https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Sunday, May 11, 2014

CHANETA wahaha kusaka nauli ya Botswana

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

CHAMA Cha Netiboli Tanzania (CHANETA), kinahangaikia fedha za kuwafikisha nchini Botswana wanapotakiwa kwenda kushiriki mashindano ya Kombe la Afrika kwa kwa timu za Taifa za vijana, chini ya miaka 18.


Mashindano hayo yamepangwa kuanza kutimua vumbi Juni 22 mwaka huu, ambapo timu hiyo ya Taifa inapaswa kufika huko kati ya Juni 19 hadi 20.


Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa CHANETA, Anna Kibira, alisema kwamba uwezo wa chama chao kifedha sio mzuri, hivyo nauli ya kuwafikisha nchini Botswana ni changamoto kubwa.


Alisema wanaendelea kuhaha kusaka nauli hiyo ambapo kwa pamoja timu hiyo itakuwa na wachezaji 12 na viongozi watano, hivyo kufika idadi ya watu 17.


“Tunaomba wadau na serikali kwa ujumla watusaidie katika hili ili tuweze kwenda kuiwakilisha nchi kwa kupitia mashindano ya netiboli nchini Botswana.


“Haya ni mashindano makubwa yanayoshirikisha mataifa mbalimbali ya Afrika, hivyo endapo tutakwenda tutaiweka nchi katika nafasi nzuri zaidi kwa kupitia sekta ya michezo, hususan hii ya netiboli,” alisema Anna.


Kwa mujibu wa Anna, CHANETA ilianza kuwaomba wadau juu ya mashindano hayo wakihitaji msaada wa gharama za kwenda na kurudi pamoja na posho tu, maana kula na kulala itakuwa chini ya viongozi wa Botswana.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...