https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, March 18, 2015

Mgambo Shooting yaiumbua Simba kwa kuwachapa 2-0, Yanga SC yaichapa Kagera Sugar bao 2-1 Taifa

Na Mwandishi Wetu, Tanga
TIMU ya Mgambo Shooting yenye maskani yake Kabuku, wilayani Handeni, mkoani Tanga, leo imeiadhibu timu ya Simba kwa kuwafunga bao 2-0. Katika mchezo wa Ligi ya Tanzania Bara, uliochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga.

Mabao ya Mgambo yalifungwa na Ally Nassoro dakika ya 44 kipindi cha kwanza, akiunganisha pasi ya Fully Maganga na kuibua shangwe kwa mashabiki wao, huku likiwanyong’onyesha wale wa Simba, waliokuwa na hamu ya timu yao kuibuka na ushindi.

Bao la pili lilifungwa na Malimi Busungu dakika ya 66 kufuatia kipa wa Simba, Ivo Mapunda kumchezea madhambi Fully Maganga ndani ya eneo la hatari na mwamuzi Amon Paul kuamuru ipigwe penati iliyozaa bao hilo la pili hivyo kuzamisha jahazi la timu hiyo ya Simba.

Kwa ushindi huo, Mgambo sasa imefikisha pointi 23, huku ikitakiwa kufanya bidii katika kujinusuru ili wagosi hao wa Kaya wasiweze kushuka daraja katika Ligi iliyokuwa na ushindani wa aina yake kutokana na timu zote kupania kufanya vizuri.

Kufungwa kwa timu hiyo ya Simba kumeondoa furaha yote ya kuwafunga watani zao wa jadi Yanga SC, waliyoupata hivi karibuni. Wakati Simba ikipata kipigo hicho, wenzao Yanga wameibuka na ushindi wa bao 2-1 dhidi ya Kagera Sugar, mchezo utakaopigwa katika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.




No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...