https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, September 26, 2011

Zifanyie kazi kasoro zako muungwana

KARIBU kwenye ulingo huu wa mambo ya malavidavi huku tukiwekana sawa katika vitu hivyo vitamu kunoga. Katika mfululizo wa kona hii, msomaji utapata habari nzuri zinazohusu uhusiano na maisha.
 
Nia ni kuwekana sawa, ukizingatia kuwa hakuna aliyekamilika hapa chini ya jua. Nikiwa kama muungwana nashukuru kwa kila anayeguswa na kazi zangu, ikiwamo hii inayoelezea mambo ya kimapenzi.
 
Naamini hali hiyo inanipa changamoto na ushawishi wa kuendelea kuwa pamoja kila wiki, katika dhana ya kuiendeleza kona hii.
 
Ndugu msomaji wangu, lazima ujuwe wewe ni nani na upo vipi katika jamii. Nasema hivyo, huku nikiwa muwazi kabisa kwako, kwamba fanyia kazi kasoro zako.
 
Jiangalie mara mbili mbili kwa nia ya kubaini matatizo yako, ili unapokuwa na mtu wako umfanyie yale unayohisi kuwa atavutiwa nayo.
 
Wapo watu wanaojifanya wao ndio kila kitu. Licha ya kukera sana wenzao kwa sababu moja ama nyingine, ila wanabaki kimya, kama wao ni wafalme.
 
Hiyo ni mbaya mno. Kwani wale wanaokosewa kwa makusudi na watu wao, huwa nafasi yao kutafuta sehemu nyingine zenye utulivu.
 
Si ameshakujua ulivyo? Ameshajua wewe ni wa moja tu, huwezi kuvaa kumi moja, hivyo lazima afanye ya kuweza kumpa amani moyoni mwake.
 
Kwa siku kadhaa sasa nimekuwa nikipata maoni ya aina mbalimbali, jambo linalonifanya nizame kutoa mada zinazotoa majibu kwa wale wapenzi haswa wa kona hii inayokujia kila Jumamosi.
 
Wapo watu ambao licha ya kuwa na kasumba zinazowakera watu wapenzi wao, ila wamekuwa kimya kabisa. Wanachofanya wao ni kujiweka karibu na vitu vya kileo, kama luninga, manukato ya aina aina bila kujua kuwa hali zao kihusiano ni mbaya.
 
Lazima uwe makini ndugu yangu. Unaweza kuishi vizuri bila tatizo lolote, endapo uhusiano wako utakuwa umetulia. Na kwa bahati mbaya, hakuna mwingine wa kuuweka sawa zaidi yako mwenyewe.
 
Kwa mikono yako unaweza kujenga nyumba yako na pia kuimoboa kwa mikono yako mwenyewe. Kuwa na uchungu wa kweli msomaji wangu.
 
Kwanini? Jivuwe gamba leo na uape kuishi vema na mwenziwako ili mfurahie ndoa yenu au uhusiano wenu. Nasema hivyo nikiamini kuwa wengi wanavunja uhusiano wao kwa tabia zao za ajabu.
 
Wanashindwa kujiweka sawa na kuona huruma nafasi za wenzao, kitu kinachotakiwa hekima kubwa. Kutojitambua ni kupoteza muda wa mwenzako.
 
Unajua fika unachofanya hakiwezi kumfurahisha mwenzako zaidi ya kumchukiza. Faida ya chuki ni kusambaratisha maana hakuna anayeweza kuishi na mtu ambaye amejaa kasumba za kila aina.
 
Huu ni wakati wako wa kujifanyia marekebisho, maana unachofanya ni kujiharibia wewe mwenyewe. Angalia yote utendayo kwa faida ya uhusiano wako.
 
Kama hufahamu kasoro zako jaribu kumshirikisha mwenzako kwa faida yenu. Sidhani kama anaweza kuwa kimya bila kukwambia ukweli wakati hana amani na kasumba zako za kila siku ya Mungu.
 
Mapenzi hapo ndipo huzaa utamu wake. Kwanza kujitambua na kujifanyia marekebisho kwa faida yenu wote, maana bila hivyo ni hatari kubwa.
 
Angalia kwa makini na kuufanyia kazi urembo wako, maana haitakuwa picha nzuri kuharibu ulipokuwapo sasa, ukizingatia kuwa huko utakapokwenda kunaweza kuwa kubaya kupita kiasi, hivyo kujisumbua.
 
Hapo unapopendwa ndio pakushika kwa nguvu zote, ila tu, ukiwa makini na kuficha nyufa zinazoweza kujitokeza wakati wowote unapobaini mapungufu yako.

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...