https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, December 24, 2013

Umeme sasa bei juu kuanzia Januari Mosi mwakani


Taarifa ya EWURA YA bei mpya za umeme zitakazoanza kutumika Januari, Mosi,2013
Tarehe 11 Oktoba 2013, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) liliwasilisha maombi ya kurekebisha bei ya umeme kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA). TANESCO ilipendekeza kuongeza bei kwa asilimia 67.87 kuanzia tarehe 1 Oktoba 2013, asilimia 12.74 kuanzia tarehe 1 Januari 2014 na asilimia 9.17 kuanzia tarehe 1 Januari 2015.

Vilevile TANESCO waliomba kuidhinishwa kwa kanuni ya kurekebisha bei ya umeme kulingana na mabadiliko ya bei za mafuta, mfumuko wa bei na mabadiliko ya thamani ya shilingi ya kitanzania. Aidha, TANESCO iliomba kuidhinishwa viwango vya gharama za kuunganisha umeme vinavyozingatia ruzuku inaliyotolewa na Serikali, na kuidhinishwa tozo mbalimbali kwa huduma zitolewazo na TANESCO.

Kwa mujibu wa TANESCO, kupitishwa kwa maombi haya kutaliwezesha Shirika (a) kupata fedha za uendeshaji na uwekezaji wa miundombinu, (b) kulifanya Shirika liweze kukopesheka na hivyo kuwezesha kupata mikopo yenye masharti nafuu, (c) kuliwezesha Shirika kukabiliana na ongezeko la mahitaji ya umeme kwenye Gridi ya Taifa, na (d) kuongeza uwezo wa 
kufanya matengenezo ya mara kwa mara ya miundombinu iliyopo ili kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa huduma za umeme wa uhakika kwa wateja.

Itakumbukwa kwamba bei za umeme zinazotumika hivi sasa ziliidhinishwa mwezi Januari 2012. Bei hizo zilipanda kwa asilimia 40.29 ikilinganishwa na maombi ya TANESCO ambapo ilipendekeza bei zipande kwa wastani wa asilimia 155. Sababu ilikuwa ni kuongezeka kwa gharama za uendeshaji kulikosababishwa na hali ya ukame katika maeneo yanayotiririsha maji katika mabwawa ya kuzalishia umeme, toka mwaka 2011. 

