https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Friday, May 30, 2014

Makamu wa Rais Dkt Bilal afungua kituo cha tiba, uchunguzi na mafunzo kwa wagonjwa wa saratani

Maskamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akimkabidhi zawadi mmoja kati ya washiriki waliosaidia ujenzi wa jengo jipya la Kituo cha Tiba, Uchunguzi na Mafunzo ya Magonjwa na Saratani za Matumbo na Ini cha Hospitali ya Taifa Muhimbili, Mwakilishi wa Taasisi ya Else Kronner Fresenius Stiftung, Prof. Konrad Mebmer, baada ya ufunguzi huo. Picha na OMR

HOTUBA:- HOTUBA YA MHE. DKT. MOHAMMED GHARIB BILAL, MAKAMU WA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KATIKA UFUNGUZI WA KITUO CHA TIBA, UCHUNGUZI NA MAFUNZO YA MAGONJWA NA SARATANI ZA MATUMBO NA INI CHA HOSPITALI YA TAIFA MUHIMBILI,
TAREHE 30 MEI, 2014

Mhe. Dkt. Kebwe Steven Kebwe
Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii;

Dkt. Gabriel Upunda
Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini, Hospitali ya Taifa Muhimbili;

Dkt. Rufaro Chatara
Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO)

Prof. H.C. Konrad Meßmer (MESSMER);
 Mwakilishi wa Else Kroner – Fresenius Stiftung ya Ujerumani;

Prof. Meinhard Classen;
Mwenyekiti, Munich Society of Gastroenterology;

Waheshimiwa Mabalozi;
 
Dkt. Marina Njelekela
Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili;

Prof. Ephata Kaaya
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha  Afya na Sayansi za Tiba Muhimbili;

Prof. Msemo Diwani
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji, Taasisi ya Saratani Ocean Road;

Wageni Waalikwa;

Mabibi na Mabwana;

Napenda kuchukua nafasi hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa uongozi mzima wa Wizara ya afya kwa kunialika kushirikiana nanyi katika tukio hili. Kwa namna ya pekee nikupongezeni kwa maandalizi mazuri na kwa kuwa na wazo la kuanzisha kituo hiki ambacho kinaongeza nguvu katika utoaji huduma za afya hapa Tanzania. Kituo hiki ni cha kwanza katika nchi za Afrika Mashariki na kitatoa huduma za tiba, uchunguzi na mafunzo kwa kutumia Hadubini. Ni wazi kuwa kituo hiki kitasaidia wananchi wetu kupata huduma hapa nchini na kitawapunguzia gharama zilizotokana na wao kwenda nje kutafuta tiba ya magonjwa haya.

Mabibi na Mabwana;
Ninafahamu kuwa ujenzi wa Kituo hiki umewezekana kutokana na ushirikiano baina ya Serikali ya Tanzania na Chama cha Magonjwa ya Tumbo cha Munich. Serikali ya Tanzania imechangia shilingi Milioni Mia Nane na Chama cha Magonjwa ya Tumbo cha Munich kupitia msaada kutoka ELSE KRONER FRESENIUS STIFTUNG ya Ujerumani, imechangia zaidi ya shilingi za kitanzania Bilioni Moja kwa ajili ya ununuzi wa vifaa. Huu ni uwekezaji mkubwa sana na naomba kutumia nafasi hii kukuombeni wenzetu wa Hospitali ya Muhimbili kuhakikisha kuwa mnakitumia kituo hiki ipasavyo huku pia mkivitunza vifaa vilivyopo.

Mabibi na Mabwana;
Magonjwa ya mfumo wa chakula na ini ni  miongoni mwa  matatizo makubwa ya kiafya yanayoikabili dunia nzima kwa sasa. Kumbukumbu za magonjwa ya Saratani duniani zilizotolewa mwaka 2008 zinaonyesha kuwa, jumla ya wagonjwa wapya takribani milioni tatu na laki tano, waliugua saratani za mfumo wa chakula na ini.  Kati ya hao asilimia 65% walitoka katika nchi maskini, ikiwemo Tanzania.

