https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, October 26, 2013

Tamasha la Utamaduni Handeni na mipango kabambe ya kimaendeleo




Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
ILI kujenga jamii bora na yenye kujua tamaduni zao, kunahitajika kuandaliwa matamasha muhimu yenye dhamira ya kweli katika kona mbalimbali za nchi yetu. Huo ni mpango mzuri na wenye tija.
Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Muhingo Rweyemamu, pichani.
Katika suala hilo, wale wadau wanaotarajia au waliowahi kuandaa matamasha ya aina hiyo ni dhahiri wanatakiwa waungwe mkono badala ya kukatishwa tamaa.


Kwa sasa, tamasha ambalo linatajwa katika vinywa vya watu wengi ni lile la Handeni, linalotarajiwa kufanyika Desemba 14, wilayani Handeni mkoani Tanga.


Tamasha hilo la utamaduni na michezo linatambulika kwa jina la ‘Handeni Kwetu,’ jina lililotokana na mtandao ‘blog’ ya Handeni Kwetu.
Mratibu wa Tamasha la Handeni, Kambi Mbwana, pichani.
Vyovyote litakavyotajwa na wadau wa matamasha duniani kote, ili mradi linatimiza na kutoa majibu halisi ya namna ya kutangaza na kukuza utamaduni wa Tanzania, si vibaya na njia ya kulitangaza mbele ya jamii.


Katika mazungumzo yaliyofanyika mapema wiki hii, mwishoni mwa wiki iliyopita, Mratibu Mkuu wa tamasha hilo, Kambi Mbwana, anasema kuwa lengo la kuandaa tamasha hilo ni kushirikiana na serikali na wananchi wote kujua mbinu imara za kuutangaza utamaduni wetu.
Mbunge wa Handeni na Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt Abdallah Kigoda, pichani.
Anasema kwa maeneo kama Handeni na kwingineko, kumekuwa na changamoto kubwa za wananchi kuacha utamaduni wao na kufuata wa wenzao jambo linalotakiwa lipingwe vikali.

“Nilikaa chini na kutafakari namna gani ya kuwaunganisha watu wote katika tukio moja na kuwa sehemu ya wao kuangalia ngoma zetu, nyimbo zetu na mbinu za kijamii kwa ujumla wake.

“Naamini katika umri wa taifa letu la Tanzania, kuna mengi yametokea na yaliwahi kutokea hasa wakati wa ukoloni, hivyo naamini siku hiyo tutajua ni kiasi gani watu wa asili ya Handeni walikuwa na mchango kwenye jamii yao,” alisema Mbwana.

Mbwana ambaye ni mwandishi wa habari na mmiliki wa ‘blog’ ya Handeni Kwetu (www.handenikwetu.blogspot), anasema kwamba kwa kukutana watu wote ni sehemu ya kuangalia namna ya kulitumikia taifa letu la Tanzania na kubuni mbinu za kujikomboa kiuchumi.

Mdau huyo wa mambo ya utamaduni, michezo na sanaa kwa ujumla wake ukiwamo muziki, anasema kwamba Handeni ni miongoni mwa wilaya zenye changamoto kubwa hivyo kuna haja ya wadau wote kukutana kwa pamoja na kuangalia namna ya kuzitatua, hasa kwa kupitia tamasha hilo.

“Huu si wakati wa kuangalia Mkuu wa Wilaya (DC) Muhingo Rweyemamu anafanya nini au Mbunge Abdallah Kigoda na viongozi wote wa serikali, ila jambo la muhimu ni kushirikiana nao kuleta maendeleo.

“Mtu wa kwanza katika maendeleo ni mwananchi mwenyewe, hivyo naomba kuwakaribisha Watanzania na hata wale wasiokuwa Watanzania kukutana pamoja na sisi kwenye tamasha hili,” alisisitiza Mbwana.

Aidha, Mbwana anatumia muda huo kuwaomba wadau wote, wakiwamo viongozi wa serikali, mashirika na kampuni kujitokeza kudhamini tamasha hilo litakalokuwa la aina yake.

Tamasha la Utamaduni la Handeni Kwetu linafanyika kwa mara ya kwanza, likipangwa kuanza saa tatu asubuhi hadi saa 12 jioni, ambapo vikundi mbalimbali vya sanaa vitashiriki.

Ili kuleta hali ya kimkoa, Mbwana anasema juhudi zinafanyika kupata vikundi katika baadhi ya wilaya za Mkoa wa Tanga ili kuimba nao, kucheza nao na kushiriki nao katika jambo la kimaendeleo.

Mdau huyo wa habari anasema kwamba hadi sasa wadau kadhaa wamejitokeza kudhamini tamasha hilo linalotikisa katika maeneo ya Handeni na Tanzania kwa ujumla.

Anawataja wadau hao kuwa ni pamoja na Yusuphed Mhandeni, ambaye ni Mchumi wa CCM Kata ya Makumbusho kwa kupitia Kampuni yake ya Yusuphed Trans, yenye magari yanayotoka Dar es Salaam kwenda Mkata, wilayani Handeni, Grace Products, Screen Masters na mtandao wao wa Saluti5.com, Dullah Tiles & Construction Ltd, Katomu Solar Specialist, Country Business Directory (CBD) na Michuzi Media Group.

Wengine ni duka la mavazi la Chichi Local Ware, Smart Mind & Arters chini ya Anesa Company Ltd, ikidhamini kwa kupitia kitabu chao cha ‘Ni Wakati Wako wa Kung’aa’, Lukaza Blog, Kajunason Blog, Jiachie Blog na Taifa Letu.com.

Mbwana anasema kwamba kwa kupitia tamasha hili, wadau wote watapata fursa ya kutangaza biashara zao, ukizingatia kuwa tamasha hili linatarajia kukutanisha watu wengi zaidi sehemu moja.

“Tunaomba udhamini kwa watu wote ili tushirikiane katika kufanikisha tamasha hili la kihistoria, huku tukiamini kuwa wenzetu wa Kilindi, Korogwe tutakuwa nao pamoja.

“Maandalizi yanaendelea kuhakikisha kuwa tunafanya kitu cha tofauti katika tamasha hilo, nikiamini kuwa mguso huu utaendelea kushika kasi na habari hizi njema kuenea nchini kote,” alisema.

Mbwana anasema kwamba wazo la kufanyika kwa tamasha hilo limepewa baraka na viongozi wote, akiwamo DC Rweyemamu na Mbunge, Abdalah Kigoda, ambaye pia ni Waziri wa Viwanda na Biashara.

Anasema kuwa kwa kufanyika kwa tamasha hili ni muendelezo wa mipango mingi mizuri ya kimaendeleo itakayoandaliwa kwa kushirikiana na Watanzania wote, hususan wananchi wa Handeni.

Mwisho kabisa Mbwana alitumia muda huo kuwakumbusha wafanyabiashara mbalimbali wilayani Handeni na Tanga kwa ujumla, kuingia moja kwa moja katika tamasha hili la aina yake.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...