https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, October 10, 2016

Wadau waendelea kuipinga adhabu ya kifo Tanzania


 Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk.Helen Kijo- Bisimba (kushoto), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, wakati akisoma tamko la kupinga adhabu ya kifo. Kulia ni Mkurugenzi wa Uwezeshaji na Uwajibikaji, Imelda Urio na kushoto ni Mkurugenzi wa Utetezi na Maboresho wa LHRC, Anna Henga.

Na Dotto Mwaibale, Dar es Salaam
KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimefungua kesi ya kikatiba kuhusiana na ulinzi wa haki ya kuishi na urekebishwaji wa sheria ya kanuni ya adhabu juu ya ulazima wa kutolewa kwa adhabu ya kifo katika makosa ya uhaini na mauaji.

Kesi hiyo imefunguliwa dhidi ya mwanasheria mkuu wa serikali  wakitaka ufafanuzi zaidi juu ya adhabu ya kifo, wakibainisha kuwa adhabu hiyo haimpi nafasi mtuhumiwa kujirekebisha bali ni ya kulipiza kisasi.
 Mkurugenzi wa Uwezeshaji na Uwajibikaji, Imelda Urio (kulia), akisisitiza jambo kwenye mkutano huo.

Kituo hicho kimesema endapo Tanzania itatekeleza hukumu ya kifo  kwa sasa inamaanisha watu wapatao 228 na zaidi watapoteza maisha yao huku  wengine 244 wanasubiria maamuzi ya rufaa zao.

Akizungumza wakati akitoa tamko la kupinga adhabu ya kifo  Dar es Salaam leo Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Hellen- Kijo Bisimba alisema hadi  mwaka 2015 jumla ya watu 472 walikuwa wamehukumiwa kunyongwa.
 Mkurugenzi wa Utetezi na Maboresho wa LHRC, Anna Henga akizungumza katika mkutano huo.
 Mkutano na waandishi wa habari ukiendelea.
Mkutano na waandishi wa habari ukiendelea.

Alisema kituo kinaiomba serikali kurekebisha sheria ya kanuni ya adhabu na sheria ya ugaidi yenye kutoa adhabu ya kifo kwa makosa ya mauaji, uhaini na ugaidi.

Dk. Bisimba alisema kituo  kina sababu za kupinga adhabu hiyo ya kifo na  hawafurahii watu kuua wengine na ndio maana hawapendi pia hata muuaji auawe.

“Adhabu ya kifo ni vigumu kuhakikisha kuwainatekelezwa tu  kwa wale watu ambao huwezi kuirekebisha kwani mfumo wa utoaji haki huwa pia na mianya ya makosa na hivyo maisha ya mtu yanaweza kupotea bure,” alisema Dk. Bisimba na kuongeza kuwa hakuna ushahidi wowote kuwa adhabu hiyo inaweza kuzuia watu wengine kutokutenda makosa  kama hayo.

Alisema licha ya adhabu  hiyo kutokutekelezwa nchini kwa takriban miaka 22 , taaarifa zinaonesha kuwa watu 72 ambao walishawahi kunyongwa kutokana na adhabu hiyo.

Hata hivyo aliiomba serikali kutengeneza utaratibu wa kuelimisha jamii juu ya kuheshimu haki za binadamu hususani haki zakuishi na kuweka mazingira ya kuiheshimu haki hiyo, pia ibadilishe sheria  kwa kuondoa adhabu ya kifo na kuweka adhabu mbadala kwenye makosa ya jinai na kwa wafungwa waliopo mfano vya muda mrefu  gerezani.


No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...