https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Wednesday, November 02, 2016

Watoto walivyojiachia kwenye ‘party’ ya Bayport Kibaha

Afisa Mtendaji Mkuu wa Bayport Financial Services, John Mbaga, akizungumza jambo katika sherehe za Siku ya Familia ya wana Bayport waliosherekea pamoja na watoto wao pamoja na watoto wanaolelewa na kituo  cha Kibaha Children Village Centre (KCVC), mwishoni mwa wiki iliyopita. 

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
TAASISI ya Kifedha ya Bayport Financial Services inayojihusisha na mikopo, iliwaacha watoto hoi mwishoni mwa wiki baada ya kuandaa sherehe maalum kwa ajili ya wafanyakazi wa tasisi hiyo pamoja na watoto wao kufurahia pamoja na watoto wenzao wanaolelewa na kituo cha Kibaha Children Village Center (KCVC), wilayani Kibaha, mkoani Pwani.

Sherehe hizo zilianza asubuhi na kumalizika jioni ambapo tukio hilo liliongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa Bayport, John Mbaga, pamoja na mlezi wa Kituo hicho ambaye ni mke wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa.
Baadhi ya watoto wakipata chakula cha mchana katika party hiyo ya Bayport Kibaha.
Baadhi ya michezo waliyocheza watoto hao ni kubembea, kucheza muziki, kupewa burudani ya mazingaombwe sanjari na nyinginezo nyingi zilizowaburudisha na kuwafurahisha.

Akizungumza katika salamu za ukaribisho kwenye kituo hicho, mlezi wa KCVC, Mama Anna Mkapa, alisema amefurahishwa na ujio wa Bayport na watoto wao kwenda kufanya sherehe maalum ya kuonyesha upendo na ukarimu kwa watoto wanaoishi na kulelewa na kituo hicho.

“Siwezi kusema mengi kutokana na ujio wenu badala yake niwakaribishe tu nyie na watoto wenu ili wote tufarahi pamoja hususan watoto ambao ndio msingi madhubuti wa kutukutanisha hapa,” alisema Mama Anna Mkapa.
Zilikuwa ni shangwe kutwa nzima kutoka kwa wafanyakazi wa Bayport na watoto.
Akizungumzia sherehe hizo mwishoni mwa wiki, Afisa Mtendaji Mkuu wa Bayport Financial Services, John Mbaga, alisema wamejisikia faraja kubwa kufurahi pamoja na watoto wote waliokuwapo kwenye sherehe za wana familia wa Bayport, wakiamini kuwa wametumia wakati huo kubadilishana mawazo na kuwapa watoto haki ya kupendwa.
Katika wakati wote wa burudani hizo, watoto hao walionekana kufurahia zaidi uandaaji wa tukio hilo lililotanguliwa na wimbo wa ukaribisho ulioimbwa na watoto hao mara baada ya wageni kutoka jijini Dar es Salaam kuanza kuingia katika maeneo ya kituo hicho.

Mlezi wa kituo cha KCVC, Mama Anna Mkapa, akisalimia wafanyakazi na watoto katika sherehe za familia zilizofanyika mwishoni mwa wiki.

“Nimefurahishwa sana na jinsi tulivyoshiriki katika sherehe hizi za familia, zaidi kuona watoto wetu wana furaha kubwa nikiamini kwamba utaratibu huu utatumiwa na watu wote kutenga muda mahususi kwa ajili ya kukutana na kujumuika pamoja na watoto wao pamoja na wale wanaoishi katika vituo kama hivi kwa sababu wote wana haki ya kupendwa.

“Si mimi tu, bali nina uhakika wafanyakazi wote wa Bayport tumefarijika kwa kufurahia pamoja siku ya familia ya wana Bayport kufurahia siku nzima na watoto wetu wanaolelewa na kituo hiki cha KCVC kwa sababu nao kama tulivyowaona wamefurahishwa pia,” alisema.

 Naye Meneja Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Ngula Cheyo, alisema ni jambo la kujivunia mno kupata nafasi ya kuburudika na watoto, akiamini kuwa taasisi yao ina kila sababu ya kuishi karibu na jamii kutokana na kuungwa mkono na Watanzania wote.

“Bayport imeanzishwa nchini Tanzania tangu mwaka 2006 na imekuwa ikiungwa mkono kwa kiasi kikubwa na Watanzania, hivyo tutaendelea kuwa karibu na jamii kwa kushiriki mambo mbalimbali yenye tija na yenye kujenga ushirikiano sahihi kwa watu wote,” Alisema Cheyo na kusema kuwa wana matawi 83 katika wilaya na mikoa ya Tanzania Bara.


Mbali na mikopo ya fedha isiyokuwa na amana wala dhamana inayotolewa na taasisi hiyo, pia wana huduma ya mikopo ya viwanja katika maeneo mbalimbali kama vile Msakasa (Kilwa), Tundi Songani (Kigamboni), Boko Timiza (Kibaha) na Kimara Ng’ombe (Bagamoyo).

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...