https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Friday, June 09, 2017

Mvua haijazuia kompyuta za Bayport kusambazwa mikoani

Mratibu wa Masoko wa Bayport Financial Services, Mercy Mgongolwa akimkabidhi kompyuta mbili Kaimu Mkurugenzi wa Mbulu, mkoani Manyara, Deogratias Kashasha.


Na Mwandishi Wetu, Mbulu
KWA miezi kadhaa sasa mvua imeendelea kunyesha katika mikoa mbalimbali ya Tanzania, hali inayoonyesha kukidhi kiu ya watu wengi waliokuwa wakiiomba inyeshe katika maeneo yao.

Hata hivyo, licha ya mvua hiyo kunyesha, lakini baadhi ya maeneo imekuwa na matokeo mabaya kutokana na kuezua nyumba, kuharibu miundo mbinu muhimu ikiwamo ya barabara.

Matokeo hayo yameibua changamoto mpya hususan za kufikika kwa urahisi katika maeneo hayo yanayoendelea kukumbwa na mvua kubwa. Mbali na mvua hiyo kunyesha, hata hivyo uwajibikaji unaendelea kufanyika kwa sekta na watu mbalimbali kuendelea na maisha yao ya kila siku ili wakuze uchumi.
Zoezi la kutoa msaada wa kompyuta lilivyokuwa linaendelea katika mikoa mbalimbali ya Tanzania.


Licha ya maeneo mengi kukumbwa na mvua, lakini Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services imeendelea na usambazaji wa kompyuta katika ofisi za serikali mikoani kama ilivyozindua utaratibu huo mwishoni mwa mwaka jana.

Bayport ambayo ni Taasisi ya Kifedha inayojihusisha na mikopo ya fedha, mwaka jana ilianzisha mpango wa kusambaza kompyuta kwenye ofisi za serikali ambapo tukio la uzinduzi lilihudhuliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angellah Kairuki. Jumla ya kompyuta ambazo Bayport iliamua kuzisambaza kwa serikali ni 205, ambapo tayari maeneo mbalimbali wamefikiwa na kompyuta hizo kwa ajili ya kupunguza changamoto ya vifaa vya ofisi.

Akizungumza katika usambazaji wa kompyuta kwenye mikoa ya Singida, Manyara, Iringa, Songwe na Ruvuma, Mratibu wa Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Mercy Mgongolwa, anasema licha ya mvua kubwa kupiga, lakini wameendelea na zoezi lao la kuhakikisha wanafikisha msaada wa kompyuta.

Anasema kufikisha kompyuta hizo ni sehemu ya kushirikiana vizuri na ofisi za umma katika mikoa ya Tanzania ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi, ukizingatia kuwa baadhi ya ofisi zimekuwa na tatizo la kukosa huduma muhimu za kompyuta.
“Hatujaangalia mvua kubwa inayonyesha katika nchi yetu kwa muda mrefu sasa, badala yake tuliendelea na zoezi letu zuri la kufikisha kompyuta katika ofisi za umma kama tulivyopewa mpangilio mzuri na Wizara ya Utumishi mwaka jana.

“Ukiacha maeneo tuliyosambaza kompyuta kwa hatua ya awali, msimu huu wa mvua pekee tumefikisha vifaa hivi katika maeneo ya Mbulu (Manyara), Kilolo (Iringa), Kondoa, Mbinga (Ruvuma), Songwe na Busokelo mkoani Mbeya ambapo kila ofisi ya Umma iliyopangwa kupokea msaada huo ilipokea kompyuta mbili,” Alisema Mercy.

Mratibu huyo wa Masoko wa Bayport anasema kwamba ulimwengu umebadilika kutokana na mahitaji makubwa ya sayansi na teknolojia, hivyo wazo la kutoa msaada wa kompyuta limekuja wakati muafaka, akiamini kuwa litapunguza changamoto ya utendaji hafifu wa watumishi wa umma waliokuwa wanakabiliwa na uhaba wa kompyuta.

