https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, November 21, 2013

Tukijua mpira ni pesa, tutaheshimu uwezo wa Kaseja


Na Kambi Mbwana, Handeni

WIKI iliyopita, hoja kubwa vinywani mwa wadau wa soka Tanzania, ilikuwa namna Juma Kaseja, aliyewahi kuichezea klabu ya Simba kwa mafanikio makubwa, akisajiliwa Yanga.

Hakuna asiyejua mchango na uwezo wa kipa huyu. Kila mtu anamthamini na kugundua kipaji chake anapoweza kusimama langoni kwa mafanikio makubwa.
Juma Kaseja, kipa wa timu ya Yanga.
Kwangu mimi, Kaseja bado anabaki kipa bora, hivyo sishangai kusajiliwa katika klabu yoyote ya Tanzania, ikiwamo Yanga SC. Pamoja na kutambua umuhimu wake langoni, lakini baadhi ya wadau, wanaojiita wanazi wa Yanga, wamekuwa wakimuangalia tofauti Kaseja.


Hao ni wale wanaosema yeye ni mnazi mkubwa wa klabu ya Simba, timu pinzani. Wengine wanasema kusajiliwa tena Yanga ni kudhihirisha kuwa klabu yao haina mbinu za kusonga mbele, hasa kusajili wachezaji wenye uwezo zaidi kuliko wa Kaseja.

Sawa, tunaweza kuangalia uwezo wake, ila itakuwa mbaya tukimuangalia Kaseja kama mnazi wa Simba, ukizingatia kuwa Dunia imebadilika sasa.


Kaseja atakuwa mwendawazimu kama ataabudu unazi wake hata akiwa kwenye timu nyingine. Kwa sasa wadau tumuangalie kipa huyo kwa uwezo wake na sio kutajwa kama moja ya wachezaji wenye mapenzi na Yanga.


Hii siwezi kuvumilia. Nakumbuka kipa huyu aliwahi kusajiliwa Yanga, akitokea Simba. Je, hakucheza kwa kiwango cha juu? Kwa hiyo Kaseja amerudi tena Yanga kwakuwa ndiko kwenye ofa nzuri na timu iliyoonyesha kumthamini.

Na lazima wadau wa soka tufahamu, Kaseja hajaachwa Simba kwasababu hana kiwango. Kipa huyu aliachwa kutokana na mizengwe.


Tukijua mpira ni pesa, tutaheshimu uwezo wa Kaseja, maana ni wazi ataichezea Yanga kwa mafanikio bila kuweka hata nusu ya unazi.

Na hata kama akifungwa, basi sitamuangalia kama ameuza mechi au ameibeba timu kwa mapenzi yake, ila matokeo ya kawaida ya mpira wa miguu.


Kaseja aliyeachwa kwa dharau timu ya Simba, atakuwa na akili ndogo kama akicheza chini ya kiwango ili kuipa nafasi timu yake hiyo ya zamani.

Dunia nzima itamcheka na kumshangaa. Ni hilo ndilo litakalomfanya Kaseja acheze kwa moyo wote, kujituma bila kuchoka, kwasababu soka ndio sehemu ya maisha yake, hivyo mashabiki wampe moyo.


Huu ni wakati wa wadau wa soka wa Yanga kuhakikisha kuwa wanakuwa na imani kubwa kwa kipa wao ili naye aonyeshe kwanini mpaka sasa anajulikana kama (Tanzania One).

Kinyume cha hapo, sitaweza kuvumilia kuona baadhi yao wanampa wakati mgumu Kaseja kwa kumuona ni mnazi wa Simba, wakati yeye anacheza soka kama ajira yake, huo unazi anaoangaliwa nao kwani anataka kugombea uongozi Yanga au Simba?


+255712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...