https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Friday, November 16, 2012

Mtaalamu wa urembo mwenye ndoto lukuki




 Mrembo anavyoonekana baada ya kutengenezwa nywele zake na Salumu Mwombeki

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam
KILA kitu kinahitaji mipango kama kweli dhamira ni kukiletea maendeleo na kutambulika pia kwa jamii mbalimbali.

Wakati hao yapo kwenye sekta zote zikiwamo za sanaa, hata kwenye nyanja ya urembo huko nako ni kawaida.

Ili sekta hiyo iweze kupiga hatua na kufanya kazi kwa mafanikio makubwa, ni wazi juhudi zinahitajika pamoja na mipango kwa jamii husika.

 Salumu Abdallah Mwombeki akiwa kazini kwake.

Katika mazungumzo yaliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita, Salum Abdallah Mwombeki, ambaye ni mtaalamu wa upambaji na mitindo kwa akina mama, anamiliki saluni yake maeneo ya Tabata Chama.

Jina la kijana huyo limeenea kwa kiasi kikubwa katika mtaa huo kutokana na umati wa watu kujaa katika saluni kwa ajili ya kujilemba, ukizingatia kijana huyo kwa mikono yake, ana uwezo wa kuifanya kazi hiyo kwa ufanisi.

“Nashukuru Mungu nimezidi kujipatia mafanikio makubwa kutokana na kuweza kuwamudu vyema kuwalemba akina mama, kuanzia kubuni mavazi ya kuvaa kwa wakati husika, hasa harusi na mengineyo.

“Pia wateja wangu wakija huwashauri mitindo ya kuwasuka kulingana na aina ya vichwa vyao, nikiwa na lengo la kuwapendezesha na kuwafanya waendelee kufanya kazi na mimi, ukizingatia kwamba kazi hii ni kipaji changu,” alisema.

Salum anasema katika kazi hiyo, watu wengi bila kuangalia hadhi na majina yao wamekuwa wakimtafuta kwa ajili ya kufanya kazi nae, jambo ambalo linamfanya aamini atafanikisha mipango ya kufanya kazi hiyo kwa mafanukio makubwa.

Kijana huyo anasema mipango yake ya baadaye ni kupanua biashara zake hizo za saluni ya kike, huku akipanga kumiliki saluni iliyotengenezwa maalum katika gari kubwa na kupaki mahali popote na kuwahudumia wateja wake.

Anasema gari hilo linaweza kuwekewa ratiba ya kuzunguukia maeneo mbalimbali, yakiwamo ya mikoani na kuwapa nafasi watu mbalimbali kuipata huduma yake bila kuangalia wapo mahali gani na wana kipato cha aina gani.

“Kwa mfano gari linaweza kusafiri hadi Mwanza, Arusha, Tanga, Dodoma na kupaki pembeni kwa ajili ya kuwapatia huduma hiyo watu ambao huenda walikuwa wakikosa fursa hiyo kwasababu ya makazi yake kuwa Dar es Salaam,” alisema Salum.

Kijana huyo anasema kwamba saluni yake hadi sasa inafikia mtaji wa Shilingi Milioni 15, ikiwa na vitu vya kila aina vinavyohusu mambo ya urembo wa akina mama.

Anasema mtu anapoingia hapo, hujikuta amebadilika kwa kutengenezwa vizuri nywele zake kwa mitindo ya aina mbalimbali anayoitaka mwenyewe.

Salumu aliyezaliwa miaka kadhaa iliyopita, anasema utundu wa kupamba maharusi, usukaji wa nywele za aina mbalimbali ameupata kutoka kwa Mungu, ingawa anaamini kuwa kipaji cha mama yake mzazi, Madina Nuru, pia kimechangia.

Anasema mama yake alikuwa mjuzi wa usukaji wa vitu mbalimbali, ikiwamo mikeka, jambo ambalo hata yeye limempa mwangaza huo, ambao leo unamfanya aweze kuishi vizuri kwa kutumia kichwa na viungo vyake vya mwili, hasa mikono.

