https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Thursday, October 24, 2013

Mgombea Urais TFF, Athuman Nyamlani afungua kampeni zake kwa kutaja vipaumbele tisa vya kukuza soka la Tanzania



Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MSUGUANO wa mbio za Urais katika Shirikisho la Soka nchini (TFF), umeendelea leo baada ya mgombea wa nafasi hiyo kubwa katika ngazi ya mpira wa miguu Tanzania, Athman Nyamlani kutaja vipaumbele tisa vya maendeleo ya soka, iwapo atapata ridhaa ya wapiga kura kuliongoza Shirikisho hilo.
Mgombea nafasi ya Urais wa TFF, Athuman Nyamlani, akifanya mahojiano na waandishi katika moja ya matukio ya kimichezo Tanzania.
Maneno ya Nyamlani yamekuja baada ya kujitosa katika kinyang’anyiro hicho cha Uchaguzi Mkuu wa TFF, akipambana na Jamal Malinzi.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam, katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), ikiwa sehemu ya uzinduzi wa kampeni zake za uchaguzi utakaofanyika Jumapili, Nyamlani alisema akipewa nafasi hiyo, atainua kiwango cha soka kwa kutekeleza msingi imara wa soka la Tanzania.

Nyamlani ambaye kitaaluma pia ni hakimu wa Mahakama ya Wilaya Kinondoni, alisema katika kipindi cha miaka minne ataimarisha usimamizi na Manejimenti ya soka katika ngazi zote kwa kupitia nafasi hiyo ya urais sanjari na kushirikiana na viongozi wa klabu na vyama vya soka vya wilaya na mikoa kwa ujumla wake.

Alisema ataimarisha usimamiaji na menejimenti ya soka katika ngazi zote kwa kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa viongozi na kusimamia sheria na taratibu za uendeshaji wa soka la Tanzania na suala la viongozi  kujiendeleza kielimu litapewa kipaumbele na litakuwa ni agenda endelevu.
Nyamlani alisema suala lingine ambalo litakuwa katika utekeleza wake ni rushwa katika soka nchini.

“Naomba nikiri kuwa kumekuwa na malalamiko na vitendo vya rushwa ambavyo vinawahusisha viongozi wa soka. Hivyo basi kwa kushirikiana na serikali na viongozi wa soka katika ngazi zote nitahakikisha naendeleza mapambano dhidi ya rushwa,” alisema Nyamlani.

Kipaumbele cha tatu kitakuwa ni kukuza soka la watoto, vijana na wanawake, akiwa kama Rais wa TFF, atalipa uzito wa kipekee soka la watoto wenye umri wa miaka chini ya 16 na soka la vijana na kukuza vipaji kuanzia miaka tisa hadi 12, 13-14, 15-17 na 18-21 na soka ya wanawake.

Nyamlani alisema kazi hiyo ataitekeleza kwa kuanzisha program mbali za mashindano na za kukuza vipaji kwa makundi haya ya vijana kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa soka.

Kwa sababu kubwa ya kufanya hivyo ni ukweli kwamba haya makundi ambayo yameonesha uwezo yatatoa mwanga jambo ambalo uongozi uliopita ulilifanya na alihaahidi kuendeleza kulitekeleza kwa kushirikiana na viongozi wa soka katika nagzi mbalimbali na serikali.

Kipumbele kingine muhimu ni Kuimarisha Uwezo wa Rasilimali Fedha wa Shirikisho, kama Rais wa TFF atahakikisha kuwa TFF inapata vyanzo endelevu na vya kuaminika ili kuweza kujenga uwezo wa shirikisho katika kutekeleza mipango kikamilifu.

Nyamlani alisema ataimarisha idara ya masoko ili kuweza kupata wadhamini zaidi na kuweza kuuza nembo za shirikisho.  

Alisema kipaumbele kingine ni Kuongeza Idadi na Ubora Waamuzi, Walimu wa soka na Wataalamu wa Afya ya Michezo.

Nyamlani alisema atahakikisha kunakuwa na program endelevu ya mafunzo kwa makocha, waamuzi wa soka nchini na wataalamu wa afya ya michezo ili kuongeza ufanisi wao katika kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa sheria na taratibu zinazoongoza michezo wa soka, pia kufikia viwango vya kimataifa vilivywekwa na Caf na Fifa.

Kipaumbele cha sita ni Kuongeza Ubora wa Ligi Kuu, Ligi Daraja la Kwanza, Ligi za wilaya na mikoa, mashindano ya Ligi daraja la 1, ligi za wilaya, mikoa na Ligi Kuu ni ngazi muhimu ya kukuza soka katika nchi.

Nyamlani alisema atashirikiana na viongozi wa soka na vyama vya kitaalamu ili kuweza kuboresha kanuni mbalimbali zitakazowawezesha wachezaji vijana kuwa wachezaji wa kulipwa.

Alitaja kipaumbele kingine ni Kuongeza Idadi ya Mawakala wa Wachezaji ambao ni Watanzania, kama Rais wa TFF ana imani kwamba ili soka la Tanzania likue kwa kasi ni lazima ataongeza idadi ya wachezaji na mawakala wanaozingatia weledi.

 Alisema ataimarisha Ushirikiano wa TFF na Serikali, kama rais wa TFF atahakikisha anakuza na kuendeleza mahusiano mazuri kati ya TFF na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa imani kwamba ni jambo hilo ni  muhimu kwa ustawi wa soka kwa sababu ni ukweli soka sasa ni ajira kwa vijana ambao ni nguzo ya Taifa.

Kipaumbele cha tisa ni Kuimarisha Ushirikiano wa TFF, Caf na Fifa, atahakikisha kuwa anakuza na kuendeleza mahusiano kati ya vyombo hivyo ili kuongeza kasi ya ukuaji wa soka nchini, kufikia viwango vya kimataifa kwa kutumia misaada mbalimbali ya kitaalamu na kifedha inayotolewa na Taasisi hizo kubwa duniani.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...