Hali hiyo ilipelekea TANESCO kulazimika kununua umeme kwa gharama kutoka kwa wazalishaji wa dharura (Emergency Power Producers). Hali ya maji katika mabwawa ya kuzalishia umeme bado sio nzuri na hivyo TANESCO itaendelea kununua umeme kutoka kwa wazalishaji wa dharura (Emergency Power Producers).
USHIRIKISHWAJI WA WADAU
Kulingana na Kifungu Na. 19(2) (h) cha Sheria ya EWURA, Mamlaka ilifanya Taftishi ili kupata maoni juu ya ombi la kurekebisha bei za umeme. Ukusanyaji wa maoni ulihusisha pia mikutano minne (4) iliyofanyika Iringa na Shinyanga tarehe 15 Novemba 2013, Bagamoyo tarehe 20 Novemba na kuhitimishwa Dar es Salaam tarehe 22 Novemba 2013. Aidha, tarehe 6 Desemba 2013, EWURA iliitisha mkutano wa mwisho wa wadau wakiwemo wawakilishi kutoka Wizara ya Nishati na Madini(MEM), TANESCO, Shirika la Umeme la Zanzibar (ZECO), Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania, Baraza la Watumiaji na Baraza la Ushauri la Serikali, Umoja wa Wazalishaji wa Saruji wa Afrika Mashariki, na kiwanda cha ALAF. Katika mkutano huo EWURA iliwasilisha mwelekeo wa maamuzi kuhusu maombi ya TANESCO na namna zilivyokokotolewa. Wadau walipewa fursa ya kutoa maoni yao kuhusu mwelekeo wa bei na maoni yao yamezingatiwa katika kufikia maamuzi ya mwisho.
UCHAMBUZI NA UAMUZI
Kwa kufuata sheria na kanuni zinazoelekeza kuhusu uchambuzi wa bei ya umeme, EWURA ilifanya uchambuzi wa kifedha na kiufundi ili kubaini uwezo wa TANESCO katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku. Uchambuzi uliangalia utendaji wa Shirika la TANESCO katika miaka iliyopita na pia iliangalia majukumu yanayoikabili TANESCO katika miaka mitatu ijayo. EWURA imebaini kwamba hali ya kifedha ya Shirika la Umeme sio nzuri. Shirika limeendelea kupata hasara, ambayo iliongezeka kutoka shilingi bilioni 47.3 katika mwaka 2010 na kufikia shilingi bilioni 223.4 mwishoni mwa mwaka 2012. Pamoja na mapungufu ya kiufanisi, sababu kubwa ya ongezeko la hasara ni kuongezeka kwa gharama za uzalishaji wa umeme ambao TANESCO inanunua kutoka kwa wazalishaji binafsi. Hali hii imelifanya shirika kushindwa kulipa madeni yake ya muda mfupi na ya muda mrefu, ambayo yamelibikizwa na kufikia TZS 456.8 bilioni tarehe 22 Novemba 2013, hali ambayo inatishia uendelevu wa huduma ya umeme hapa nchini.
Mamlaka imetumia Kanuni ya Ukokotoaji wa Bei kama ilivyopendekezwa na AF-MERCADOS wakati wa kukokotoa mahitaji ya mapato ya TANESCO. Kanuni hiyo inawezesha kukokotoa bei zinazolandana na gharama halisi kwenye mfumo wa umeme na kuzigawa kwenye makundi ya watumiaji umeme, kadiri kila kundi linavyosababisha gharama kwenye mfumo wa umeme kwa mujibu wa mahitaji ya Sheria ya Umeme ya 2008 Kifungu cha 23(2)(f).
EWURA imejiridhisha kwamba, ufumbuzi wa matatizo ya kifedha ya TANESCO, unahitaji njia/mikakati miwili itekelezwe kwa pamoja:
kuongeza bei ya umeme ili kufikia bei inayokidhi gharama halisi (Cost Reflective Tariff); na
TANESCO kupata mkopo wa gharama nafuu ama ruzuku kutoka Serikalini ili kulipa limbikizo la madeni ya Shirika.
Bodi ya Wakurugenzi wa EWURA, katika kikao chake cha tarehe 10 Desemba 2013 pamoja na mambo mengine, ilitoa maamuzi ya ongezeko la bei za umeme kwa viwango mbalimbali kwa makundi mbalimbali ya wateja, kama ifuatavyo:
