https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Saturday, July 30, 2016

MGODI UNAOTEMBEA: Tuzipinge siasa za mtaji wa damu zinazohitajiwa na Chadema

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
HATA vitabu vya dini vinatueleza binadamu tuzitii mamlaka halali tulizochagua wenyewe ili zituongoze. Ndio, inapotokea mtu anakwenda kinyume na maandiko hayo,  ni dhahiri hatufai, hastahili kuchekewa.
Kambi Mbwana, mwandishi wa makala haya.
Na kutii huko hakupo kwa mwananchi wa kawaida tu. Maadamu ni mamlaka halali, hapana shaka kila Mtanzania wa nchi yetu anapaswa kutii hilo bila kujali dini yake au itikadi yake ya kisiasa. Kwa bahati mbaya, tangu kuanzishwa kwa sheria ya vyama vingi, mwaka 1992, kumekuwa na kasumba ya baadhi ya viongozi wa upinzani, kufanya mambo ambayo ni kinyume, wakiwa na malengo yao binafsi.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dr John Pombe Magufuli pichani.
Malengo ya kutafuta sifa ya kuungwa mkono na wafuasi wao bila kujali wanafanya kitu kizuri au cha kijinga. Bahati mbaya mfumo huo kadri unavyozidi kupewa nafasi na wapinzani hao, dalili za wazi za kutowesha amani ya nchi yetu inazidi kuonekana. Kwanini isionekane? Utawekeje tone moja la damu kwenye nguo nyeupe na bado ukajindanganya kwamba nguo hiyo itaendelea kuvutia? Pamoja na dalili ya machafuko inayozidi kuonekana, bado hakuna juhudi zinazochukuliwa na wanasiasa kutoka mlengo wa upinzani, wakiamini siasa za kumwaga damu za wananchi wao ndizo zinazoweza kuwaweka juu.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe pichani.
Hili haliwezi kukubalika.  Watanzania tusikubali. Tumeshahudia mara kadhaa damu za Watanzania wenzetu zikimwagika bila soni wala haya. Machafuko ya kisiasa yanayoanzishwa na wanasiasa kama Arusha, Morogoro na katika maeneo mengine yameendelea kuonekana, huku chanzo chake kikiwa ni siasa chafu, nyepesi, zisizokuwa na tija kupewa nafasi hususan na chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Kwa mfano, Chama Kikuu cha Upinzani Tanzania (Chadema), kwa kupitia mwenyekiti wao Freeman Mbowe JUZI wametangaza kufanya maandamano na mikutano nchi nzima katika siku ya Novemba Mosi. Na mikutano hiyo itafanyika bila kuangalia imeruhusiwa na jeshi la Polisi au itazuiwa. Inawezekana kuandamana ni halali kwa mujibu wa Katiba, lakini pia busara na usalama lazima ziimarishwe kwa faida ya nchi yetu.

Kufanya maandamano yenye viashiria vya uvunjifu wa amani hakuwezi kuruhusiwa hata kama yamewekwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hii ni kwa sababu si Watanzania wote wanapendezwa na siasa za upinzani. Wapo ambao hawaungi mkono agizo lolote la upinzani. Na wengine si wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wala CUF. Isipokuwa wote ni Watanzania. Hivyo endapo hayo maandamano yatafanyika bila kufuata sheria, kanuni na taratibu tulizojiwekea, ni wazi kutakuwa ni kupoka haki ya kuishi na kulindwa kwa wengine watakaoathiliwa na maandamano hayo yasiyokuwa na kichwa wala miguu, kama wanavyotaka kufanya viongozi wa juu wa Chadema.
Ndio maana kunakuwa na taratibu. Nani asiyejua kuwa siasa za namna hiyo zimepelekea kifo cha Mtanzania mwenzetu, mwandishi wa habari Daud Mwangosi kule mkoani Iringa?

Ingawa Chadema wanasema mauaji hayo yamesababishwa na Jeshi la Polisi, lakini chanzo kikuu ni ghasia zilizoendeshwa na wao na wakiwa na nia waliyojua wenyewe, ikiwamo hii ya kujulikana kwa lazima bila kujali athari kutoka kwa baadhi ya Watanzania wasiokuwa na hatia. Licha ya kifo hicho au machafuko yaliyotokea katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu, wapinzani wameendelea kutembea katika njia ile ile, wakiamini ndio mtaji wao wa kisiasa ulipo. Hii haikubaliki. Watanzania tusikubali siasa za kumwaga damu zinazofanywa na kuhubiriwa na wanasiasa wa upinzani kwa sababu hazina faida kwetu. Tunachafua tunu ya Taifa letu.

