https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, October 22, 2013

Historia fupi muhimu ya marehemu Julius Nyaisangah aliyeagwa leo Leaders Club

Marehemu Nyaisangah (R.IP.)
Marehemu Julius Nyaisangah, Jina ambalo kwa hakika litabaki kutajwa katika historia ya muziki Tanzania. Mtangazaji huyu ambaye alitokea Kenya na kuja kujiunga na Radio Tanzania Dar es Salaam, alikuja na aina mpya ya utangazaji ambayo ilimfanya apate nafasi ya pekee katika nyoyo za wasikilizaji wa RTD kwa miaka yote aliyokuweko huko. 
 
Akifahamika kwa wengi waliopenda kusikiliza sauti yake kama  Uncle J, Nyaisanga ambaye mwenyewe alisema alitengeneza staili yake ya utangazaji kwa kumuiga mtangazaji maarufu wa KBC Leonard Mambo Mbotela aliyejulikana sana kwa kipindi chake 'Je huu ni uungwana?' alikuja na utangazaji uliochangamsha kumsikiliza.  
 
Nyaisanga alikuwa Producer wa mamia ya nyimbo za bendi zilizorekodiwa na bendi mbalimbali katika studio za RTD miaka ya 80. Nilipata bahati ya kufanya nae kazi wakati nilienda kurekodi nikiwa katika bendi tatu tofauti, Orchestra Mambo Bado, Tancut Almasi Orchestra, na  Vijana Jazz Band. Alishauri vizuri na matokeo yake ni nyimbo nyingi zilizopitia mikononi mwake zingali zinapendwa mpaka leo.

Pamoja na utangazaji, na u producer wa muziki, Nyaisanga alipenda muziki na wanamuziki, alikuwa rafiki wa wanamuziki wengi sana, alikuwa na tabia ya kutembelea bendi zinapopiga na aliweza hata kutembelea bendi nne au tano kwa usiku mmoja. 
Na hasa kama bendi iko katika ratiba ya kurekodiwa. Aliwahi hata kufika Iringa kutembelea tancut Almasi Orchestra kabla ya kurekodi toleo lao lililokuwa naule wimbo usiochosha Masafa Marefu.
 
Nyaisanga alipita kwenye bendi kadhaa kututaarifu kuhusu kuanza kwa radio mpya ambayo ingekuwa katika masafa ya FM, na ndipo muda si mrefu Radio One ikaingia hewani wakati huo ikiwa pale katika jengo la NASACO ambalo lilikuja kuungua na baada ya kukarabatiwa sasa linaitwa Waterfront
 
Pia akiwa Radio One Nyaisangah aliendelea kuwa Nyaisanga, japo sera za Radio One hakika zilikuwa tofauti na zile za RTD, lakini pia huko mchango wake katika muziki ulikuwa mkubwa sana. 

Hatimaye Nyaisanga alihamia Abood Radio Morogoro ambako amekuweko mpaka hatimae usiku wa kuamkia leo 20 October 2013, umauti umemkuta katika hospitali ya Mazimbu Morogoro kutokana na kusumbuliwa kwa muda mrefu na Kisukari.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...