Kundi D1: Hili ni kundi la wateja wadogo wa majumbani, hasa vijijini, ambao hutumia wastani usiozidi wa Uniti 75 kwa mwezi. EWURA imeongeza wigo wa mahitaji ya umeme na kufikia uniti 75 kwa mwezi, lengo likiwa ni kuongeza idadi ya wateja wa TANESCO wanaoweza kulipa kidogo kwa matumizi ya umeme kwa kiwango hicho, na pia kuwahamasisha kutumie zaidi umeme. Awali kundi hili lilikuwa linatunia wastani wa matumizi ya uniti 50 kwa mwezi. Bei mpya ni shilingi 100 kwa uniti moja, kutoka shilingi 60 za sasa, sawa na ongezeko la shilingi 40.
Kundi T1: Hili ni kundi la watumiaji wakubwa wa umeme majumbani, biashara ndogondogo, mashine za kukoboa na kusaga nafaka, taa za barabarani, mabango n.k. Bei iliyoidhinishwa ni shilingi 306 kwa uniti moja, ikiwa ni ongezeko la Shilingi 85 ya bei ya sasa. TANESCO ilipendekeza ongezeko la shilingi 131.
Kundi T2: Hili ni kundi la watumiaji umeme wa kawaida ambao hupimwa katika msongo wa volti 400, na ambao matumizi yao ya wastani kwa mwezi ni zaidi ya uniti 7,500 wateja wafanyabiashara kubwa, viwanda vya kati. Bei ya nishati iliyoridhiwa ni shilingi 205 kwa uniti moja, sawa na ongezeko la shilingi 73 ya bei ya sasa. TANESCO walipendekeza ongezeko la shilingi 145 ya bei ya sasa.
Kundi T3-MV: Hili ni kundi la wateja wakubwa kama viwanda vikubwa waliounganishwa katika msongo wa kati (Medium Voltage). EWURA imeidhinisha bei ya nishati kwa kiwango cha shilingi 166 kwa uniti moja, sawa na ongezeko la shilingi 45 ya bei ya sasa. TANESCO walipendekeza ongezeko la shilingi 148 kwa uniti moja.
Kundi T3-HV: Hili ni kundi la wateja wakubwa waliounganishwa katika msongo wa juu (High Voltage – Voti 66,000 na zaidi) ikiwa ni pamoja na ZECO, Bulyanhulu, na Twiga Cement. Bei iliyoidhinishwa ni shilingi 159 kwa uniti moja, sawa na ongezeko la shilingi 53 la bei ya sasa. TANESCO waliomba ongezeko la shilingi 80 kwa uniti moja.
Bei ya umeme itakuwa inarekebishwa kila baada ya miezi mitatu kulingana na mabadiliko ya kiwango na bei za mafuta; mfumuko wa bei, mabadiliko ya thamani ya fedha, na upatikanaji wa ruzuku toka Serikalini.
Vilevile, TANESCO inatakiwa kutekeleza miradi ya uwekezaji iliyoainishwa kwa kutumia fedha zitakazokusanywa kutokana na bei zilizoidhinishwa. EWURA inaweza kurekebisha bei ya umeme ya TANESCO kila mwisho wa mwaka 2014 na/au mwaka 2015 endapo TANESCO itashindwa kutekeleza miradi iliyotajwa katika Jedwali husika. Marekebisho hayo yatatokana na makadirio ya gharama za miradi ambayo haikutekelezwa.
Kutokana na matazamio ya kuwa na mabadiliko makubwa katika uzalishaji wa umeme (generation mix) katika mwaka 2015 na kuendelea, kutokana na matarajio ya kuongezeka kwa kwa upatikanaji wa gesi asilia, EWURA itafanya utafiti kubaini gharama halisi (Cost of Service Study) ya huduma ya umeme kwa wakati huo. Hivyo, bei zilizoidhinishwa zitatumika mpaka mwaka 2016, kama utafiti unaotazamiwa kufanywa hautakamilika kabla ya mwisho wa mwaka 2015.
EWURA ililinganisha bei za umeme kwa kila Uniti, katika nchi za Afrika ya Mashariki, na kuona kuwa bado bei za umeme za Tanzania zipo chini ukilinganisha na bei za katika nchi jirani kama inavyoonyeshwa hapa chini, kwa makundi mbalimbali ya watumiaji umeme.
Pamoja na maamuzi hayo, Bodi ya Wakurugenzi wa EWURA, pia iliagiza TANESCO kutekeleza yafuatayo:

