https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, October 28, 2013

SIWEZI KUVUMILIA:Tutadanganyana tu, kwani nani anajali?



Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

SITAKI kusikia nani ameshinda nafasi za Uchaguzi Mkuu wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), kwakuwa kuna uwezekano mkubwa uwapo wa mabwana wakubwa hao ukawa kazi bure.
Kikosi cha Twiga Stars
Siku zote wamekuwa wakitogotea pale pale. Mawazo au juhudi za kuokoa soka letu huwa zinaishia hewani. Ingawa kwa siku za hivi karibuni soka linaonekana kufika mbali, ila upande wa wanawake hakuna kitu.


Kila siku ya Mungu kilio kinakuwa kile kile. Wasichana ambao ndio wahusika wakuu wanaocheza mpira huo, wanaishia kulalama wakiangalia jinsi wanavyosuswa.


Kama hivyo ndivyo, kwanini nibabaike na majina ya wagombea wa TFF, katika Uchaguzi uliofanyika jana Jumapili? Nasema hivyo kwasababu juhudi nyingi zinaishia njiani.


Tumebakia watu wa siasa. Tunapenda sana kuzungumza mdomoni wakati vitendo vyetu vina matege. Ndio maana naona tunadanganyana tu,kwani nani anajali kuona soka letu linaanguka?


Nimefanikiwa kuzungumza na wachezaji mpira wa miguu wanawake kwa nyakati kadhaa na kuona jinsi wanavyolalamika. Hata maisha yao ya baadaye hawajui wataishi vipi.


Wengi wanaingia kwenye soka lakini hakuna mashindano yoyote yenye nguvu kiasi cha kukuza uwezo wao. Hakuna ligi yoyote inayoashiria kuwa ni njia ya kukuza soka letu.


Nini hatma ya maisha yao? Wanacheza mpira ili wapate nini? Nani wa kuwainua kiuchumi, kama ajira yao inatia mashaka? Ni tofauti na soka la wanaume, ambao tunasikia wanavyovuna utajiri mkubwa mno.


Leo tunashuhudia jinsi Mrisho Ngassa anavyoweza kuvuna fedha nyingi, wakati mwenzake Sophia Mwasikili hana anachopata. 


Timu ya Taifa, Taifa Stars inalala hoteli ya nyota tatu hadi nne wanapoweka kambi yao, lakini ndugu zangu wa Twiga Stars wananyang’anyana maji ya kunywa.

Wadhamini wanapigana vikumbo Taifa Stars, lakini Twiga wao wanabembeleza bila mafanikio. Hii ni laana. Na ni unafiki uliopitiliza. 


Na ndio maana siwezi kuvumilia hadi nichekee Uchaguzi wa TFF usiokuwa na dhamira, kama waliochaguliwa watapita njia ile ile iliyotufikisha hapa.


Jambo jema ni kutambua makosa yetu. Sitaki kuamini kwamba wadau wa soka, wakiwamo TFF wenyewe kama wamejitambua. 


Mara kadhaa TFF wanachojua wao ni kuandaa mechi kubwa zenye kugusa watu wengi na sio kuboresha ligi zinazoweza kutoa wachezaji mahiri.


Mpira unalipa mno. Tukiwa makini, kila anayejihusisha nao kwa asilimia zote basi lazima anufaike nao. Ukiacha sasa wanaonufaika ni viongozi wanaofikia kugawana mapato ya milangoni.


Najua ni mapema kuanza kulaumu juu ya nani ametangazwa jana kuwa mshindi wa nafasi ya Urais wa TFF au makamu wa Rais, ila kwasababu watendaji wapo ndani ya Shirikisho hilo, bado hawawezi kukwepa lawama zangu.


Ni ukweli huu japo ukiusema wadau baadhi yao wanakataa kwa kudhani labda tuna ajenda za siri juu ya viongozi hao. Tusipokuwa makini, tutaishia kupiga porojo kila siku ya Mungu.


Wenzetu wanasonga mbele, sisi tunaishia kupiga soga katika vijiwe vya kahawa, jambo ambalo kamwe haliwezi kuwa mkombozi wa soka letu. 


Hakika siwezi kuvumilia. Tunapaswa kuzinduka, hasa kwa kuandaa ligi za wanawake, ligi daraja la kwanza yenye nguvu pamoja na mashindano mbalimbali ya vijana katika mikoa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Huu ndio ukweli wa mambo. Kinyume cha hapo, tutaishia kuwa wajuaji wa kupiga kampeni za uchaguzi, kutoa ahadi za uongo zisizotekelezwa kwa vitendo na kutufanya tuwe kama majuha.


Kwanini? Nadhani huu ni wakati wa kuangalia nyendo zetu na kukumbusha safu mpya ya uongozi iliyopatikana jana katika Uchaguzi wa TFF.

Mungu ibariki Tanzania.


+255712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...