https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, October 30, 2012

Waigizaji waanzie kwenye makundi

                            Wema Sepetu, msanii wa filamu Tanzania
Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

KWA wasanii wa maigizo, wanafahamu namna gani makundi yanavyoweza kuwaibua na kuwapa vipaji halisi, kuliko wale wanaoingia kwenye sanaa kwasababu ya mwonekano wao, mvuto wao wa sura au uwezo wa kuzungumza lugha ya Kingereza.

Hata kama uwe na mvuto wa kiasi gani, lakini uwezo wako utazidi kuimarika endapo utapata nafasi ya kufanya mazoezi na vikundi vya sanaa vinavyofundisha sanaa ya ukweli. Kwanini nasema hivyo?

                          Jacob Steven (JB) mkali wa filamu Tanzania
Wasanii waliobukia kwa miaka miwili hii, wengi wao wamekutwa klabu wakinywa pombe au vileo vingine na kuombwa washiriki kwenye filamu zao. Kwa makubaliano wanayojua wenyewe, wasanii hao hupewa (Script) maneno yanayoandikwa kwenye karatasi kwa ajili ya kuzungumzwa na yule anayetakiwa kupigwa picha.

Akishafanya hivyo, masuala mazima ya kurekodi filamu hiyo huanza kwa kutafuta (location) maeneo ya kupigia picha yao, kabla ya miezi miwili baadaye filamu hiyo kutangazwa eti tayari imeshakamilika.

                   Wolper akionyesha mvuto wake mbele ya kamera
Msanii wa aina hiyo siyo tu anasumbua katika filamu zake kwa kutovaa uhusika wa kweli, bali pia hukosa maadili na namna gani ya kujiweka katika kundi la wasanii muhimu wa Tanzania, huku pia akikosa kufahamu mbinu za uigizaji.

Msanii wa aina hiyo, kamwe hawezi kufahamu kuigiza jukwaani, wenyewe wanaita (Stage Drama). Ingawa wasanii walio wengi hawawezi sanaa ya aina hii maana ni ngumu, lakini sio kweli kama watakuwa hawajui taratibu za uigizaji huo.

Sitaki kuamini kuwa wasanii waliopitia kwenye makundi hawajui jinsi ya kuigiza jukwaani huku mwiko wa kwanza wa kutowapa mgongo watu wete ukumbini humo akitakiwa kuzingatiwa kwa ajili ya kuonyesha umahiri wao.

                     Mkali mwingine wa filamu, Aunt EZEKIEL
Atakuwa anajua tu. Lakini sio wasanii wa leo. Wasanii hawa wanachoangaliwa wao ni sura zao au wanavyoweza kujikwatua na kuvaa ngozi za wazungu. Mimi sio mtaalamu sana wa sanaa ya maigizo, lakini nafahamu vitu vingi.

Pia naelewa umuhimu wa kuigiza sanaa za majukwaani. Ni nzuri zaidi. Wasanii wa wanaotaka kupewa Script leo wanafahamu lolote? Kama hawajui basi ni wakati wao kutafuta makundi na kupewa sanaa hiyo nzuri.

Wasipende kuigiza kwenye filamu tu. Sanaa hiyo ni nyepesi na kila mtu anajua. Sanaa ya filamu na tamthiliya kwenye luninga ni nyepesi na kila mtu ana uwezo wa kuifanya. Hata kama akishindwa kulia, basi atakamuliwa ndimu ili machozi yatoke.

                        Mkali mwingine wa filamu Tanzania, Irene Uwoya
Lakini sio sanaa ya jukwaani. Nani atakubali kuangalia mtu anakamuliwa ndimu kuonyesha machozi yake jukwaani. Ni wazi hawawezi. Lakini waliokomaa katika sanaa, wakianzia na makundi, walau mbinu hizo watakuwa wanajua.

Msanii aliyebobea katika uigizaji, akianzia kwenye makundi, hawezi kukosa chozi lake hata kwa dakika tatu tu. Lazima alie. Anajua mbinu zote. Namna ya kufanya na mbinu za kuonyesha ukomavu wake kwa wadau wa sanaa.

                             Mrisho Mpoto, msanii wa filamu na muziki wa asili
Nasema haya baada ya kuona sanaa yetu ya maigizo inazidi kupoteza dira ingawa wengi wanaibuka na kujipatia majina makubwa. Hao wote waliokuwa na majina makubwa leo sio wasanii wazuri.

Ukitaka kuamini hilo, wachukuwe ili waonyeshe ukomavu wao kwa kuonyesha sanaa ya jukwaani, ambayo mvuto wake ni mkubwa na inaweza kuwaingizia kipato. Sanaa ya majukwaani ni nzuri na ni ajira tosha kwa wasanii husika.

Kwa mfano, wasanii wa aina hiyo wanaweza kujiunganisha na kufanya maonyesho katika kumbi mbalimbali na watu wakaingia. Kwanini wasiingie? Wema Abraham Sepetu, ambaye kila mtu anamjua kwa urembo wake na jinsi anavyowika katika sanaa nani hatapenda kuingia ukumbini kumuona anavyofanya manjonjo yake.

Lakini ni dhahiri hawezi. Kwanza hata sauti yake ameijenga katika sanaa ya filamu tu na sio jukwaani. Ili aweze lazima kwanza ajitengeneze upya. Kwa kuhakikisha kwamba anaweza kufanya sanaa za aina zote.

                            Vicent Kigosi, Ray 
Kwa kulijua hilo, kuna kila sababu ya wasanii wetu kupenda kwanza kuanzia chini, kwenye vikundi vya sanaa mitaani kwao. Hata kama wakipata bahati ya kupita moja kwa moja kama walivyotoka wengine, lakini watafute sasa vikundi hivyo.

Vikundi vinaweza kuwafanya wakaishi maisha mazuri zaidi na heshima ya kujiita msanii mzuri anayeweza kubadilika wakati wowote. Kwa mfano, msanii kama vile Mrisho Mpoto, huyu hawezi kufa njaa hata kidogo.

Ni mjuzi wa sanaa za aina hiyo. Na ndio maana anapata safari nyingi za nje ya nchi kwa ajili ya kuonyesha sanaa yake. Nadhani hilo lazima watu walijuwe kwa ajili ya faida yao wenyewe. Naamini bila hivyo, watakuwa wasanii wenye majina makubwa, lakini kiuwezo wa uigizaji wanakuwa wepesi na badiliko lolote linaweza kuwaangusha.

Niwatakie sanaa njema.

0712 053949
0753 806087

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...