https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, December 20, 2012

Victoria Sound kuibukia kwenye Krismasi



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
BENDI ya muziki wa dansi ya Victoria Sound ambayo kwa sasa iko kambini mjini Mtwara, inatarajia kutoa burudani mjini mkoani Mtwara kwa siku tatu mfululizo wakati wa sikukuu ya Krismasi na Boxing Day.

Hayo yalisemwa na rais wa bendi hiyo Mwinjuma Muumin alipokuwa akizungumzia maendeleo ya kambi kwa njia simu kutoka mjini Mtwara na kusema kuwa maonyesho yataanza mkesha wa Krismasi.

"Siku ya mkesha wa Krismasi tutakuwa ndani ya ukumbi wa Makonde Beach mjini hapa na kisha sikukuu ya Krismasi tutakuwa Tandahimba katika ukumbi wa CCM," alisema Muumin.

Rais huyo wa bendi alisema kuwa Boxing Day bendi hiyo itafanya vitu vyake Ndanda  na kisha itarudi kambini kuendelea na mazoezi ya kuandaa nyimbo mpya.

Alifafanua kuwa kwenye maonyesho hayo Victoria Sound itaporomosha baadhi ya nyimbo ambazo alitamba nazo akiwa na bendi mbalimbali zikiwemo za African Revolution, Double M Sound na Bwagamoyo Sound.

"Pia tutatambulisha nyimbo mpya ukiwemo wa Shamba la Bibi ambao nimetunga, hivyo nina uhakika mambo yetu yatakuwa mazuri kwani dalili zimeshaanza kuonekana kwamba tunakubalika," alisema.

Bendi hiyo iliingia kambini wiki iliyopita ikiwa na baadhi ya
wanamuziki kama; Seleman Muhumba (solo) kutoka Twanga Pepeta, Kassim Muhumba (besi) toka Mashujaa Musica na Joyce Musiba (mwimbaji) toka FM Academia.

Wengine ni Kuziwa Abdala (mwimbaji) toka Ufipa Sound, George Gama (besi), Papii Pamba mwimbaji toka Mapacha Watatu na Ramso Bushoke (mwimbaji) na Jonas Mnembuka (solo).

Mbali na wanamuziki hao, kwenye kambi hiyo pia wapo Queen Star, Chuki Kasika na Mariam Lerapee toka Mashujaa Musica na Maga One wa Twanga Pepeta ambao wote ni wanenguaji.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...