https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Tuesday, February 10, 2015

SIWEZI KUVUMILIA:Tumekubali kuwa na wanamichezo masikini?

NA KAMBI MBWANA, DAR ES SALAAM
IFIKIE wakati kama Taifa tuone haya pale tunaposhuhudia wingi wa wachezaji ambao mwisho wa siku ni masikini. Mchezaji anawika kwa nyakati kadhaa, lakini ukimuangalia mfumo wake wa maisha utagundua hakuna kitu chochote anachoweza kujivunia.

Mimi si wa kwanza katika kilio hiki. Watu mbalimbali wameshawahi kuonyesha malalamiko yao, wakiwamo wanamichezo wenyewe. Kabla ya kuhukumiwa kifungo cha miaka 3 jela, bondia tishio, Francis Cheka, mara kadhaa Amelia juu ya maisha yake kuwa magumu, licha ya umaarufu aliokuwa nao.

Ukiacha Cheka, wapo wengine ambao majina yao hayalingani kabisa na kipato chao, hususan hawa wanaocheza michezo tofuati na mpira wa miguu wenye unafuu katika jamii yetu.

Wachezaji kama vile Mbwana Matumla, Rashid Matumla, Francis Miyeyusho, Japhet Kaseba, unaweza kulia utakapogundua majina yao makubwa si sawa na kipato chao na maisha yao kwa ujumla.

Na hili ndio sababu kuu ya kuwaathiri wanamichezo hao kisaikolojia. Na suala hilo litazidi kuwazorotesha wao kimichezo. Kamwe siwezi kuvumilia. Ni wakati sasa wa wanajamii kuweka mipango yenye tija na mbolea.

Tuelezane ukweli na kuamua kwa dhati kufanya mambo yenye kusababisha maendeleo na mafanikio. Mabondia wetu na wanamichezo wote kwa ujumla wawekewe mazingira bora na rafiki.

Kwa bahati mbaya, matatizo yote hayo yanaanzia chini ya serikali kwa kupitia Wizara ya Habari, Michezo na Utamaduni ambako hakuna sera au zipo lakini zina matege.

Na ndio maana tumekuwa na wanamichezo wengi wenye majina, lakini ni masikini wa kutupwa. Hii si sawa. Tuweke mifumo mizuri si tu kwa ajili ya kuendeleza michezo, bali pia kuwapatia maisha bora wanamichezo hao ili waishi vizuri kulingana na majina yao.

Kuanzishwe mashindano, mapambano makubwa kwa mabondia wa Tanzania, sambamba na kuwekewa mifumo ya kutoka nje na kushiriki kwenye matukio makubwa yenye kuingiza fedha nyingi.

Kinyume cha hapo michezo na wanamichezo wetu wa Tanzania wataendelea kuwa hohe hahe. Tatizo hili si rafiki kwa wanamichezo wetu. Na pia ni sehemu inayoifanya michezo ishindwe kupiga hatua.

Ukiacha mpira wa miguu tena ule wa wanaume, michezo mingine kwa Tanzania inatoa ajira kwa wanamichezo wetu au inawapotezea muda tu, maana muda mwingi mazoezini, lakini hakuna wanachoambulia zaidi ya kufanikisha majina makubwa, lakini mfukoni sifuri.

Hii ni hatari na haiwezi kuvumilika. Nani anafurahia tatizo hili kwa wanamichezo wengi wa Tanzania? Je, wadau wa michezo na viongozi wanaliangalia suala hili kwa kirefu?
Serikali inachoweza wao ni kutoa pongezi tu au kutoa pole panapokuwa na msiba, lakini si kubuni au kusimamia sera zenye mashiko kwa ajili ya kuendeleza michezo na kuwapatia maisha bora wanamichezo na Watanzania kwa ujumla.

Tunapaswa kubadilika, kinyume cha hapo siwezi kuvumilia kuona wanamichezo wetu wanaendelea kuogelea kwenye wimbi la umasikini, hali ya kuwa wana vipaji kama vile vinavyowapatia utajiri nyota duniani kote.
Tuonane wiki ijayo
+255712053949

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...