka nyumbani na Samaki wengi.

Biashara hii inajulikana kama “ubadilishanaji wa ngono kwa samaki” ama, kwa lugha ya kiluo, inajulikana kama “jaboya”. Lucy Odhiambo, 35, anatayarisha ununuzi wake wa mwisho, ambao ataupeleka sokoni; anawapasua samaki na kuwatoa uchafu wa tumboni. Ni mjane, na mama wa watoto tano, anasema kuwa wanawake hapa wanalazimika kufanya wasiyotarajiwa kufanya na jamii.


"Inanilazimu niuuze mwili wangu kwa wavuvi ili nipate samaki kwa sababu sina uwezo wa kujikimu", anaiambia BBC."Kawaida, mimi hulala na wavuvi wawili au watatu kwa juma. Naweza pata magonjwa, ila sina budi kufanya hivyo. Nina watoto ambao nafaa kuwalipia karo. Jaboya ni tendo baya mno. "  

Ugonjwa anaouongelea hapa ni ukimwi ambao umeenea sana katika eneo hili. Ripoti za afya zinadhihirisha kuwa ugonjwa wa Ukinmwi umekithiri katika eneo hili ukiipiku kwa 15% maradufu ile idadi ya wastani ya nchi. Hii inatokana na biashara hii ya “ubadilishanaji wa ngono kwa samaki.Japo polepole, tabia hii inabadilika, huku ikielekea kuisha.
‘Hatutegemei tena wanaume’
Agnes Auma ananipileka ufuoni mwa bahari katika dau analomiliki. Dau hilo linatumiwa na wavuvi ambao amewaajiri kazi, na wanapovua Samaki, yeye ndiye hufanya uuzaji.
Anawalipa wafanyakazi wake na pia gharama za huduma za dau lake, kisha anasalia na hela kadhaa za kujikimu.Mradi unaoendeshwa na shirika la uthamini la eneo hilo linalooitwa Vired unapata msaada kutoka kwa shirika la Marekani la US Peace Corps, na umeweza kuyabadilisha maisha ya wanawake katika eneo hilo.
Tunapiga gumzo wakati dau linazidi kuingia ndani ya ziwa , huku likipita juu ya magugu, na mimea ya baharini, jitihada inayowafanya wavuvi kuloa jasho."Niliona kuwa ningekufa iwapo ningeendelea kuuza mwlili wangu kwa minajili ya kupata samaki-na singeendelea,” Bi. Auma alisema.
“Mradi huu unanisaidia kupata riziki yangu, hivyo basi, si lazima niwategemee wanaume kujikimu. Na, ninapolipia gharama za huduma za dau, nafanya hivyo nafsi yangu ikiwa safi na tulivu.” Tunapofikia sehemu Fulani ndani ya ziwa, wavu unatupwa majini.
Dakika chache baadaye, wavu unatolewa ukiwa umejaa Samaki.Kisha, samaki mkubwa wa kamongo anainuliwa na kutupwa ndani ya dau, huku Bi. Auma akitazama.“Nina furaha kubwa kutokana na jitihada za wavuvi wangu, pia nina furaha kuwa mimi ni mvuvi wa kike ambaye ana bidii na nguvu,” anasema huku akitabasamu.
Leo hii, mradi huu wa Vired, una idadi ya wanawake 19, ila shirika hilo linatumai kuwa idadi hii itaongezeka kadiri muda utakavyoendelea. "Ubadilishanaji wa ngono kwa Samaki ni biashara yenye hatari kwa sababu, kila siku tunagundua kuwa watu wanakufa kutokana na ugonjwa wa Ukimwi,” anasema Dan Abuto wa shirika la Vired.
"Tunahitaji kuwainua wanawake hawa kiuchumi, kinafsi na pia kijinsia ili waweze kupata namna ya kujikimu na kujisimamia. Tuna furaha kuwa mradi huu unavuna matokeo mazuri, na pia wanawake hawa wanadhihirisha bidii na utashi.”
‘Nina aibu’
Ila, hii ni sehemu moja tu ya nchi yangu ambayo “jaboya” ni maarufu. Na hata hapa, kuna wale wavuvi ambao wanafurahia wakilipwa kwa pesa. Lucy Odhiambo: "Nalazimika kulipia samaki kwa kuuza mwili wangu kwa sababu sina namna nyingine ya kujikimu” 
Nakutana na Felix Ochieng, 26, mvuvi ambaye ameoa ila bado anajihusisha na matendo ya ngono nje ya ndoa na wanawake wengine watatu kwa juma, huku akiwapa samaki. Ananiambia kuwa mwanamke atalipia samaki wa shilingi 1000 kwa pesa taslimu ya shilingi 500 ($6; £3.50), huku akitumia mwili wake kujaza akiba ya hiyo shilingi 500 nyingine iliyosalia.
“Niilirithi tabia hii kutoka kwa babangu mwenye alikuwa akifanya vivi hivi," anasema, huku akiapa kuwa anatumia kinga.Namuuliza iwapo ana aibu kutokana na kile anachofanya.
"Ndiyo, nina aibu,” anajibu huku akiangalia upande wa ziwa, “na ni tendo ovu. Ila, kuna matamanio yanayotokana na wanawake." Bado kuna kazi kubwa inayotarajiwa kufanywa ili kuimaliza tabia hii ambayo imekita mizizi katika sehemu kadhaa nchini.
Ila japo kidogo kila siku, idadi ya wanaoshiriki tabia hii inapungua, na wanawake wanaoishi katika maeneo ya ziwa Viktoria wanapata kujua hatari zinazotokana na biashara hii.Kuimaliza biashara hii ya “ubadilishanaji wa ngono kwa samaki” kabisa, tutahitaji kubadilisha fikra na mitazamo yetu, ili kuweza kupata mtazamo mzuri ulio faafu wa jinsia zote.
Na hiyo itakuwa ngumu kufanikisha; kikwazo cha kuweza kufanya biashara ya ubadilishanaji wa samaki kuwezeshwa na pesa pekee.
MAKALA HAYA YAMEANDALIWA NA SHIRIKA LA HABARI UINGEREZA, BBC

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...