Saratani ya koo la chakula na ini, ndizo zinazoongoza katika nchi maskini ukilinganisha na nchi zilizoendelea, zikifuatiwa na saratani ya tumbo. Hapa kwetu Tanzania, wastani wa watu 30 hadi 35 kwa kila wananchi 100,000 hufariki dunia kila mwaka kwa saratani ya koo la chakula.

Sababu kubwa za maradhi haya ni za mtindo wa maisha kama unywaji wa pombe na uvutaji wa sigara. Pia, magonjwa ya kuambukiza kama homa ya ini na bakteria aina ya Helikobakta, ni sababu mojawapo ya mtu kupata saratani za mfumo wa chakula na ini.

Mabibi na Mabwana;
Ninaelewa kuwa hatuna wataalamu wa kutosha katika huduma hii ya afya wakiwemo madaktari, wauguzi na wataalamu wengine ili kufanikisha kuendesha kituo hiki vizuri. Mmenitaarifu kuwa kuna Mabingwa wa Hadubini wanane (8) hapa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa sasa, pamoja na wauguzi watano tu ambao ni wachache sana.

Katika kusaidia kukabiliana na upungufu huu, serikali yetu itasaidia katika kufanikisha mafunzo kwa wataalamu zaidi ndani na nje ya nchi katika maeneo haya ili walau tuwe na idadi inayohitajika.

Nitumie nafasi hii pia kuwaomba wenzetu wa Taasisi za Hospitali ya Taifa Muhimbili, Chuo Kikuu cha Afya na Sayanzi za Tiba Muhimbili na Taasisi ya Saratani Ocean Road, kupanua huduma zenu na kutoa huduma za kitaalamu zaidi kama vile upandikizaji wa figo na nyinginezo. Pale mnapohitaji msaada kutoka serikalini, msisite kufanya hivyo kwani suala la afya linagusa maisha ya kila mwananchi wetu.

Mabibi na Mabwana;
Pamoja na mikakati ya kutoa huduma za tiba, nakisihi kituo hiki pamoja na taasisi wadau kufikiria namna ya kuanzisha kinga ambayo inajumuisha chanjo kwa magonjwa kama hepatitis B na C ambayo yanachangia kwa kiasi kikubwa magonjwa ya tumbo na ini (hepatology) ikiwemo saratani ya ini. Ninaelewa kuwa katika mpango wa chanjo (Expanded Program of Immunisation) chanjo ya Hepatitis B inatolewa kwa watoto.

Hata hivyo, jitihada zinatakiwa kuendelea ili kujumuisha watu wazima ambao hawajapata chanjo hiyo. Zaidi ya hayo, tafiti zinazohusu maeneo ya Afrika ni muhimu sana kwani zitatuonesha mwelekeo na kutusaidia katika kubuni jitihada mbalimbali za kukabiliana na matatizo ya kiafya yanayokabili nchi zetu.

Ndugu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Hospitali ya Taifa Muhimbili; 
Katika hotuba yako umetaja upungufu mkubwa wa wafanyakazi kama moja ya changamoto. Ni kweli changamoto hii ipo katika kila sekta, ikiwemo sekta ya afya. Hata hivyo, serikali yetu inafanya kazi kwa bidii kukabiliana nayo ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya wanafunzi wanaosomea shahada ya uzamili katika tiba na uuguzi.

Mabibi na Mabwana;
Sekta ya afya ni moja  ya sekta zinazoathiriwa sana na tatizo la wataalamu kuondoka kwa ajili ya kupata maslahi bora zaidi nje ya nchi. Naelewa kuwa kwa maendeleo ya utandawazi tuliyonayo, mtu yeyote angependa kupata maslahi bora zaidi. Serikali yetu imekuwa ikijitahidi na inaendelea kujitahidi kuhakikisha kuwa wataalamu wetu wanapata maslahi bora kadiri ambavyo tunamudu.