Anayataja maeneo mengine ya nchi ambayo yamepokea kompyuta zao ni pamoja na Arusha, Kilimanjaro, Morogoro, Mbeya, Mwanza na Bukoba, huku wakijipanga kwa maeneo mengine yaliyopangwa wafikishiwe msaada huo haraka ambapo ukiacha kompyuta 125 zilizobakia Utumishi, nyingine 80 zinaendelea kusambazwa katika mikoa mbalimbali ya Tanzania.

“Ni matumaini yetu kuwa watumishi wa umma watatoa huduma bora kwa wananchi wao kwa kupitia msaada wa kompyuta tunaotoa kwa ofisi serikali kama tulivyoelekezwa na serikali tulivyopeleka wazo la kutoa msaada wa kompyuta 205 zenye thamani ya Sh Milioni 500,” Alisema Mercy.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbulu, mkoani Manyara, Deogratias Kashasha, anasema msaada wa kompyuta mbili waliyopokea kutoka Bayport umekuja wakati muafaka, hivyo ni wajibu wao kufanya kazi kwa bidii kwa kuzitumia vyema mashine hizo.

“Wenzetu wa Bayport wamefanya jambo sahihi kwa sababu wametuletea msaada wa kompyuta ambazo kwa hakika zitatusaidia kwa namna moja ama nyingine kutoa huduma bora kwa Watanzania kwa kupitia ofisi zetu.

“Dunia ya leo inahitaji matumizi makubwa ya kompyuta kwa mambo mengi, hivyo wakati tunashukuru kwa msaada huu, niwahakikishie kwamba zitarahisisha utendaji kazi kwa watumishi wetu kulingana na matumizi tutakayojipangia,” Alisema Kaimu huyo Mkurugenzi wakati anapokea kompyuta hizo hivi karibuni ofisini kwake.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Singida, Rashid M.Mandoa Anasema kwamba ni jambo la kutia moyo kuona taasisi ya Bayport imeamua kujitoa vyema kusaidia wadau wao kuwasaidia vifaa vya kiutendaji vya kompyuta ambazo ni muhimu.

Anasema hakuna asiyejua umuhimu wa kompyuta kwa mambo mengi kama vile kuweka rekodi mbalimbali za kiofisi, kuunganisha mawasiliano ya kiofisi au hata kuweka urahisi wa kumbukumbu katika maeneo mengi hali inayoweza kurahisisha.

“Tumepokea msaada huu wa kompyuta mbili kutoka kwa Bayport likiwa ni wazo zuri lililoanzishwa mwaka jana tulipoona linazinduliwa pia na ofisi ya Utumishi wa Umma kwa minajiri ya kuorodesha maeneo yatakayofikiwa, huku wilaya yetu ikiwa miongoni mwao.

“Hakika tunashukuru kwa msaada huu na kwa kiasi kikubwa utatusaidia kuwahudumia wana Singida ambao kwa  namna moja ama nyingine wana uhitaji mkubwa wa huduma bora kutoka kwenye serikali yao ya Hapa Kazi tu,” Alisema huku akishuhudiwa na Meneja wa Bayport mkoani Singida Awali Chaula.

Halmashauri ya Kilolo mkoani Iringa, Mkurugenzi wake Violet Issacka Hakuwa nyuma kuwapongeza Bayport akiwataka waendelee kushirikiana naye katika kuwakomboa na kuwahudumia wananchi kwa kupitia sekta mbalimbali za kimaendeleo.

“Ni bahati kubwa kufikiwa na msaada huu kwa sababu tunaamini si kila Halmashauri ya Tanzania inaweza kupata msaada wa kompyuta kutoka kwenye taasisi ya Bayport Financial Services.

“Tufanya kazi kwa bidii na tunaomba Bayport muendelee kushirikiana na sisi kwa mambo mengine ya kimaendeleo, tukiamini kuwa uwezo huo mnao kutokana na kuguswa kwenu kwa mambo mengi ya kijamii mnayoendelea kuyafanya kila siku,” Alisema.

Bayport ni miongoni mwa taasisi zinazojitolea kwenye jamii kwa mambo mengi, huku mwaka jana wakifanya sherehe kubwa za kutimiza miaka 10 ya huduma zao za mikopo sanjari na kujitolea kwenye jamii kwa mambo mengi.



No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...