Leo Mbowe anatangaza maandamano au mikutano isiyokuwa na ruhusa, lakini sidhani kama katika matukio hayo ataambatana na familia yake. Si ajabu watoto wake watakuwa wakiendelea na maisha yao iwe ndani ya nchi au nje, huku watoto wa masikini wakitaabishwa. Kuna vitu vingi vya msingi ambavyo wapinzani wanaweza kuvifanya kama karata yao katika siasa za nchi yetu. Nzuri zaidi, wamefanikiwa kuwa katika majimbo kadhaa wakiongoza kama wabunge, madiwani au mameya. Wakae chini watafute namna ya kufanya siasa zenye chembechembe za huruma, uzalendo na uwajibikaji ili iwe njia ya kupaisha gurudumu la maendeleo ya nchi.
Ni wazi wanayofanya hayana tija. Wanazalisha dalili za ghasia. Ghasia zinazoweza kutowesha amani ya nchi yetu. Nchi ambayo kila mtu ana haki ya kuilinda na kuidumisha amani ya Taifa letu kama wajibu wa kila mwananchi.

Kwanini tusijifunze kutii mamlaka? Kama wapinzani leo hawataki kutii mamlaka na ushauri wowote kutoka kwenye serikali iliyochaguliwa na Watanzania wengi, hata wao kesho wakichaguliwa ni wazi wengine hawatawatii. Jana akiwa mkoani Singida, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dr John Pombe Magufuli amewaeleza kuwa vitendo vyao vyovyote vibaya havitavumiliwa. Na pia akasema, kama wanataka kufanya siasa, basi wafanye kwenye majimbo yao, kwa wale waliofanikiwa kuwa wabunge.

Kauli ya Magufuli imekuja baada ya Chadema kutangaza maandamano yao na kuyapa jina la UKUTA wakisema yatafanyika nchi nzima Novemba Mosi, kama njia ya kupinga vitu walivyoviita ni udikteta kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambaye pia ndio Amri Jeshi Mkuu wa nchi yetu.
Ukiangalia kwa haraka utagundua kuwa lolote linalosemwa na rais ni agizo kwa watu wa chini. Ni wazi vyama vya upinzani, ama Chadema mahitaji yao yatakwama.

Yatakwama kama wataendelea kutumia nguvu badala ya kuweka busara kwa faida ya nchi, ukizingatia kuwa siasa yoyote iwe ya upinzani au chama tawala inategemea uwepo wa nguvu kazi ya wananchi. Watanzania ndio wanaolipa kodi kiasi cha kuvifanya vyama vya siasa vipate ruzuku na kulipwa mishahara wanasiasa wao. Hivyo badala ya kutaka wamwage damu yao, ni bora wakawekewa mfumo mzuri wenye tija ili waendelee kufaidi raha ya uwajibikaji wao.

Ndio maana nasema wapinzani watii mamlaka. Wamtii Dr Magufuli na chama chake. CCM haikujiweka yenyewe madarakani. Imechaguliwa na wananchi wengi kutoka mijini na vijijini, huku wakiamini kuwa mgombea wake, ambaye ni Dr Magufuli ataivusha nchi yetu salama. Dalili njema zinaonekana. Utendaji wa Rais Magufuli na safu yake yote imeonyesha wazi kuwa nchi yetu itapiga hatua kubwa kimaendeleo. Tuitunze amani yetu. Watanzania tuwe makini na matamko ya wanasiasa mfano wa Mbowe na wenzake kwa sababu hayana nia njema.
Wakisema tuwasikilize lakini tuyachuje maneno yao kabla ya kuwafuata kikondoo ili tusiiweke nchi yetu rehani. Nchi yetu ina kila zuri linaloweza kuifanya iwe tajiri. Lakini hilo zuri haliwezi kupatikana kama hakuna amani.

Amani inayotaka kuchezewa na wanasiasa hawa wanaotegemea damu ya wananchi kama msingi wa maendeleo yao kisiasa na vyama vyao. Vyama vingi vya siasa havijaanzishwa ili vilete uhasama, chuki na vita kwa wananchi, ila kusaidia kuikosoa na kuishauri serikali ili viharakishe maendeleo yaliyokusudiwa kwa nchi yetu. Japo nao wana ndoto za kuishika dola, lakini zipo njia nzuri ambazo kutokana na uongozi wao, washauri wao wanaweza kukaa na kutafakari njia bora na kuacha njia ya mkato kwa sababu hazitawasaidia wananchi wao.

Si Dr Magufuli tu, ila hata angekuwa nani, asingekubali kuona kuna kikundi cha watu kinataka kutibua uongozi wake, hivyo lazima atakishughulikia tu. Inawezekana Dr Magufuli ni dekteta kama wasemavyo wapinzani, lakini hakuna sehemu nzuri ya kupambana naye hadi maandamano? Mbona lipo Bunge? Bunge ambalo tumeshuhudia hao hao wapinzani wakitoka nje mara nyingi kuliko siku walizokaa ndani katika mijadala mbalimbali. Sasa kama wanakimbia ndani ya jengo lenye kazi ya kutunga sheria (Bunge) na wao wakiwa ndio watungaji wenyewe wa sheria, huku mtaani maandamano yatasaidia kitu gani?

