https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, March 17, 2015

Yanga na Platinumz ya Zimbabwe yaingiza Milioni 91, Simba kuwavaa Mgambo Shooting ya Handeni Uwanja Mkwakwani kesho

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
MECHI ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika kati ya Yanga dhidi ya timu ya FC Platinum ya Zimbambwe iliyofanyika mwishoni mwa wiki katika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es salaam imeingiza jumla ya milioni 91,660,000 baada ya kuingiza watazamaji 14,563.

Msemaji wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Baraka Kizuguto, aliuambia mtandao huu kuwa mgawanyo wa mapato katika mchezo huo ni, VAT 18% sh. 13,982,033, Gharama ya tiketi sh. 12,380,000, Uwanja 15% sh. 9,794,694.92, Gharama za mchezo 15% sh. 9,794,694.92, TFF 5% sh. 3,264,898.31, CAF 5% sh. 3,264,898.31 na Yanga kupata 60% sawa na sh.39.178,779.66.

Katika hatua nyingine, ligi Kuu ya Vodacom inatarajiwa kuendelea kesho (jumatano) kwa viwanja vitatu kutimua vumbi, Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam ambapo Yanga watawakaribisha Kagera Sugar mchezo utakaoanza majira ya saa 10 kamili jioni.

Jijini Tanga maafande wa Mgambo Shooting watakua wenyeji wa Simba SC katika mchezo utakaofanyika uwanja wa Mkwakwani, huku jijini Mbeya wenyeji Mbeya City watawakaribisha timu ya ya Stand United kutoka mkoani Shinyanga kwenye uwanja wa Sokoine.

 Aidha, msafara wa watu 25 wa timu ya Taifa ya Tanzania ya Wanawake (Twiga Stars), unatarajiwa kuondoka nchini siku ya ijumaa kuelekea nchini Zambia kwa ajili ya mchezo wake wa kwanza dhidi ya timu ya Taifa ya Wanawake ya Zambia siku ya jumapili.

Twiga Stars inaanzia hatua ya pili katika kuwania kufuzu kwa Fainali za Afrika kwa Wanawake baada ya kuwa katika nafasi za juu kwa viwango barani Afrika, na endapo itafanikiwa kuwaondoa Wazambia itafuzu moja kwa moja kwa fainali hizo.

Msafara utaongozwa na Blassy Kiondo (Mjumbe wa Kamati ya Utendaji), Beatrice Mgaya (kiongozi msaidizi), Rogasin Kaijage (kocha mkuu), Nasra Juma (kocha msaidizi), Furaha Francis (Meneja), Christine Luambano (Daktari) na Mwanahamis Abdallah (Mtunza vifaa).

Wachezaji watakokweda Zambia ni Asha Rashid, Mwajuma Abdallah, Mwanahamis Omar, Donisi Minja, Amina Bilal, Fatuma Bashiri, Esther Chabruma, Shelda Mafuru, Maimuna Kaimu, Najiat Abbas, Stumai Abdalla, Fauma Issa, Thereza Yona, Fatuma Hassan, Fatuma Omary, Sophia Mwasikili, Fatuma Khatibu na Etoe Mlenzi.


Wakati huo huo, timu ya Taifa ya Tanzania ya soka la ufukweni (Beach Soccer) inatarajiwa kuodoka siku ya alhamisi kuelekea jijini Cairo nchini Misri kwa ajili ya mchezo wa marudiano kuwania kufuzu kwa fainali za Mataifa Afrika kwa soka la ufukweni utakaofanyika siku ya jumapili.

Tanzania inapaswa kupata ushindi katika mchezo wa marudiano dhidi ya Misri utakaofanyika siku ya jumapili jijini Cairo ili kufuzu kwa fainali za soka la ufukweni barani Afrika zitakazofanyika visiwa vya Shelisheli kufuatia kupoteza mchezo wake awali uliofanyika Escape 1 jijini Dar es salaam mwishoni mwa wiki.

Msafara wa timu ya Beach Soccer utakaoondoka na shirika la ndege la Ethiopia, utaongozwa na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Ahmed Msafiri Mgoyi, kocha mkuu John Mwansasu, kocha msaidizi Ali Sheikh Alhashby, meneja Deogratius Baltazar na daktari wa timu Dr Leonidas Rugambwa.

Wachezaji ni Rajabu Chana Kipango, Ahmed Rajab Juma, Roland Revocatus Kessy, Samwel Sarungi Opanga, Feisal Mohamed Ussi, Mohamed Makame Silima, Mwalimu Akida Hamad, Juma Sultan Ibrahim, Kashiru Salum Said na Ally Rabby Abdallah.





No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...