https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, May 16, 2015

MKUTANO MKUU:Wanahisa wa CRDB wanavyopigania kuiweka juu benki yao



*Wafanya Mkutano Mkuu wa 20 AICC Arusha
*Dkt Kimei aanika mikakati ya kuipaisha CRDB

Na Kambi Mbwana, Aliyekuwa Arusha
NI kama vile uhai na mafanikio ya benki ya CRDB umejulikana upya, baada ya menejimenti, Bodi ya Wakurugenzi na Wanahisa kukubaliana kwenye Mkutano wao Mkuu wa 20 wa Wana Hisa uliofanyika Mei 9, mwaka huu.
Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB benki, Dkt Charles Kimei, akizungumza jambo katika Mkutano wa wanahisa wa benki hiyo jijini Arusha.
Mkutano huo ulifanyika katika Ukumbi wa Simba, kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha AICC, huku ukifurika wana Hisa wengi kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania.

Mtangazaji mkongwe nchini Tanzania,  Salimu Mbonde, akisikiliza kwa makini mkutano wa hisa wa benki ya CRDB, jijini Arusha.
 Katika mkutano huo ulioanza saa 3 asubuhi, mengi yalijadiliwa, ikiwamo ripoti ya wakaguzi na mwelekeo wa benki hiyo katika kufungua matawi, bila kusahau tawi lao lililokuwa nchini Burundi.

Katika mazungumzo yaliyofanyika jijini Arusha, Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Dkt Charles Kimei, anasema kwamba kufanyika kwa amani na mafanikio mkutano huo, ni kama vile benki yao imezaliwa upya.

Anasema biashara yoyote inayohusiana na wana hisa, kunahitaji mipango ya kukubaliana kwa pande zote, jambo linalowafanya menejimenti, bodi na wanahisa kuona ipo dhamira ya dhati ya kuhakikisha kwamba bendi yao inapiga hatua.

“Wanahisa ni watu muhimu na ndio maana tumekuwa tukifanya mkutano wa mwaka kwa ajili ya kupitisha ripoti, kutaja vipaumbele na kuangalia jambo gani la kufanya katika kuhakikisha kwamba benki yetu inakuwa bora zaidi.

CRDB ni kati ya benki bora nchini ambayo tumefanikiwa pia kuwa na tawi letu nchini Burundi ambapo hata hivyo kumekuwa na hali ya sintofahamu katika mambo ya kisiasa,” alisema.

Katika mkutano huo, baadhi ya wanahisa walitoa ushauri wao juu ya mwenendo bora wa benki yao, ikiwamo taratibu za ufunguaji wa matawi katika mikoa mbalimbali.

Awali, mkutano huo ulikuwa na dondoo kama vile kufungua mkutano, Kuchagua Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Mkutano Mkuu, Kuridhia ajenda ya mkutano, kuthibitisha kumbukumbu za Mkutano Mkuu uliopita, kujadili yatokanayo na kumbukumbu za Mkutano Mkuu wa 19, kujadili na kupokea taarifa ya Bodi ya Wakurugenzi na taarifa hesabu zilizokaguliwa za mwaka 2014.

Dondoo nyingine ni pamoja na gawio kwa mwaka 2014, hesabu zilizokaguliwa za mwaka ulioishia na Desemba 31 mwaka 2014, taarifa ya Bodi ya Wakurugenzi, kuidhinisha ongezeko la mtaji kwa kutoa hisa stahili (rights issue), kuidhinisha mapendekezo ya mabadiliko kwenye Katiba ya benki-Azimio Maalum, kuidhinisha ada ya wakurugenzi, kuteua wakaguzi wa hesabu, kuchagua wajumbe wa bodi, ikiwa ni pamoja na wajumbe wawili wa bodi watakaowakilisha kundi la wanahisa wenye chini ya asilimia moja, bila kusahau mjumbe mmoja wa Bodi atakayewakilisha kundi la wanahisa wenye hisa asilimia moja na kumi.

“Pia tulijadili dondoo kama vile kujadili mapendekezo kutoka kwa wanahisa, mengineyo kwa idhini ya mwenyekiti, kupanga mahali na tarehe ya mkutano ujao pamoja na kufunga.

