https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, September 28, 2011

Mawazo mgando yanawasumbua wasanii wetu

Wasanii wa Tanzania wanatakiwa wafuate nyayo za wenzao kama hawa wa Dikakapa Traditional Dance wenye maskani yao nchini Botswana.

Juu kabisa msanii Rehema Chalamila, maarufu kwa jina la Ray C akiwa katika pozi.



 Juma Nature akiwa jukwaani. Msanii kama huyu anatakiwa awe makini ili aweze kufikia malengo ya kuwa nyota kama wengine wanavyowika duniani.




 
 

NIMEKUWA makini mno kufuatilia maisha ya wasanii wetu nchini na kujua mambo mengi yanayowahusu kila uchwao. Nafanya hivi maana ni mdau na mwenye kupenda zaidi kazi zao kila siku ya Mungu.
 
Katika hilo , mengi nimeyaona na kuyaacha kama yalivyo. Najua kabla ya kuyaacha yapite, huwa kwenye wakati mgumu kusumbua akili yangu nikitaka wafanye lile na kuaacha hili, hata hivyo mwisho wa siku wao ndio wahusika wakuu.
 
Hata hivyo katika hili siwezi kuliacha mara baada ya kuling’amua siku chache baada ya kumaliza uchunguzi wangu kwa wasanii mbalimbali hasa wa muziki wa Bongo Fleva, wanaotamba kwa muda zaidi ya bigijii.
 
Huo ndio ukweli, maana ni makosa na yanatakuwa yafanyiwe kazi kwa faida yao , ukizingatia kuwa supu inanywewa ikiwa ya moto. Sasa naanza. Wasanii wa Bongo fleva wana kasumba kuwa boashara wanayoweza kuifanya ni kuuza nguo.
 
Yani mara baada ya kupata kajina kadogo, hutafuta flemu ya duka na kufungua sehemu ya kuuza nguo. Ni biashara nzuri pia, ila inaishia hapo hapo au nini malengo yao ? Hivi biashara ni kuuza nguo peke yao ?
 
Mbona biashara ni nyingi mno zinazoweza kufanywa na vijana hao wanaona sanaa ndio maisha yao na hawawezi kuishi bila kuwa kwenye kundi hilo ? Hapa lazima tufanye jambo.
 
Ni wasanii wengi wanaofanya kazi hiyo japo kuwa maduka hayo hufa maara baada ya wao kupotea katika ramani ya sanaa, hivyo kuonyesha kuwa hawakuwa na malengo ya aina yoyote katika kufungua biashara hiyo, zaidi ya kupoteza muda.
 
Sitaki nionekane tofauti hapo, maana haya ni mawazo yangu nikitaka wasanii hao wafike mbali zaidi kuliko kupoteza muda wao. Kwa bahati mbaya aina yao ya sanaa ni ya siku tatu na kupotea kabisa.
 
Maisha yao huwa magumu mno wanapofilisika kisanaa hivyo kusumbua ndugu na marafiki zao, wakitaka wapewe msaada kimaisha. Ni wengi japo kuwa ni ngumu kuwataja maana hawakawii kupayuka wakisema wameharibiwa majina yao .
 
Hapa hakuna kufichana, japo kuwa tunaheshimiana, ukizingatia kuwa nia ni kuwafanya wasanii hao wafike mbali zaidi. Ipo haja ya wasanii hao kukaa chini na kuangalia biashara za kufanya, ikiwamo zile zenye tofauti na mavazi.
 
Nasema hivyo kwasababu biashara zipo nyingi kama wamejipanga na kuumiza vichwa vyao kwa ajili ya  maisha yao . Angalia msanii Judithi Wambura maarufu kama Lady Jay D. Huyu ni msanii aliyefika mbali zaidi kibiashara.
 
Ameweza kufungua vitega uchumi vyake zaidi ya vitatu na kumuingizia kipato kikubwa. Nzuri zaidi, bendi yake nayo inaendelea kufanya vema na kulinda jina la heshima yake. Labda ni kwasababu Jay D yupo na mtu makini, Gadna G Habash.
 
Habash aliweza kuacha kazi yake ya utangazaji Clouds FM kwa nia ya kuambatana na mke wake huyo mwenye uwezo mkubwa kisanaa. Sawa, ila nadhani hata mwanadada huyo pia anashaulika, kitu kinachompatia maendeleo.
 
Vipi hawa wengine? Je, hawana watu wa kuwaongoza kwa faida yao ? Jibu wapo wengi tu, ila mawazo yao nahisi ni ya kupelekena katika majumba ya starehe wakikata kilaji kwa raha zao, maana wanasema maisha yenyewe kimini.
 
Haya ni mawazo mgando. Nasema hivyo maana pesa inayotoka bila kuingia kamwe haiwezi kukaa muda mrefu. Nadhani huu ni wakati wa wasanii hao kukaa na kuangalia aina yao ya maisha kwa faida yao wenyewe.
 
Napenda kuona wasanii hao wakipiga hatua kubwa kimaisha, maana majina yao ni tofauti na maisha yao baada ya muda mchache. Kwanini kila msanii aone biashara ni ya kuuza nguo. Tena duka moja, lililozunguukwa na mangine?
 
Huo ni upungufu mkubwa. Jina la Ahmad Ally Madee ni kubwa ndio, ila linaweza kumuingizia fedha nyingi kwa kubuni biashara yenye tija. Wapo wengi, ila sidhani kama inaweza kuwa chachu yao ya kupiga hatua na kuishi maisha mazuri, kama watafungua vijibiashara vya kupoteza muda, kama wanavyofanya sasa.
 
Wakati ndio huu. Kaeni chini muangalie aina yenu ya maisha. Uvivu wa kufikiria usiwafanye mfe maskini, hali ya kuwa mngekuwa matajiri hata kama kuna kasumba ya kuibiwa kazi zenu, maana hao mnaowata wadosi hawawezi kuingia hadi kwenye biashara zenu.
 
Zindukeni kwa faida yenu wenyewe.
0712 053949
0753 806087



No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...