Bajeti ni ndogo, lakini naelewa kuwa Hospitali ya Taifa ina huduma ya wagonjwa binafsi yaani “Intramural Private Practice (IPPM)” ambayo si kwa wagonjwa binafsi tu bali pia mifuko mbalimbali ya bima ya afya kama vile Mfuko wa Taifa wa Bima  ya Afya (NHIF) na Mfuko wa Afya ya Jamii. Hivyo mnaweza kabisa kutumia mapato yanayopatikana kutokana na huduma hii katika kuboresha vipato vya wataalamu wenu. Ninaamini kuwa kama ikitumika vizuri, maslahi bora yanayosemwa hayatakuwa popote zaidi ya hapa hapa Hospitali ya Taifa Muhimbili

Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini Muhimbili, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi za Tiba Muhimbili na Wakurugenzi Watendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili na Taasisi ya Saratani ya Ocean Road,

Kuhusiana na kudumu kwa kituo hiki, ninafahamu kuwa marafiki zetu wa Gastroenterology Foundation of Munich na Else Kroner Fresenius Stiftung hawataendelea kutusaidia milele. Ni wakati muafaka sasa kwa kituo kupitia Hospitali ya Taifa Muhimbili kuwa na bajeti yake inayojitegemea kila mwaka ambayo itajumuishwa katika bajeti yote ya mwaka bila kutegemea bajeti ya jumla ya Hospitali.

Zaidi ya hayo, kupitia huduma ya IPPM, kituo kifanye kazi kama kitengo kinachotengeneza mapato yaani kwa lugha ya kigeni “business unit” ili kutengeneza mapato yake.  Mapato hayo yatumike kununua mahitaji ya kitengo kama vile vifaa tiba kuepuka kushindwa kutoa huduma kutokana na ukosefu wa vifaa. Hii itakihakikishia kitengo kufanya kazi vizuri muda wote na huduma zake zitakuwa endelevu.

Mabibi na Mabwana;
Nitakuwa sijatenda haki kama sitatoa shukrani za dhati kwa “Gastroenterology Foundation of Munich” na “Else Kronner Fresenius Stiftung” chini ya usimamizi wa Prof. Meinhard Classen kwa jitihada zake katika kuanzishwa kwa kituo hiki na kuifanya siku ya leo kuwa ya kukumbukwa. Ni ukweli usiopingika kuwa, ufadhili wa fedha uliofanywa na Else Kronner- Fresenius Stiftung ambaye Mwakilishi wake Prof. Dr. H.C. Konrad Meßmer (MESSMER) ambaye yupo hapa pamoja na kazi ya usimamizi wa mradi huu uliofanywa na Prof. Classen binafsi kupitia Gastroenterology Foundation of Munich, haukuwa rahisi wala nafuu.

Hawa ni watu wenye upendo wa dhati na wenye kujali wagonjwa na zaidi wenye mapenzi na Afrika ndio wanaweza kufanya kazi kubwa kama hii. Hivyo kwa niaba ya Serikali ya Tanzania nasema asante sana kwako Prof. Classen pamoja na rafiki zako wa Ujerumani ambao wachache wako hapa na wale wote waliochangia katika kufanikisha kituo hiki.  

Mabibi na Mabwana;
Ningependa kuchukua nafasi hii kuishukuru Serikali ya Ujerumani kwa misaada mbalimbali iliyokwishatoa kwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa watanzania. Mmekuwa pamoja nasi mara zote siyo tu katika sekta ya afya bali pia katika sekta nyingine, ikiwemo uongozi bora. Kama watanzania, tunathamini ushirikiano huu na tunaamini kuwa utadumu kadiri nchi zetu mbili zitakavyodumu.

Nashukuru tena kwa kunikaribisha hapa na sasa natamka kwamba Kituo hiki cha TIBA, UCHUNGUZI NA MAFUNZO YA MAGONJWA NA SARATANI ZA MATUMBO NA INI CHA HOSPITALI YA TAIFA MUHIMBILI kimezinduliwa rasmi.

Asanteni kwa kunisikiliza

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...