https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, November 06, 2013

The Tanzanite chini ya ulinzi mkali Msumbiji


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

MECHI ya marudiano kati ya timu ya Taifa ya vijana ya Wanawake, Tanzanite, itachezwa katika ulinzi mkali kutokana na kuendelea kwa machafuko yanayosababishwa na msigano wa vyama viwili vya siasa nchini Msumbiji, kati ya FRELIMO na  RENAMO.
Kikosi cha The Tanzanite, kikiwa uwanjani.
Mechi hiyo ya marudiano imepangwa kupigwa mjini Maputo nchini humo, Novemba 8 na 10, huku wawakilishi hao wa Tanzania waliofanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 10-0 wakitarajiwa kuondoka leo kuelekea Msumbiji.


Mkurugenzi msaidizi wa Michezo katika wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Juliana Yasoda alisema kuwa serikali haina taarifa zaidi ya machafuko hayo.

“Serikali hatuna taarifa za machafuko hayo na ugumu wa timu yetu katika mechi hiyo ya marudiano dhidi ya Msumbiji,” alisema Yasoda.

Naye Kaimu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Boniface Wambura, alisema kuwa serikali ya Msumbiji kwa kupitia Chama cha Soka cha nchi hiyo imehakikisha ulinzi kwa wawakilishi hao wa Tanzania.

“Tutakwenda kama tulivyopanga kwasababu tumepata ulinzi na mchezo utakuwa wa amani katika nchi hiyo ya Msumbiji, hivyo hakuna tatizo lolote,” alisema.

Tanzanite ilishinda mabao 10-0 dhidi ya Msumbiji, ikiwa ni mechi ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za vijana chini ya miaka (20), zitakazochezwa mwakani nchini Canada.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...