https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, December 15, 2012

Mashindano ya ngumi Temeke kuanza Februari mwakani




Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
CHAMA cha Ngumi cha Mkoa wa Temeke (TEABA), kimeandaa mashindano ya mkoa yatakayofanyika Februari 10, 2013 jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa TEABA, Omari Said ameiambia Handeni Kwetu kuwa mashindano hayo yatazishirikisha klabu zote za jijini Dar es Salaam, pamoja na zile za jeshi.

Alisema awali mashindano ya mkoa yalipangwa kufanyika Desemba mwaka huu, ili yaweze kuwa kipimo kwa mabondia wa mkoa huo kabla ya kushiriki michuano ya klabu bingwa taifa itakayofanyika Januari mwakani.

"Mashindano hayo ambayo yamo kwenye kalenda ya TEABA, yanatarajia kuzishirikisha klabu zote za Mkoa wa Ilala na Kinondoni pamoja na klabu ya Magereza, Ngome na JKT ambazo zitatumiwa barua ya mwaliko.

Wakati huo huo maandalizi ya pambano la bingwa wa ngumi za ridhaa Afrika mwaka 1998 na 1999, Said Omari na bingwa wa mashindano ya Jumuiya ya Madola mwaka 1998, Michael Yombayomba la kuchangia watoto wenye ugonjwa wa moyo yanaendelea.

Pambano hilo litakalofanyika Februari 25 mwakani katika Uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam, limeandaliwa ili kusaidia gharama za matibabu ya watoto hao wanaopelekwa nchini India kwa ajili ya matibabu.

Mabondia hao walisema kabla wao hawajapanda ulingoni yatachezwa mapambano ya utangulizi yatakayowashirikisha mabondia wakongwe waliowahi kuchukua ubingwa katika mashindano mbalimbali.

Omari alifanikiwa kupata ubingwa huo mjini Nairobi, Kenya mwaka 1998 na Cairo, Misri 1999 wakati Yombayomba alijinyakulia ubingwa huo nchini Malaysia.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...