https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, April 23, 2014

SIWEZI KUVUMILIA: Azam FC imewaumbua ‘Doto na Kulwa’

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
NITAUMIA kama kuna mtu atashindwa kuipongeza timu ya Azam iliyofanikiwa kutwaa ubingwa wa Tanzania Bara msimu huu.

Ndio, maana timu hii imeweza kunyakua ubingwa mbele ya timu za Doto na mwenzake Kulwa zinazoaminika ni timu vigogo vya soka vya Tanzania Bara. Kwa wasiojua, timu za Doto na Kulwa, basi ni Simba na Yanga, zilizoanzishwa miaka ya 1935 kwa Yanga na 1936 kwa mwenzake Simba SC.

Wakati inanyakua ubingwa wa Tanzania Bara, wapo baadhi ya watu wanaoshikwa na machungu kiasi cha kufikiria kuwa Azam wameshinda kwa kubebwa, jambo ambalo si kweli hata kidogo.

Hapa siwezi kuvumilia kamwe. Siku moja baada ya kushinda mbele ya Mbeya City kwa bao 2-1 jijini Mbeya, Kocha wa Mbeya City, Juma Mwambusi aliibuka akisema kuwa Azam wanabebwa.

Hapa unaweza kushangaa kauli hii. Tujiulize. Vipi Mbeya City wangefungwa na timu za kina Doto na Kulwa yani Simba na Yanga?
Vipi timu hizi zingeendelea kutawala soka la Tanzania kwa kuibuka mabingwa kila mwaka? Hapana. Hii si njia nzuri.

Kwa timu kama Azam FC, nathubutu kusema kuwa imestahili kunyakua ubingwa wa Tanzania Bara. Na inastahili pia kushiriki michuano mikubwa, ikiwamo Ligi ya Mabingwa Afrika, msimu ujao.

Wasimamizi wa soka la Tanzania, Shirikisho la Soka nchini (TFF) iwe makini katika hili. Azam ni miongoni mwa timu zenye wachezaji mahiri mno.
Hata hivyo haitoshi, pia imewekeza vizuri, hivyo sioni ajabu ikichukua ubingwa wa Tanzania Bara au hata taji lolote barani Afrika.

Huu ni wakati wa kujivunia matunda ya uwekezaji mzuri wa soka na kuachwa kubabaishwa na timu zinazojiita vigogo.

Tangu kuibuka kwa timu ya Mbeya City, nilipenda aina ya soka lake. Kuna uwezekano mkubwa soka letu likapanda chati kwa kuzalishwa wachezaji wazuri kutoka katika timu za kawaida huko mikoani, maana soka halipo Simba na Yanga tu.

Huu ndio ukweli hivyo ni wakati wetu kujivunia na kuwaunga mkono mabingwa wapya, timu ya Azam FC, huku nikishindwa kuvumilia kama yupo anayeumizwa na matokeo haya.

Ndio maana nasema, hizi timu za kina Doto na Kulwa zifikie wakati zithaminiwe kwa ukongwe wao ila si kwa soka lao. Hazina kitu kabisa hizi.
Zimechoka, zimeishiwa. Ni Baraka ya majina tu, ila uwanjani ni sifuri.
Tuonane wiki ijayo.
+255712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...