https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, March 04, 2015

MGODI UNAOTEMBEA:Ni punguani pekee anayefurahia kifo cha Kapteni Komba

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
NAPOKEA simu ambayo nashindwa kuielewa. Simu hii inatoka kwa rafiki yangu anayeishi mjini Dodoma, anayejulikana kwa jina Mustafa Mussa Seiph. Kijana huyu ananiuliza juu ya habari za kifo cha Mbunge wa Mbinga Magharibi, Kapteni  John Komba.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete, akimuaga marehemu Kapteni John Komba.
Komba amerafiki Dunia  huku akiwa anategemewa kwa kiasi kikubwa kwa jimbo lake la Mbinga Magharibi, bila kusahau Chama Cha Mapinduzi kinachojiandaa na Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Mwezi Oktoba mwaka huu nchini kote.

Kuulizwa juu ya kifo cha Komba kiliendelea kutoka kwa watu tofauti waliokuwa wameshangazwa na habari hizo juu ya msiba wa nguli huyo wa muziki, ambaye mara kadhaa nyimbo zake zimekuwa zikitumika kwa matukio muhimu. 
 
Marehemu Kapteni John Komba, enzi za uhai wake
Baada ya kufuatilia katika vyanzo tofauti, hatimae nilikubali matokeo kuwa Kapteni Komba hatupo naye duniani, yani ametangulia mbele ya haki, Februari 28 katika Hospitali ya TMJ, jijini Dar es Salaam, akisumbuliwa na ugonjwa wa kisukari. Ni majonzi makubwa kumpoteza mtu kama Komba, hii ni kutokana na umuhimu wake ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Katika kufuatilia suala la kifo cha Komba, mtu anaweza kufika mbali kwa kuona ni bora angebaki yeye na kuondolewa watu kadhaa ambao kwa namna moja ama nyingine wamekuwa wa kawaida ndani ya chama na serikali kwa ujumla.

Hata hivyo, wakati tunaendelea kuomboleza kifo cha Komba, wanajitokeza wachache wenye roho mbaya na kufurahia kifo chake. Kwanini? Ni binadamu gani mwenye roho ya utu anayeweza kufurahia kifo cha binadamu mwenzake?

Hata jamii hiyo inatofautiana kisera, kidini au kiitikadi bado si sababu ya kuona mtu anashangilia kifo cha mwenzake, kama anavyoweza kushangilia mnyama aliyeangushwa. Nchi yetu yenye amani na utulivu, watu wa aina hii wanatokea wapi.

Inashanaza na kuumiza. Ni punguani pekee anayefurahia kifo cha Kapteni Komba. Ingawa alikuwa mwana CCM, lakini pia alikuwa mbunge na mwakilishi wa wananchi wa jimbo la Mbinga Magharibi Tanzania Bara.

Hakuwa na uadui kiasi hicho. Ndio maana tulishuhudia watu wengi wakipokea kifo cha Komba kwa masikitiko makubwa. Nani atairithi sauti yake. Nani atatumia muda mchache kutoa nyimbo bora zinazosimamia uzalendo na kuhamasisha mengi nchini kwetu.

Inasikitisha kuona siasa zinaondoa utu wetu. Kama viongozi wa upinzani wote wameumizwa na kifo cha Komba, mfuasi gani anayeweza kuwa tofauti na wakubwa wao? Hata kama alikuwa na jambo lisilofurahisha wachache wao, bado sio sababu ya kuanza kumdhihaki kwa namna moja ama nyingine, hata pale tunapoliona jeneza lake.

Binadamu duniani tunapita tu. Safari yetu ni moja. Unapoona mwenzako ametangulia mbele za haki, jua na wewe unafuata. Huo ndio ukweli. Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk Willbroad Slaa, alizungumzia kifo cha Komba kwa huzuni za aina yake.

Kama hivyo haitoshi, Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, alionyesha mapenzi kwa Komba. Idadi kubwa ya viongozi kutoka vyama vya upinzani walionekana kwenda kwa wingi kumuaga marehemu Komba, aliyezikwa jana kijijini kwao Lituhi.

Hii ni kuonyesha kuwa upinzani na kushindana ni kwenye siasa tu. Inapotokea suala la kifo, hakika kila mmoja wetu anapaswa kuumia. Kama hivyo ndivyo, hakika nawashangaa wanaotumia muda mwingi kumdhihaki, wakitumia mwanya huo kutokana na misimamo yao tofauti.

