Na Oscar Assenga, Muheza
JAMII ya watanzania imehimizwa kujenga utamaduni wa kuchemsha maji ya kunywa na kuyatumia,matumizi ya dawa za kutibu maji ‘water guard’ na matumizi ya vyoo bora utaratibu ulioelezwa kuwa utawasaidia kujiepusha kupatwa na magonjwa ya mlipuko.
 
Meneja wa shirika la PSI mkoani Tanga,Geofrey Mwankenja alitoa rai hiyo juzi kwenye maadhimisho ya siku ya kunawa mikono duniani,utumiaji wa vyoo bora na uzinduzi wa kampeni ya usafi wa mazingira ambapo kimkoa ilikuwa kata ya Mhamba huko Muheza.
 
Akiwahutubia wakazi kata hiyo ya Mhamba,Mwankenja alisema ili watu wengi hususani wale wanaoishi maeneo ya vijijini kuweze kunusurika  kupata magonjwa ya mlipuko ni vyema wananchi wakachukua tahadhari kwa kuchemsha maji kabla ya kutaka kuyatumia.
Mwankenja alisema kuwa taratibu zote za kiafya zikizingatiwa ni dhahiri kuwa wananchi wengi wataepuka adui maradhi kama yale ya mlipuko ambapo aliwasisitiza wakazi wa Mhamba kunawa mikono kwa sabuni pindi wanapotoka maliwato kujisaidia hatua aliyoieleza kuwa itasaidia kuokoa maisha ya watanzania waliowengi hususani watoto.