https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, November 14, 2013

Utamu wa Malaika bendi kuanikwa rasmi kesho katika uzinduzi wao unaosubiriwa kwa hamu

Rais wa bendi ya Malaika, Christian Bellah, pichani.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
BENDI mpya ya muziki wa dansi, Malaika Music, kesho itazinduliwa rasmi katika Ukumbi wa Mzalendo Pub, uliopo Kijitonyama, Dar es Salaam.

Akizungumza mapema leo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa bendi hiyo, Michael Rocky, alisema maandalizi yamekamilika na tayari bendi yake imekamilisha kutengeneza nyimbo zaidi ya tano.

Rocky alisema ujio wa bendi hiyo ni kutaka kuongeza changamoto katika muziki huo ambao hivi sasa una ushindani mkubwa kutoka katika bendi nyingine.

Mkurugenzi huyo alisema kuwa, bendi hiyo tayari imetoa nyimbo mbili ‘Nakuhitaji’ na ‘Mtu wa Watu’ ambazo zinasikika katika vituo mbalimbali vya redio.
Alisema, wataanza kufanya maonesho rasmi baada ya uzinduzi wa bendi hiyo leo, kwa kuipeleka mikoani ili mashabiki wa muziki waweze kupata burudani zake.

Bendi hiyo iliyo chini ya Mfalme wake, Christian Bella ‘Obama’, ilianza kambi Dar es Salaam mwezi uliopita, ikiwa na wanamuziki zaidi ya 20 kutoka bendi mbalimbali za ndani na nje ya nchi.
 

"Tuna wanamuziki wa ndani na nje ya nchi, hivyo tumechanganya radha na tunategemea mashabiki wetu watapata burudani nzuri," alisema.

Katika uzinduzi huo, bendi ya muziki wa taarab ya Mashauzi Classic chini ya Isha Mashauzi itawasindikiza kwa kuwapa mashabiki raha ya muziki huo wa mwambao, huku Dully Sykes na Kassim Mganga "Cassim' wakitoa burudani ya muziki wa kizazi kipya.

"Tuliwaomba kama wasanii wenzetu, walikubali na kutuahidi kutoa burudani nzuri katika onesho hilo maalumu la kuzaliwa kwa bendi mpya," alisema.

Bella anasaidiwa na rapa Totoo Zebingwa , wakati katibu wa bendi hiyo ni mpapasa kinanda maarufu, Andrew Andrew Sekidia.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...