Hizo sio siasa. Angalia, Komba alikuwa akiamini kuwa anayestahili kumrithi Rais, Dr Jakaya Mrisho Kikwete ni Edward Lowassa tu. Alilisema hili mchana na usiku. Alisimamia kwenye hoja yake hiyo bila woga wowote. Lakini kuonyesha ukomavu wa kisiasa na pia huzuni katika matatizo, bado haikuwa sababu ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, kuacha kuhudhuria msiba wa mwanasiasa huyo.

Si Membe tu, kundi la wagombea urais wengi ndani ya CCM walimiminika kwa wingi kuomboleza msiba huo bila kuangalia Komba aliwaunga mkono au aliwapinga. Ndio siasa zinavyotaka moyo na uzalendo wa hali ya juu.

Ukiacha katika majukwaa ya kisiasa, bado sote ni binadamu na Watanzania halisi. Tunapaswa kuishi kwa upendo. Hatupaswi kufurahia matatizo yanayotokea wenzetu. Huo si ubinadamu. Ni zaidi ya unyama usiostahili kuungwa mkono.

Mara baada ya kupata taarifa za msiba huo, sikuridhishwa hata kidogo juu ya watu waliokuwa wakisambaza picha mbaya za marehemu Komba. Wengine walifika mbali kwa kusambaza picha ya saa chache baada ya kifo chake.

Bado najiuliza. Watu wa aina hii hawajui uchungu wa kufiwa? Hivi kama aliyefariki ni baba zao, mama zao au mtu wao wa karibu anaweza kupata ujasiri wa kuisambaza picha ya marehemu? Hata kama anao moyo huo, bado hauwezi kumtuma awatumie picha isiyoridhisha wengine.

Huu si uungwana. Fikiria usambaziwe picha ambayo kiuhalisia tu haifai, utajisikiaje? Kama sababu ni siasa, je picha hizo za marehemu zimesambazwa na Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe, Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalimu au viongozi wengine?

Upuuzi huo unafanywa na watu wasiofahamu hata gharama za ada ya uanachama wa Chadema kwa kipindi cha mwaka mmoja. Watanzania tusifike huko. Msiba wa Komba si wa CCM na familia yake tu, ila Watanzania wote wameguswa.

Kabla ya kuingia kwenye siasa, Komba alikuwa mwalimu. Pia akawa mwanajeshi. Nafasi zote hizo zilikuwa ni za kuwatumikia Watanzania wote. Na kama kelele zinakuja kwa sababu ya kupingana juu ya maoni ya Katiba, sidhani kama ni sahihi.

Hii ni kwa sababu kila mtu alikuwa na ruhusa ya kutoa maoni yake aliyoona yanafaa kwa ajili ya kujenga mustakabali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na si Komba tu, ila inapotokea msiba, hakuna haja ya kuonyesha chuki dhidi ya wenzetu hao.

Tuwaombee dua tukiamini nasi tunaelekea huko. Hakuna atakayeishi milele. Leo ni Komba, kesho ni wewe au mimi. Pamoja na mambo hayo machache ambayo wasiojua nini maana ya siasa wanalalama, bado Komba alikuwa mmoja wa viongozi makini na wenye mchango katika Taifa letu.

Komba aliweza kusimamia hoja zake bila haya wala soni.  Siasa sio chuki wala uadui. Mtu anayeweza kuudhihaki mwili wa marehemu huyo ana walakini. Ni punguani pekee anayeweza kufurahia msiba wa Komba au binadamu mwenzake yoyote.

Watanzania sisi wote ni wamoja. Rais Kikwete alidhihirisha namna gani kifo cha Komba kimemgusa yeye na Watanzania wote baada ya kushindwa kujizuia kutoa chozi. Wengine walionekana kutoa chozi ni Katibu Mkuu mstaafu wa CCM, Yusuf Makamba na wengineo wengi waliomiminika katika Viwanja vya Karimjee kumuaga Kapteni Komba.

Huenda viongozi hao wa CCM walijaribu kuvuta picha katika kampeni zijazo. Lakini pia wengine wanajaribu kuangalia namna gani umuhimu wa Komba ulipaswa kuendelea kuwapo katika nchi yetu inayopambania maisha bora kwa kila Mtanzania.

Ni kutokana na hilo, naomba Watanzania tuwe wamoja katika kumuombea marehemu Komba akapumzike kwa amani, sanjari na kuomba dua kwa viongozi na wananchi wote katika sekeseke la uchaguzi lililozidi kushika kasi.

Hakuna haja ya kumdhalilisha marehemu hata kama kuna aliyokuwa akiyafanya huvutiwi nayo, hii ni kwa sababu hakuna aliyekamilika hapa chini. Nenda Komba. Tutakumbuka, ila ni punguani pekee anayefurahia kifo chako.
+255712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...