https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, February 22, 2016

Bayport yazindua miradi sita ya mikopo ya viwanja, serikali yapongeza

Mkurugenzi Mkuu wa Bayport Financial Services, John Mbaga, kulia akizungumza jambo katika uzinduzi wa huduma mpya wa mikopo ya viwanja vinavyotolewa na taasisi yao katika maeneo sita ambayo ni Kilwa, Bagamoyo, Kigamboni, Chalinze, Kibaha na Morogoro. Kulia kwake ni Zahra Moore kutoka kwenye kampuni yao ya BlackWood na Mwanasheria wao Ntiiba Muganga. Picha na Story kwa Hisani ya Bayport Financial Services.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
TAASISI ya Kifedha ya Bayport Financial Services inayojihusisha na mikopo, imezindua miradi sita mipya ya mikopo ya viwanja katika maeneo ya Kibaha, Bagamoyo, Chalinze, Temeke, Kilwa na Morogoro, ikiwa ni mwendelezo wa utoaji huduma bora za viwanja baada ya ule wa Vikuruti kuungwa mkono Watanzania wengi.

Kuzinduliwa kwa huduma hizo mpya za viwanja huku wakiongozwa na Mbunge wa Kigamboni, Faustine Ndugulile, mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya Temeke, Bertha Minga, kunatanua wigo wa urahisishaji wa maisha ya Watanzania, hususan katika suala la ardhi linalozidi kupanda thamani siku hadi siku, jambo linalohitaji juhudi za taasisi kama Bayport za kuwasaidia wananchi wake kupata maeneo ya makazi kwa utaratibu rahisi na nafuu.
Mwakilishi wa Mkuu wa wilaya Temeke, Bi Bertha Minga, aliyesimama akizungumza katika uzinduzi wa hudumaya viwanja inayotolewa na taasisi ya kifedha ya Bayport Financial Services, leo mchana katika Ukumbi wa Ramada Encore, Posta, jijini Dar es Salaam. Anayeshuhudia ni mwanasheria wa Kampuni ya BlackWood, Ntiiba Muganga na Mkurugenzi wa Uzalishaji wa BlackWood Zahra Moore.

Akizungumza katika uzinduzi wa miradi hiyo mipya ya viwanja, Mkurugenzi Mkuu Bayport Financial Services, John Mbaha, alisema huduma zao zitakuwa na njia rahisi kwa ajili ya
kuwawezesha wananchi wote kuchangamkia fursa ya upatikanaji wa viwanja hivyo.
Meneja Masoko na Mawasilianowa Bayport Financial Services, Ngula Cheyo kushoto akibadilishana mawazo na Mwakilishi wa Mkuu wa wilaya Temeke, Bi Bertha Minga.
Mkurugenzi Mkuu wa Bayport Financial Services, Jonh Mbaga, akipiga picha ya pamoja na Mbunge wa Kigamboni, Mheshimiwa Faustine Ndugulile katika uzinduzi wa huduma ya mikopo ya viwanja, uliofanyika leo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni mwakilishi wa Mkuu wa wilaya Temeke, Bi Bertha Minga.
Meneja Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Ngula Cheyo akizungumza katika uzinduzi huo wa huduma ya mikopo ya viwanja.
Meneja Biashara wa Bayport Financial Services, Thabit Mndeme, akimsikiliza kwa makini Mkurugenzi Mkuu wa taasisi yao John Mbaga kulia kwake wakati anazungumza na wageni waalikwa katika uzinduzi wa huduma yao ya mikopo ya viwanja.

Alisema njia hizo ni pamoja na ununuaji wa kiwanja kwa pesa taslimu ambapo mteja anatakiwa kulipia fedha zote za kiwanja kwenye akaunti ya Bayport, kukabidhi nakala za nyaraka za malipo hayo kwenye ofisi za Bayport na kusubiri ndani ya siku 90 ili akabidhiwe hati yake baada ya kukamilisha malipo yote.

“Kwa wateja wa mkopo wa upande wa ujasiriamali na watumishi wa kampuni binafsi, wanatakiwa kulipia malipo ya awali ya mita za mraba walizochagua, huku Bayport ikikamilisha malipo yaliyosalia na wateja hao kupatiwa nyaraka zao baada ya kukamilisha mkopo wao, ambapo thamani ya viwanja hivyo vikianzia sh Sh 550,000,” Alisema  Mbaga.

Naye Meneja Biashara wa Bayport Financial Services, Thabit Mndeme, alisema watumishi wa umma hawatakuwa na gharama za awali, badala yake wakichagua maeneo watakayo, wataingizwa kwenye kundi la mkopo na kutakiwa kulipa mkopo huo kila mwezi kwa kipindi cha miaka mitatu, huku makato yakikadiliwa kuwa Sh 73,684.49 kila mwezi.

“Bado tunaendelea kutanua wigo kwa watu wote kama vile watumishi wa umma, watumishi wa kampuni binafsi, bila kusahau kundi kubwa la wajasiriamali ambalo limeendelea kujumuishwa kwenye miradi yetu ya viwanja, tukiamini gharama ya makato ya kila mwezi ya Sh 102,855 ni rahisi na yanaweza kuwa mkombozi wa maisha ya watu wengi,” alisema Mndeme.

Kwa mujibu wa Mndeme, huduma za viwanja zinapatikana katika maeneo ya Bagamoyo na mita moja za mraba zitauzwa kwa Sh 10,000 tu na (Boko Timiza) Kibaha mita moja za mraba itauzwa kwa Sh 9,000 na (Kibiki na Mpera) Chalinze mita moja za mraba zitauzwa Sh 4500, huku (Tundi Songani) Kigamboni mita moja ya mraba itanunuliwa kwa Sh 10,000 na (Msakasa) Kilwa mita ya mraba itapatikana kwa Sh 2000, bila kusahau (Kiegea) mita moja ya mraba Sh 3500 tu.

Naye Meneja Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Ngula Cheyo, alisema kwamba hakuna Mtanzania atakayelalamika kushindwa kujenga nyuumba, kama watafanyia kazi juhudi za taasisi yao yenye dhamira na malengo makubwa ya kuwakwamua watu wote ili wawe na vitu vya thamani kama vile nyumba na viwanja.

Kwa upande serikali kwa kupitia mwakilishi wa Mkuu wa wilaya Temeke, Bertha Minga, aliitaka Bayport kushirikiana na serikali katika mambo yao hususan ya viwanja ili kuhakikisha kwamba wananchi wanafanikiwa kwa dhati na kuepusha migogoro hususan katika suala zima la hati ambalo ndio muhimu katika mambo yanayohusiana na ardhi.

Naye Mbunge wa Kigamboni Faustine Ndugulile alisema kwamba amefurahishwa mno na huduma ya viwanja vya Bayport sambamba na kuguswa kwa jimbo lake la Kigamboni, jambo linaloweza kuiweka eneo hilo katika nafasi za juu.
Mkurugenzi wa Uzalishaji wa Kampuni ya BlackWood Zahra Moore kushoto akizungumza jambo katika uzinduzi wa huduma ya viwanja ya Bayport Financial Services.
Mwanasheria wa Kampuni ya BlackWood Ntiiba Mungana akizungumza jambo kwenye uzinduzi huo wa huduma ya mikopo ya viwanja.  
Meneja Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Ngula Cheyo, akipiga picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Uzalishaji wa kampuni ya BlackWood, Bi Zahra Moore.

No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...