https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Friday, November 15, 2013

Wadau wa michezo Mondo mkoani Dodoma wamlalamikia diwani wao, eti anataka kuvuruga mashindano aliyoanzisha mwenyewe



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
DIWANI wa Kata ya Mondo iliyopo Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma, Said Sambala, amelalamikiwa na wadau wa mpira wa miguu wa kata hiyo,  kutokana na kuhusishwa kuvuruga mashindano ya Diwani Cup.
Diwani wa Kata ya Mondo, Comrade Said Sambala, pichani.
Diwani huyo anatuhumiwa kuvuruga mashindano hayo kwa kuonesha mapenzi yake wazi wazi kwa kuzibeba baadhi ya timu, licha ya kuwa yeye ndiye mwanzilishi na mwendeshaji wake.

Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Mondo, Nahodha wa timu ya Mondo Rangers, Ally Hussein maarufu kwa jina la Pengo, alisema diwani amefika wakati mwingine anaingilia ufundi wa waamuzi ndani ya uwanja.

Alisema katika mechi iliyopangwa kuchezwa Novemba 12 mwaka huu, timu ya Sesa ya Kitongoji cha Waida ilichelewa kufika uwanjani, hivyo mwamuzi Chachu Pili kuipa ushindi Mondo Rangers wa pointi tatu na bao 2 kama sheria zinavyoelekeza.

“Awali mashindano yalianza vizuri, ila kadri siku zilivyozidi kusonga mbele, diwani alikuwa akiingilia matakwa ya waamuzi akiwa na lengo la kuzibeba zile timu anazozipenda, ikiwamo hii ya Sesa ambayo aliingilia kwa kupinga mechi kumalizwa na kupewa ushindi Mondo FC.

“Diwani anatumia nguvu anataka timu ya Sesa ishinde ili achukue ng’ombe, hii ni timu yake hata juzi aliikodishia gari na wachezaji alikwenda kuchukua Kondoa mjini tunajua mchezo wake.

“Mpaka sasa ligi haijulikani itachezwa lini kwasababu hakuna kinachofanywa, ukizingatia kuwa diwani amevuruga mashindano yake akiweka mbele maslahi ya baadhi ya timu ambazo kwa bahati mbaya hazina uwezo,” alisema.

Akijibu tuhuma hizo, Sambala alisema habari hizo hazina ukweli, maana alianzisha mashindano hayo si kwa ajili ya kuibeba timu moja, ila kutoa fursa kwa timu zote za Mondo kuonyesha uwezo wao.

“Hakuna timu ninayoipendelea na tayari tumekaa na viongozi wa timu zote na wadau wa michezo kwa ajili ya kuhakikisha kuwa mashindano hayo yanafanyika kwa mafanikio,” alisema Sambala.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...