https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, December 21, 2015

Tanzania yajikita mstari wa mbele kushughulikia mgogoro wa nchini Burundi

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WAZIRI wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki Kikanda na Kimataifa, Balozi Dk Augustine Mahiga amesema Tanzania iko mstari wa mbele kushughulikia mgogoro unaoendelea nchini Burundi.

Balozi Mahiga alisema sio kweli kuwa Tanzania imekaa kimya na haijishughulishi na mgogoro huo, bali ilikuwa imekasimu kazi hiyo kwa Serikali ya Uganda kutokana na majukumu mazito yaliyokuwa yakiikabili nchi hususan Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba mwaka huu.

Alitoa kauli hiyo juzi alipozungumza na vyombo vya habari Arusha wakati wa ziara ya kujitambulisha kwa Bodi mpya ya Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) na kutembelea miradi mbalimbali ya kituo hicho.

Alisema Tanzania kutokana na kukabiliwa na mambo mbalimbali likiwemo la uchaguzi, kuchelewa kutangazwa kwa Baraza la Mawaziri ndipo ilipoamua kukasimu uongozi wake wa Uenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kwa Uganda ili kuanzisha mazungumzo kuhusu mgogoro huo.

Aliongeza kuwa baada ya Tanzania kuwa katika hali nzuri ya kujikita katika kutafuta suluhu ya mgogoro huo, ndipo yeye kama waziri wa masuala hayo, alipopokea maagizo kutoka kwa Rais John Magufuli ya kutakiwa kufanya maandalizi yote kwa ajili ya kuanza kwa mazungumzo hayo.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...