Ni bora wapinzani wakafahamu kwamba; nchi yetu Tanzania ina mahitaji mengi kuliko hata kujua kuwa Dr Magufuli ni dekteta au la kama wasemavyo. Ila sisi wananchi tunajua nchi yetu sasa imenyooka. Hakuna mtumishi mwenye sauti kuliko mwananchi. Wananchi tunahitaji afya bora, dawa ziwepo mahospitalini, tunaziona, watumishi hewa wanaendelea kutimuliwa, wawekezaji wanaotesa wananchi wanashughulikiwa, bajeti bora imetengwa ili kuifanya nchi yetu isonge mbele. Nini tena tunahitaji? Kuna njia moja nyeti ambayo wabunge, madiwani na baadhi ya mameya wa upinzani wanapaswa kuipita na si nyingine, haiwezi kuwavusha. Njia yenyewe ni kushirikiana na serikali kusimamia maendeleo katika maeneo yao katika kipindi hiki, kuliko kusimamia ajenda ya vurugu na machafuko katika nchi yetu.

Mameya wawasimamie madiwani na wakurugenzi bila kusahau wabunge, maana ndio kusudio la wananchi kuwachagua kama viongozi wao halali kwa kipindi cha miaka mitano, sanjari na kupinga rushwa na ufisadi kwa vitendo maana ndio unaokwamisha maendeleo ya nchi yetu. Unaweza ukajiuliza mengi juu ya malalamiko ya wapinzani, mwisho wa siku ukajiona ni mjinga. Angalia, jana Mahakama Kuu ya Tanzania iliyokaa Morogoro imetupilia mbali kesi za kupinga matokeo ya ubunge wa majimbo mawili ya Kilombero na Mlimba, iliyofunguliwa na wagombea wa CCM, dhidi ya wabunge wa Chadema.

Katika kesi hiyo, aliyekuwa mgombea ubunge wa CCM jimbo la Kilombero, Abubakary Assenga, alipinga matokeo ya ushindi wa mgombea wa Chadema, Peter Lijualikali kwa madai kuwa alitumia lugha za kashfa, huku Godwin Kunambi naye akipinga matokeo ya mbunge Susanne Kiwango wa jimbo la Mlimba kwa madai ya kutoridhishwa na kampeni za mbunge huyo. Bado najiuliza, inakuwaje Dr Magufuli ni rais wa Tanzania, anashindwa kutumia udikteta wake kuwapoka wabunge wote wa upinzani ambao wamewekewa pingamizi mahakamani kutoka kwa wanachama wa CCM kama wapinzani wanavyoeneza sumu hiyo ya udikteta ya rais kipenzi cha Watanzania wote?

Badala yake rais amekuwa kimya, akisuhubiri ama kuheshimu uamuzi wa mahakama. Waswahili wana msemo wao; ukiwa mwongo, usiwe msahaulifu. Mbali na kuendesha siasa zenye kuhitaji damu za Watanzania zimwagike, bado wapinzani pia wana sifa mbaya ya uongo na usahaulifu. Lakini kwanini tusikubali tu kuwa huu ni muda wa kazi? Hivi vikao vya maandamano na malalamiko hatuoni vinachukua muda wetu mwingi wa kuipatia maendeleo nchi yetu? Kwanini vyama vya siasa vyote visivae viatu vya kuhamasisha uwajibikaji, usisimamiaji na mikakati ya kuipatia nchi yetu maendeleo badala ya kuwaza vurugu na ghasia?

Inawezekana upeo wangu wa kufikiri ni mdogo, lakini pia sitaki kuamini kuwa serikali halali iliyochaguliwa na wananchi wengi, inaweza kukubali kikundi cha watu wachache waandamane hata wasiporuhusiwa na vyombo vya ulinzi na usalama. Ndio kusema wenye mamlaka na ulinzi na usalama watajidhatiti si tu watu hao waandamane, bali pia itasambaratisha hata mkusanyiko wao, jambo linaloweza kuhatarisha usalama wa wananchi wengine wasiokuwa na hatia. Kamwe tusikubali vurugu. Tusikubali maandamano batili.
Chadema wanataka nini? Na kwa faida ya nani?

Ndio maana nawataka Watanzania tuwapuuze kwa nguvu zote wanasiasa wenye mlengo usiokuwa na tija, wanaotaka nchi yetu iwe kiota cha vurugu badala ya amani, kama Dunia inavyotambua kwa sifa yetu hiyo inayovutia wengi duniani.
Simu 0712 053949 au barua pepe


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...