Anasema katika ujuzi wake huo kwenye saluni yake, anashonea nywele za bandia, usukaji wa rasta na mitindo mbalimbali inayotamba au kubuni mingine kwa ajili ya kuwapendezesha zaidi wateja wake wanaofuata huduma yao.

Anasema awali, mwaka 2002 alikuwa akijishughulisha na biashara za kuuza nywele za akina mama, lakini duka lake lilikufa lilipovunjwa na wezi hivyo kumrudisha kutoka hatua kubwa ya kibiashara aliyokuwa nayo.

Jambo hilo lilimfanya aanze kuendeleza kipaji chake cha usukaji kwa ajili pia ya kutafuta maisha, ukizingatia kwamba tayari alishagundua uwezo wake.

Salumu anasema changamoto kubwa kwake ni kwa baadhi ya wanaume wasiomuelewa katika kazi yake hiyo, huku wengineo wakiona hana jipya zaidi ya kumendea wake za watu.

“Hapo nyuma niliwekewa mitego ya kila aina, maana wenye wake zao wanajua tuna uhusiano wowote, wakati sio kweli, ila watu wao wanafuata huduma ya urembo.

“Nashukuru maana leo wamenielewa na wengine wananipigia simu kuwawekea oda wake zao, wakiamini kuwa wamegundua mikono yangu inawapendezesha vizuri wake zao ambao naamini saluni yangu ndio chaguo lao,” alisema.

Mipango yake mingine ni kufungua kampuni ya mitindo itakayohusika na mambo mbalimbali yanayohusu medani ya urembo na mitindo hapa nchini.

Katika kutafuta mbinu za kufanya kazi kisasa na kwa mafanikio makubwa, amekuwa mwepesi kutembelea matamasha mbalimbali, pamoja na matukio ya mitindo katika kumbi za starehe na mahoteli.

Hata hivyo, huko haoni lolote, hasa anapogundua watu hao wanafanya kazi kwa kubahatisha, kiasi cha wengineo kuwaharibu hata wateja wao, wakiwamo maharusi wanaoingia katika matukio ya kukumbukwa duniani.

Kwa sasa saluni yake hajaipa jina zaidi ya wateja wake kuambiana wenyewe, huku kituo cha Tabata Chama, kikiwa maarufu kiasi cha kuleta wateja wapya kila baada ya saa chache.

“Saluni yangu sijaipa jina lakini inaleta wateja wapya, maana wanajua kuwa ramani yao ni kupanda magari yanayokwenda Tabata Kimanga na kushuka kituo cha Chama, ambapo hapo hata mtoto mdogo ananijua na kuifahamu saluni yangu.

“Nashukuru kwa dhati, maana Mungu amenipa kukubalika na kuheshimika kwa kazi yangu, ndio maana hata wasaidizi wangu nimewapa mwongozo wa kumuheshimu mteja anayetoka mbali kwa ajili ya kupata huduma zetu,” alisema Salumu.

Mtaalamu huyo anasema kikubwa anachojivunia ni uwezo wake kujua mbinu gani za kusuka nywele za wateja wake na kutoka wakiwa na furaha, huku gharama zake zikiwa ni nafuu na kuwavutia kila mtu, hivyo watu kutoka mbali na kwenda kwenye saluni yake.

Anasema makubaliano yote ya ufanyaji kazi wake, hufanywa mtu anapokwenda katika saluni yake kwa ajili ya kufanya naye kazi. Salumu anamaliza kwa kuitaka jamii kujua kuwa kazi hiyo ni nzuri na isifikiriwe vyovyote tofauti.

Anasema badala ya vijana kufanya kazi ambazo hazina maadili kwa jamii yake, kuna haja ya kuungwa mkono kwa wale wanaoamua kutafuta riziki kwa njia nzuri kama anavyofanya yeye, huku akiwa na malengo makubwa duniani.

Anamaliza kwa kuwataka watu wanaojihusisha na kazi hiyo ya saluni, kutengeneza nywele na mengineyo kuwa wepesi kujifunza na kufuata ushauri wa waliowazidi kiufundi na kipaji cha ufanyaji kazi ili iwe njia yao ya mafanikio.

Makala haya yameandikwa na Kambi Mbwana.

0712 053949
0753 806087

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...