https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, August 08, 2016

Salasala sasa yapata mwarobaini wa maji

Meneja wa mkoa wa Dawasco -Tegeta Alpha Ambokile akizungumza na wakazi wa mtaa wa Upendo Salasala jijini Dar es Salaam ambao wameanza kupata huduma ya maji safi katika maeneo yao. 
Na Dixon Busagaga wa Michuzi blog.

WANANCHI zaidi ya 265 wa mtaa wa Upendo, Mbezi Salasala wilayani Kinondoni wamelishukuru Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASCO), kwa kuwafikishia huduma ya Majisafi waliyoipatia shida kwa zaidi ya miaka 10 iliyopita. 

Akizungumza wakati wa mkutano wa pamoja wa serikali za mitaa na DAWASCO, Mjumbe wa mtaa wa Upendo Bw. Robert Massawe amepongeza juhudi zilizofanywa na Dawasco za kuwapatia huduma ya Maji wananchi wa eneo lake na kwamba juhudi hizo zinaendana na kauli ya serikali ya awamu ya tano inayosema hapa kazi tu.


Akieleza historia fupi ya eneo hilo Bw. Massawe alisema tangu watu waanze kuhamia eneo hilo huduma ya Maji ilikuwa ni ya kununua kutoka mtaa mwingine wa mbali ambao ulikuwa umefikiwa na huduma hiyo ya Maji. 
  Bomba likitoa maji katika moja ya mitaa ya Salasala jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wakazi wa Salasala wakimsikiliza Meneja wa Dawasco-Tegeta Alpha Ambokile (hayupo pichani) 
 Hivi ndivyo hali ilivyokuwa kabla ya kuanza kupatikana kwa huduma ya maji katika eneo la Salasala ambapo kwa sasa wakazi wa eneo hilo wanapata huduma ya maji.




“Ilifikia kipindi gharama ya kununua Maji ni kubwa kuliko gharama ya chakula, na wananchi wengi walikuwa wakitumia muda wao mwingi kuhangaika kutafuta Maji jambo ambalo lilikuwa likikwamisha kutekeleza majukumu mengine ya kujenga nchi” alisema Massawe.


Nae mmoja wa wakazi wa eneo hilo, Bi. Sofia alisema; “Kweli DAWASCO imemtua mama ndoo ya Maji kichwani, sisi akina mama ndio tuliokuwa tukiteseka zaidi na suala la Maji, lakini akina mama wa mtaa huu tulijitoa ili kupambana na janga la Maji ambalo lilikuwa likitukabili, na hatimaye tumefanikiwa kupata huduma ya Maji” 


Kwa upande wa Dawasco, Meneja wa Mkoa wa Tegeta, Bw. Alpha Ambokile amewataka wakazi wa mtaa huo kujitokeza kwa wingi kufanya maombi ya kuungiwa huduma ya Maji kwa kuwa tayari huduma hiyo imefika katika makazi yao, baada ya kuhangaika kwa muda mrefu wakisaka huduma hiyo, na ameahidi kuwaunganishia huduma Maji mapema na kwa uharaka zaidi, mara tu baada ya kupokea maombi yao ya kuungiwa huduma.


“Ninawaomba mjitokeze kwa wingi ili kwa pamoja tuweze kuwaunganishia huduma ya Maji, nitawatengea siku yenu maalum ambayo timu yangu ya ufundi itakuja kuwafanyia maunganisho ya Maji, ambao bado hamjafanya maombi, fanyeni haraka ili tuweze kuwaunganishia wote kwa pamoja huduma ya Maji” alisema Ambokile


PICHANI: Sehemu ya wakazi wa mtaa wa Upendo, Mbezi salasala wakiwa na Mjumbe wa mtaa huo, Bw. Robert Massawe (aliyevaa shati ya bluu), wakisikiliza kwa makini katika kikao cha pamoja na uongozi wa Shirika la Maji safi na Majitaka Dar es salaam (DAWASCO) kutoka mkoa wa Tegeta, baada ya mtaa huo kufikiwa na huduma ya Majisafi na salama kwa mara ya kwanza tangu waanze kuhamia katika makazi hayo, jijini Dar es salaam.



No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...