  • kuzalisha umeme kwa kutumia mitambo yenye gharama nafuu ("least cost merit order") na kuwasilisha ripoti kwa Mamlaka katika kila mwezi ikionyesha uzalishaji halisi na mpango wa uzalishaji kama ilivyoidhinishwa na EWURA;



  • kuhakikisha kuwa zabuni za miradi ya uzalishaji umeme zinatolewa kulingana na mahitaji kama ilivyoidhinishwa kwenye Mpango wa Umeme wa Taifa (Power System Master Plan). Miradi yote mipya lazima ipatikane kwa njia ya ushindani kwa kufuata Sheria ya Umeme, "Public Private Partnership Act", Sheria ya Manunuzi ya Umma na Kanuni husika;



  • kuwasilisha ripoti kila baada ya miezi mitatu kuhusu viashiria vya takwimu za ubora na uhakika wa umeme (supply and reliability) katika misongo ya 11kV, 33 kV, 66 kV, 132 kV, na 220 kV kwa kila mkoa kwa ajili ya uhakiki. Takwimu husika zinatakiwa kuonyesha jumla ya masaa mteja aliyokosa umeme kwa kila njia ya umeme ("feeder"), kukosekana kwa umeme kulikopangwa (planned outages), na ambao haukupangwa (unplanned outages), idadi ya matukio ya kukosa umeme katika kila "feeder", idadi ya wateja wanaohudumiwa na kila "feeder", idadi ya wateja walioathirika na katizo la umeme katika kila "feeder" na kiasi cha umeme kilichokosekana kutokana na katizo hilo (total unserved energy in kWh);



  • kuwasilisha kwa Mamlaka, katika kipindi cha miezi mitatu baada kuanza kwa Agizo hilo la Mamlaka, mpango wa utekelezaji wa "Demand Side Management Programme" ili uidhinishwe;



  • kupunguza kiwango cha upotevu wa umeme (technical and non-technical losses) katika mtandao wa usambazaji kutoka asilimia 19 ya mwaka 2012 hadi asilimia 15.1 ifikapo mwisho wa mwaka 2015;



  • kubuni mikakati ya kupambana wizi wa umeme utokanao na uunganishaji umeme usio halali, na kuondoa ucheleweshaji usio wa lazima katika kutunganisha wateja wapya;



  • kuhamisha wateja walio katika kundi la D1 kwenda T1 endapo matumizi yao ya mwezi yatazidi uniti 75 kwa miezi mitatu mfululizo;



  • kuwasilisha kwa Mamlaka, kabla au tarehe 31 Machi, 2014, Mpango wa kuwawekea wateja wake mita za LUKU na AMR ili kupunguza wateja wanaotumia mita za zamani (conventional meters);



  • kuwasilisha kwa Mamlaka, kila baada ya miezi mitatu, taarifa/ripoti ya ukusanyaji wa madeni kutoka kwa wateja wake ili kuongeza mapato ya Shirika;



  • kutoa elimu kwa wateja wake kuhusu haki na wajibu wa wateja kwa mujibu wa Mkataba wa Huduma kwa Wateja na kushughulikia kero za wateja kama inavyoelekezwa katika Mkataba husika na Kanuni za Umeme;



  • kuwasilisha kwa Mamlaka, maombi ya marekebisho ya bei yatokanayo na mabadiliko ya bei za mafuta, mfumuko wa bei na ubadilikaji wa thamani ya fedha; Ukokotoaji wa marekebisho hayo utakuwa kama ulivyoainishwa katika Kanuni za Kupanga Bei za Umeme za mwaka 2013 (Electricity (Tariff Setting) Rules, 2013);



  • kuendelea kutoa taarifa kwa Mamlaka kuhusu hali ya kifedha na kiundeshaji. Taarifa hizi zitatumiwa na Mamlaka katika kutathmini utendaji wa TANESCO ikilinganishwa na mashirika mengine ya umeme katika nchi jirani ili kuboresha utendaji wake. Tathmini hii pia itatumiwa na Mamlaka katika kubaini uhalali wa maombi ya baadae ya kurekebisha bei;



  • kuwasilisha kwa Mamlaka, kabla au tarehe 31 Machi 2014, mpango wa utekelezaji wa kila sharti katika Agizo la EWURA.

Bei mpya za umeme zitaanza kutumika tarehe 1 Januari 2014. Ni matarajio ya EWURA kwamba TANESCO watatumia fursa hii kutoa huduma bora zaidi za umeme na kuhakikisha kuwa wanashughulikia malalamiko ya wateja kila yanapojitokeza ili kurejesha imani kwa Shirika la Umeme la TANESCO.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...