https://tpc.googlesyndication.com/simgad/8045142562622600543


Recent Post

Monday, May 16, 2016

Maisha Shamba wakusudia kupanda miti milioni 50,000,000

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WADAU wa ardhi, mazingira na mambo ya misitu wanaojulikana kama Maisha Shamba Group wameweka adhma ya kupanda miti milioni 50,000,000 ifikapo mwaka 2020, ikiwa ni mipango yao ya kutunza mazingira na kujikwamua kiuchumi kwa kupitia sekta ya misitu nchini.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, January Makamba, akizungumza jambo katika mkutano wa wanachama wa Maisha Shamba Group wanaojihusisha na mambo ya misitu na mazingira mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.


Hayo yamesemwa na kiongozi mkuu wa group hilo, Asifiwe Malila, alipokuwa akizungumza na wanachama wake katika mkutano wao wa mwaka, huku mgeni rasmi akiwa ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, January Makamba, mwishoni mwa wiki, katika Ukumbi wa Shule ya Sheria Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Mdau wa mambo ya ardhi na misitu, Ally Abdallah, akisikiliza kwa makini hutuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, January Makamba, hayupo pichani katika mkutano wa wadau wa misitu wanaojulikana kama Maisha Shamba Group.


Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, January Makamba, aliwapongeza wadau hao wa mambo ya misitu, akiwataka waendelee kubuni mambo yanayoweza kuwakwamua na kuisaidia nchi katika kutunza mazingira kwa kupitia sekta ya misitu.

Mheshimiwa January Makamba wakati anaingia eneo la Mkutano huo. Kulia kwake ni mdau wa ardhi na misitu, Ally Abdallah.
Akizungumzia adhma hiyo, Malila alisema lengo lao linatokana na kujidhatiti kujikwamua kiuchumi kwa kupitia misitu pamoja na utunzani wa mazingira, huku wanachama wote wa group hilo wakimiliki miti 14,000,000, katika wilaya mbalimbali nchini Tanzania.

Wadau hao wa misitu wakifuatilia mkutano huo kwa umakini.

“Kwa pamoja tuna mipango kabambe ya kuhakikisha kwamba tunajikita zaidi katika kilimo cha miti, mifugo kama njia ya kukuza uchumi wetu, ndio maana tumeamua kuungana kwa pamoja kushirikiana kwa hali na mali katika sekta hii muhimu,” alisema Malila, katika mkutano huo uliokuwa na lengo la kujadili muungano wao huo sanjari na kupitisha rasmi rasimu ya Katiba kama njia ya kusajili jumuiya kwa ajili ya kujiwekea malengo ya juu kisheria.

Mheshimiwa January Makamba akizungumza na wadau hao wa misitu, ardhi na mazingira.


Makamba alisema serikali itashirikiana na wadau hao wa misitukwa nguvu zote, huku akiwataka washirikiane na viongozi wao, wakiwamo wabunge, ikiwa ni hatua nzuri ya wizara yake kujiandaa kupeleka muswada wa mabadiliko ya sheria ya mazingira, kuuboresha mfuko wa Taifa wa Mazingira, sanjari na kuuwekea ubora wa utendaji kazi wake, tangu ulipoanzishwa rasmi nchini Tanzania mwaka 2004.

“Mwaka huu zimetengwa Sh Bilioni 2 kwa ajili ya Mfuko wetu wa Taifa wa Mazingira uweze kufanya kazi, ingawa mahitaji ni zaidi ya sh Bilioni 100, ambapo tunajaribu kutafuta mbinu za kuweza kuzipata fedha hizo kwa sababu mazingira ni jambo nyeti duniani kote, hivyo naamini serikali yetu itashirikiana na wadau wote ili nchi yetu ipige hatua.

“Endapo tutakuwa na sera mpya, mabadiliko ya sheria pamoja na fedha, hakika yote tunayokusudia tutayafanya kwa wakati muafaka, sanjari na upandaji wa miti na utunzaji wa mazingira ili sekta hiyo iweze kunufaisha nchi pamoja na wananchi wake, wakiwamo wadau wanaojihusisha na mambo ya mazingira kwa namna moja ama nyingine,” alisema Makamba.


Aidha wanachama hao wa Maisha Shamba Group walitumia muda huo kumuomba Makamba na wizara yake kuweka utaratibu mzuri na rahisi kwa ajili ya wanachama hao wapewe mapori ya serikali ili wayaendeleze, mafanikio yao yarekodiwe, mashamba yao yapimwe na wataalamu wanaopatikana katika maeneo mbalimbali ya Tanzania, ili iwe njia ya kufanikisha adhma yao ya kuhakikisha kwamba sekta hiyo inapiga hatua nchini.





No comments:

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...