“Kwa ujumla yote yaliyotajwa katika mkutano huo yalipitishwa kwa nguvu zote na wana hisa wenyewe, ikiwa ni njia sahihi ya kuiweka juu benki hii inayoheshimika sehemu mbalimbali za Tanzania, bila kusahau katika nchi nyingine za Afrika, ikiwamo Burundi,” alisema.

Mkurugenzi huyo Mtendaji wa CRDB Benki, Dr Kimei anasema moja ya mambo yaliyoifanya benki yao ifanye vizuri ni kutokana na kuwa wabunifu na kwenda na teknolojia, kama vile huduma ya SimBanking, Fahari Huduma na mengineyo.

Anasema katika huduma ya kutuma na kupokea pesa kwa njia ya simu imeshika hatamu ambapo watu wengi wameonekana kuvutiwa na ubora wa huduma hiyo pamoja na urahisi wake kulingana na utaratibu wa matawi uliokuwapo zamani.

Dkt Kimei anasema pamoja na kuboresha huduma hiyo ya simu banking, pia wanaendelea kuhakikisha kwamba wanafungua matawi mengi ili kuifanya benki yao iwe rahisi kuwatumikia wateja wao.

Awali walikuwa na matawi 103, lakini wamefika mbali zaidi kwa kufungua matawi 20, hivyo sasa watakuwa na matawi 123,  mashine za kutolea fedha yani (ATM) 374, bila kusahau mawakala wa fahari huduma 1,067.

Aidha Dkt Kimei aligusia pia huduma ya Microfinance Services Company Ltd, akisema kuwa uwapo wa kampuni hiyo tanzu ndani ya CRDB utazidi kuongeza mapenzi na ukuaji wa uchumi kwa kuwahudumia wajasiriamali wadogo kwa kupitia SACCOS.

Katika siku zijazo, huenda kampuni hiyo nayo ikatoa huduma yenyewe kwa kujiendesha ili kutoa huduma bora na kukuza heshima ya benki ya CRDB.
“Kauli mbiu yetu iwe ni mauzo, mauzo na mauzo, tukiamini kuwa kwa ushirikiano huu mkubwa uliopo kati yetu sisi watendaji na watumishi wote wa CRDB, Bodi ya Wakurgenzi, Wana Hisa, wateja wetu na serikali kwa ujumla, naamini tutakuwa juu na imara.

“Pamoja jitihada zote hizi, bado tunaamini kwamba tunapaswa kutumia gharama kubwa ili kuyaweka matarajio yetu katika mizania stahili, hasa bejeti ya ufunguaji wa matawi mengine, ukizingatia kuwa tawi moja linahitaji hadi Sh Milioni 700,” alisema.

Hata hivyo, muda wote huo wa Mkutano huo, wanahisa walionyesha umakini, usikivu pamoja na kuhoji baadhi ya vipengele wakitaka kujiridhisha na mwenendo wa benki yao.

Mwanahisa Gervas Ngikari, aliishauri Bodi na Mkurugenzi Mtendaji kutafuta namna ya kubana matumizi ili fedha nyingi zisipotee hovyo ili iwe njia ya kuiweka benki yao katika mafanikio makubwa, bila kusahau mapato ya wana hisa, akitia hofu kuwa hesabu zinaonyesha kila Sh 100 inayoingia, 60 yote inatumika, huku Sh 40 inayobakia ndio wanaogawana waliobakia, ikiwamo serikali, benki na Wana Hisa.

Hata hivyo hoja hiyo ilifafanuliwa vizuri kwa jicho la kiuchumi, kwamba yapo baadhi ya mambo yanayohitaji fedha, hususan ufunguaji wa matawi na mahitaji mengine muhimu kwa mustakabali wa huduma za kibenki kama sheria zinavyotaka, hivyo wanahisa wote kuridhia kila kilichosemwa katika Mkutano huo.

Mwanahisa Joachim Tarimo yeye aliishauri menejimenti na Bodi ya Wakurugenzi kuhakikisha kwamba benki yao inaingia nchini Kenya kufungua tawi ili kwenda sambamba na soko la kifedha, akisema ndio njia sahihi ya kuikuza benki yao.

Mwanahisa Anna David yeye aliishauri benki hiyo kubuni miradi na fursa nyingine  za kibiashara ili kuingiza fedha kwa njia nyingine, akitoa mfano wa uwekezaji wa majengo na mengineyo muhimu, akisema kuwa njia hiyo itaokoa pia fedha za gharama ya upangaji majengo na mambo mengine muhimu.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...