https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Friday, December 28, 2012

Simba wampigia magoti Kikwete



Ali Mselemu akionyesha msisitizo
 
Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
WANACHAMA wapatao 698 wa klabu ya Simba, wamemuandikia barua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, wakitaka awasaidie ili wafanye mkutano wao kwa haki, Desemba 30, katika Hoteli ya Travertine, kama walivyopanga.

Hatua hiyo imetokana na kutumia nafasi hiyo kumshtaki mwenyekiti wao, Ismail Aden Rage ambaye pia ni Mbunge wa Tabora Mjini ili rais aone jinsi Rage anavyoichezea Katiba ya Simba.
Baadhi ya wanachama wa Simba, wakimsikiliza mzee wa zamani wa Simba, Ali Mselemu, mwenye kanzu na kofia kichwani, katika kujadili mkutano wao wa Desemba 30, Travertine Hoteli Magomeni.
                   
Akizungumza muda mchache uliopita na Handeni Kwetu, Travertine Hoteli, mmoja wa wanachama hao, Chuma Seleman, akiwa sambamba na wanachama wengine wa klabu hiyo, alisema wamefikisha barua yao Ikulu, ili kuonyesha mapenzi yao kwa Rais ambaye pia ni mwajiri wa Rage, katika nafasi yake ya Ubunge.

Alisema Rage ni Mbunge na pia ni Mwanachama wa Chama cha Mapinduzi CCM, hivyo kwa kukanyaga Katiba ya Simba, ina maana zote zilizosalia hawezi kuziheshimu.

Tumedhamiria kufanya mkutano wetu siku ile ile ya Desemba 30 kuanzia asubuhi hapa Travertine Hoteli, lakini pia tumwomba Rais ajuwe ubabaishaji huu wa Rage katika klabu yetu.

Mbali na Rais, pia tumewasilisha nakala sehemu mbalimbali, ikiwamo kwa Wizara ya Habari Utamaduni na Michezo kwa ajili ya kuliweka sawa hili, ikiwamo kuachwa tufanye mkutano wetu kwa haki kama inavyosema Ibara ya 22 kifungu cha pili ya Katiba ya Simba inayosema siku 30 zikiombwa na wanachama wasiopungua 500 ambao kwa wao wamefikia 698 wana haki ya kuitisha mkutano wa dharura.

Hata hivyo, wanachama hao wamekuwa wakikutana na matatizo mengi, yakiwamo ya kuitwa wahuni huku wengine wakijitokeza wakisema kuwa mkutano huo haupo, jambo ambalo wahusika wanasema mkutano wao upo pale pale na wanachama wenye mapenzi na klabu yao waende kujadili mamabo ya kuisaidia klabu yao ya Simba.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...